Tuesday, March 28, 2017

TANZANIA KWENYE HEADLINE ZA KIMATAIFA UVAMIZI WA CLOUDS MEDIA


Asasi za kiraia 33 barani Afrika zimelaani kitendo cha kuvamiwa kwa studio za televisheni ya Clouds na kulazimisha maudhui yasiyostahili yarushwe hewani.

Tamko la asasi hizo limetolewa ikiwa ni siku chache baada ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, (THBUB), Jukwaa la Wahariri (TEF) na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kulaani kitendo hicho kinachodaiwa kukandamiza uhuru wa vyombo vya habari.

Asasi hizo zinazohusika na utawala bora, demokrasia, haki za binadamu na uhuru wa habari zilikutana hivi karibuni mjini Kampala nchini Uganda katika mkutano uliokuwa ukizungumzia uhuru wa kujieleza na kupata habari.

Tanzania kwenye mkutano huo iliwakilishwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) , miongoni mwa mijadala iliyotawala ni kukemea vitisho na vitendo vya kunyanyasa waandishi.

Pia, wajumbe katika mkutano huo waligusia mabadiliko madogo ya baraza la mawaziri yaliyofanywa na Rais John Magufuli kwa kumtoa Nape Nnauye kwenye nafasi ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Asasi hizo zilimpongeza Nape ambaye kabla ya kuondolewa kwenye nafasi hiyo aliunda kamati iliyochunguza tukio la uvamizi wa studio za Clouds, wakisema uamuzi huo ulionyesha ujasiri wa kusimamia uhuru wa vyombo vya habari na uhuru wa kujieleza.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na asasi hizo, ilidai kwa siku za karibuni Tanzania imekuwa na matukio zaidi ya 40 yanayolenga kukandamiza uhuru wa vyombo vya habari.

“Waandishi wamekuwa wakizuiwa au wakati mwingine kubughudhiwa ili wasifanye kazi yao. Vitendo hivyo vimekuwa vikifanywa hasa na wakuu wa wilaya na polisi,” ilibainisha taarifa hiyo.

Wajumbe walikumbusha kifungu cha pili cha Azimio la kanuni za uhuru wa kujieleza Afrika la mwaka 2002, kinachoelekeza Serikali ihakikishe inachukua hatua stahiki kuzuia uvamizi kwenye vyombo vya habari.

Kifungu hicho kinaelezea endapo uvamizi huo utatokea, Serikali ina wajibu wa kuchunguza na kuwaadhibu wahusika kwa mujibu wa kosa lao.

No comments: