Tuesday, February 28, 2017

WAZIRI NAPE AWATANGAZA ALIKIBA NA DIAMOND KWEMO KATIKA KAMATI YA HAMASA SERENGETI BOYS


Waziri Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Nape Moses Nnauye (Mb), ametangaza Kamati ya watu 10 watakaohamasisha kuwaunganisha Watanzania kwa pamoja ili kuichangia timu ya Tanzania ya Vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 maarufu kama Serengeti Boys.

Mheshimiwa Nape alitangaza kamati hiyo itakayoongozwa na Mtangazaji mkongwe wa habari na Mpira wa miguu nchini, Charles Hilary mbele ya wanafamilia ya mpira wa miguu waliohudhuria kongamano ya kujadili juu ya ushiriki wa Tanzania katika michuano ya kimataifa.


Mada ilikuwa ni Tanzania kushiriki michuano ya Olimpiki Tanzania, lakini kwa kuwa kuna jambo la usoni la timu ya Serengeti Boys kucheza fainali za Kombe la Dunia huko Gabon kuanzia Mei 21, mwaka huu, Waziri Nape atakatangaza kamati ya kuhamamsisha ili Watanzania kwa pamoja waweze kuchangia.
Akitangaza kamati hiyo, Nape alisema kwamba Katibu wa Kamati hiyo atakuwa Mwesigwa Selestine ambaye ni Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wakati wajumbe ni Mtangazaji wa Radio ya EFM, Maulidi Kitenge; Mkurugenzi wa Mahusiano wa kampuni ya Airtel Tanzania, Beatrice Singano na Mrembo wa Tanzania wa mwaka 1999, Hoyce Temu.
Pia wamo Mkurugenzi wa Habari katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hassan Abbas; Mkurugenzi wa Global Publishers Limited, Eric Shigongo; bosi wa radio Clous, Ruge Mutahaba pamoja wa wasanii wa kizazi kipya Diamond Platnums na Ally ‘King’ Kiba.
Pamoja na hayo, katika kongamano hilo na wadau wa soka wadau ikiwamo Serikali iliridhia kuwa mshiriki wa karibu kwa kila hatua kuanzia Bodi ya Mfuko wa Maendeleo ya timu za taifa, Kamati ya Hamasa kwa lengo la kupanga pamoja na kushirikiana kwa pamoja.
Wameazimia kuwa na chanzo cha fedha cha kueleweka ili kufanikisha program mbalimbali za timu za taifa ikiwamo ya U23 ambayo inatakiwa kushiriki kwenye michuano ya Olimpiki. Serikali imepanga kuwa pamoja badala ya kile kinachoitwa kudandia matokeo mafanikio bila kushiriki maandalizi.
Kadhalika wameazimia mpira kuwa jambo la nchi ili hamasa inayotangazwa iguse wadau wote kwa maana ya Watanzania wote.
Pia chanzo cha kupata vipaji kiwe pia kutoka mashuleni (Umitashumta na Umiseta) ambako Mheshimiwa Waziri Nape mbali ya kuthibitisha kuwa mwaka huu itafanyika tofauti na mwaka jana, pia aliagiza kuwa isiwe kama matamasha.

No comments: