Tuesday, April 11, 2017

LHCR WAKOMALIA MCHAKATO WA KATIBA,HILI NI TAMKO LAO LEO


Kituo cha sheria na Haki za Binadamu kimeendelea kufuatilia kwa ukaribu masuala ya haki za binadamu hususani haki za kisiasa na kiraia ambazo ni miongoni mwa haki muhimu kwa binadamu. Katika kuifuatilia haki hii na kuitetea, Kituo kimeendelea kuona umuhimu wa kuwepo kwa Katiba ya wananchi, kwani masuala mengi ambayo yamelalamikiwa na wananchi na viongozi na hata juhudi za Rais John Pombe Magufuli za Kupambana na ufisadi kuirudisha heshima ya watendaji serikaliniyangeweza kupata suluhisho kwa kufufua mchakato wa Katiba Mpya ulioahirishwa bila tarehe maalum za kuurejesha .

Ikumbukwe kuwa toka mchakato wa kuandikwa  kwa Katiba Mpya ulipoanza mwaka 2011, ni zaidi ya shilingi Bilioni moja za Kitanzania zimekwisha kutumika. Matumizi haya makubwa ya kodi ya watanzania bila kupata matokeo ambayo ni kupatikana kwa Katiba Mpya ya wananchi ni sawa na ubadhirifu wa fedha hizo.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinasikitishwa sana na ukimya wa Serikali juu ya kuuendeleza mchakato huu. Awali, alipokuwa akisoma bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria aliyekuwa waziri wa Sheria na Katiba Mheshimiwa Harrison Mwakyembe alieleza nia ya Serikali kuukamilisha mchakato huu. Hata hivyo, tulishangazwa kutokujumuishwa kwa suala hili katika bajeti ya mwaka 2016/2017.Pia Mheshimiwa Rais alipokuwa akilihutubia Bunge kwa mara ya kwanza alieleza pia nia ya Serikali ya kurejea kwenye mchakato na kutanabaisha kwamba nafasi iko wazi kwa maoni yotote kuboresha Katiba Pendekezwa kabla haijapigiwa kura ya maoni.

Kutokana na hali hiyo Kituo kilihamasika kuufuatilia kwa ukaribu zaidi mchakato huu ili kuhakikisha upatikanaji wa katiba ambayo imehusisha asilimia kubwa ya maoni ya watanzania.

Kuwepo kwa kauli mbalimbali za viongozi ambazo zinakatisha tamaa, bado hakujarudisha nyuma jitihada za wananchi kudai mchakato huu kurejeshwa.

Kukosekana kwa taarifa rasmi kumeendelea kusababisha wananchi kukata tamaa ya kupata katiba mpya ambayo ingeweza kutatua changamoto zao kwa kiwango kikubwa. Kama serikali ilivyo na mipango mingi, ni muda muafaka serikali ikaleta mpango mkakati wa kumalizia mchakato wa katiba ili wanahabari wajiandae vema kushiriki kwenye hatua zitakazofuata wakiwa na taarifa za kutosha.

Pamoja na hatua iliyokwisha kufikiwa, Kituo kinaamini kwamba bado kuna fursa kubwa na wajibu mkubwa wa kufanikisha kufufua Muafaka wa Kitaifa juu ya Mchakato wa Katiba ambao ulitetereka katika ngazi ya Bunge Maalum la Katiba na hatimaye kuweka mazingira mabaya kwa umoja wa Taifa letu na kufifisha uhakika wa kukidhi lengo la awali la upatikanaji wa Katiba ya wananchi yenye misingi mizuri kwa Taifa la Tanzania.
Mapendekezo;
 Kituo cha Sheria na Haki za Binadmu kinapenda kuainisha mapendekezo yake kama ifuatavyo;
1.     Serikali iboreshe Sheria zinazoongoza Mchakato wa Katiba yaani Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Na. 83/2011 na Sheria ya Kura ya Maoni Na. 11/2013 ili ziruhusu mwelekeo mpya wa mchakato wa Katiba wenye tija na kujenga mazingira yenye kuzingatia muafaka wa Kitaifa katika upatikanaji wa Katiba Mpya. Maboresho haya ya Sheria ni vema yakazingatia kuondoa vifungu vibovu vya Sheria hizo ambavyo vimekua kivuli cha kuvurugika kwa muafaka katika hatua zilizopita za utungaji wa katiba mpya ikiwemo kupunguza uwezekano wa wanasiasa na vyama vya siasa kuuteka mchakato wa Katiba.
2.     Wananchi wote tudai kurudishwa mjadala wa kitaifa juu ya haja ya kufufua mchakato wa mabadiliko ya katiba, kwa mrengo wa maoni ya wananchi na usitishwaji wa hatua inayofuata ya Kura ya Maoni kwa mujibu wa Sheria ya Kura ya Maoni Na. 11/2013 ili kutoa fursa kwa wadau kujenga muafaka mpya wa kitaifa na kuamua namna bora ya kuelekeza Mchakato wa Mabadiliko ya Katiba.
3.     Serikali itenge bajeti kwa mwaka 2017/2018 kuwezesha mchakato huu wa Katiba Mpya kuendelea.
4.     Serikali itekeleze maagizo ya Hukumu inayohusiana na Kura ya Maoni iliyo tolewa tarehe 3 Februari 2017 Kuweza kuifanyia mabadiliko sheria ya Kura ya Maoni  No. 11 ya mwaka 2013 itakayo toa muongozo wa kuendelea na mchakato wa katiba.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu tunandelea kuwa sehemu ya uhamasishaji wa Katiba ya wananchi pasipo kukata tamaa kwa kuzingatia Mabadiliko yanayojitokeza na muelekeo wa taifa kwa ujumla.
Imetolewa na,
Dr. Helen Kijo-Bisimba
Mkurugenzi Mtendaji


No comments: