(Maelezo ya Kiongozi wa Chama katika kikao cha Kamati kuu ya Chama kilichoketi
Mjini Kahama wakati wa Miaka Mitatu ya Chama -
7/5/2017)
1.
Utangulizi
Juzi Mei 5, 2017 Chama chetu
cha ACT Wazalendo kilitimiza miaka 3 tangu kuzaliwa kwake mwaka 2014. Kwa umri
wa vyama vya siasa mbaimbali nchini, miaka mitatu unaweza usiwe umri wenye
maana yoyote, lakini kwa umri wa chama cha siasa cha Kijamaa na kinachopata
ufuasi na kupitia vikwazo vingi
kama chama chetu, basi miaka
mitatu ina maana kubwa sana. Ni miaka inayoonyesha safari ndefu ya mapambano ya
kurudisha misingi iliyoasisi Taifa, kusimika Demokrasia ya kweli na kuleta sera
mbadala za Kijamaa zinazosimamia masuala ya wanyonge wa Taifa hili na
Watanzania wote kwa ujumla.
Napenda kuwapongeza Viongozi
wote wa Kitaifa, pamoja na wale wa Mikoa na Wilaya mbalimbali nchini
walioshiriki kwa njia mbalimbali katika maazimisho ya miaka hii mitatu ya Chama
chetu. Ukiondoa chama tawala, CCM, sisi ndio chama pekee nchini ambcho kila
mwaka kinafanya maazimisho ya kuongezeka kwa umri na uhai wa chama, ndio maana
tuko hapa Kahama, kuazimisha miaka mitatu ya uhai wa chama chetu.
Lakini pia, Mei 5 hiyo hiyo,
ulitimia mwaka mmoja na nusu sasa tangu Rais wa Awamu ya Tano ale kiapo cha
kusimikwa kwa Serikali yake, Novemba 5, 2015. Hivyo basi, wakati chama chetu
kikitimiza miaka hii mitatu tangu kuzaliwa kwake, Serikali ya awamu ya tano
nayo imetimiza mwaka mmoja na nusu tangu
kusimikwa kwake. Nimeonelea basi, leo, katika kikao hiki cha Kamati Kuu, nitoe
waraka wangu huu wangu wa pili kwa Kamati Kuu ya chama chetu juu ya ‘Hali ya Kisiasa Nchini na Nafasi ya Chama
chetu cha ACT Wazalendo katika Siasa za Tanzania’, katika waraka huu
nitajikita katika kuangazia hali ya kisiasa ya nchini, nikizieleza changamoto
zetu, fursa zilizoko, hali ya kiuchumi ya nchi, changamoto za uongozi na
kushauri juu ya namna njema ya kuenenda ili kuondoa vikwazo vilivyoko na
kufaidika na fursa mbalimbali kuelekea 2020.
Na mwisho kabisa, nimefanya
tathmini ndogo, ili iwe mwongozo wa msingi wa maamuzi mbalimbali ya chama
wakati wa kutatua changamoto na kutumia fursa.
2.
MKONO
WA CHUMA: Hali ya Kisiasa Nchini na Changamoto Kuu ya Demokrasia Yetu
Waraka wangu wa kwanza kwa
Kamati kuu juu ya hali ya kisiasa ya nchi yetu na nafasi ya ACT Wazalendo
katika siasa za Tanzania nilioutoa Septemba 5, 2016 jijini Dar es salaam ulijikita katika kuelezea kwa upana juu ya
changamoto kadhaa ambazo zimezikumba siasa zetu tangu Utawala wa Serikali ya
awamu ya Tano uingie madarakani.
Nilieleza kuwa utawala huu
chini ya Rais Magufuli, kwa sehemu kubwa, umebadilisha utamaduni wa uendeshaji
wa siasa nchini na kuleta matokeo ya namna mbalimbali kwa vyama vya siasa
ikiwemo ACT Wazalendo. Niliieleza changamoto za kuzuiwa kwa shughuli za
kiuenezi za vyama vya siasa kama vile mikutano ya hadhara, maandamano, na hata
uhuru wa vyombo vya habari unavyobinywa nchini, sehemu kubwa ya changamoto
husika bado hazijaisha.
Rais Magufuli amejipambanua
kuwa Rais mwenye kupenda kutumia mkono wa chuma katika kutimiza adhma yake ya
kuhakikisha vyama vya upinzani na Asasi za Kiraia zinazoikosoa serikali
hazifurukuti. Mikutano ya hadhara imekwishapigwa marufuku na jeshi la polisi na
watendaji wa serikali wanaohaha kumridhisha Rais. Wanasiasa wanaoikosoa
serikali wametishwa na kusakwa na jeshi la polisi na baadhi yao kuwekwa
korokoroni ili kuwaziba midomo. Lengo la rais Magufuli na serikali yake ni
dhahiri: kutumia vitisho na vyombo vya dola ili kuvidhoofisha na ikiwezekana,
kuvifuta kabisa kwenye ramani vyama “vya kweli” vya upinzani nchini.
Mbali na wanasiasa, Serikali
ya Rais Magufuli imechukua pia hatua kadhaa kuviziba mdomo vyombo vya habari
vinavyoikosoa serikali. Wamiliki wa vyombo vya habari, Magazeti, vituo vya
Televisheni na Radio vinafungiwa, kuonywa na kutishiwa kwa kisingizio cha kutoa
habari za uchochezi, watu kadhaa wamefunguliwa mashtaka mahakamani kwa
kuonekana maoni yao ni kashfa kwa Rais huko kwenye mitandao ya Kijamii. Sheria
ya Mitandao inatumiwa sana kuwabana wakosoaji wa Serikali.
Kwa miezi hii 6 tangu nitoe
ule waraka wa kwanza hali husika haijabadilika kabisa, na kwa kiasi kikubwa
imezidi zaidi. Kasi ya kudogosha nguvu ya Bunge pamoja na taasisi nyengine za
uwajibikaji imekuwa kubwa zaidi, tishio kwa wamiliki wa vya vyombo vya habari,
wanahabari pamoja na vyombo vya habari vyenyewe nalo limekuwa wazi, wakati zuio
kwa siasa za vyama vya siasa (kwa maana ya Mikutano ya hadhara na Maandamano)
liko palepale. Hivyo niseme hali imekuwa mbaya zaidi.
2.1.
Matokeo
Yake Kwa Vyama Vya Upinzani Nchini
Tangu kuhuishwa kwa mfumo wa
vyama vingi nchini kwenye miaka ya tisini, vyama vya upinzani vimejikita kwenye
njia za jadi za uenezi, ambazo ni mikutano ya hadhara, maandamano na
makongamano. Hivyo basi, kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara kumeathiri sana uwezo
wa vyama vya siasa kunadi sera na kuvuna wanachama.
Wakati haya yakivikumba vyama
vya upinzani, Chama tawala kinaendelea kuwatumia viongozi na watendaji wa serikali (Rais, mawaziri, wakuu wa wilaya,
wabunge, madiwani na wakurugenzi, nk) kukitangaza chama hicho katika inayoitwa
“Mikutano ya kuhimiza maendeleo”. Fursa hiyo kwa vyama vya upinzani inapatikana
katika maeneo tu ambayo vyama hivyo vina wabunge na madiwani, au halmashauri
ambazo wanaziongoza.
2.2.
Athari
Na Faida Kwa ACT Wazalendo
Jambo hili kwa kiasi kikubwa
limekiathiri chama chetu pia, muundo wa chama chetu nao ulijiegemeza katika
njia za asili za uenezaji chama (mikutano ya hadhara, maandamano nk), hata
ziara ya kutambulisha chama ya mwaka 2015, ambayo ndiyo ziara kubwa zaidi tuliyowahi
kufanya, nayo ilikuwa katika muundo wa mikutano mikubwa ya hadhara. Hivyo kwa
kuzuiwa mikutano ya hadhara (nje ya jimbo moja tunaliliongoza, na Kata kadhaa
nchini), kumekuwa na athari kubwa kwa chama chetu.
Lakini ni ukweli pia kuwa
uwezo wetu wa kiuchumi umeshuka mno mara baada ya uchaguzi mkuu, msingi wa
chama chetu katika kuwa na vyanzo vya kiuchumi haukuwa mzuri, tangu awali
hatukujenga utamaduni wa kuhamasisha wanachama na wafuasi wetu wakichangie
chama kama chanzo kikuu cha mapato ya chama, tulijikita katika kutegemea
michango mikubwa ya viongozi wa kuu wa chama, ambao mara baada ya uchaguzi nao
waliathirika kwa kuwa na madeni makubwa ambayo yamepunguza uwezo wao wa
kukichangia chama. Jambo hilo limepunguza kwa kiasi flani hata uwezo wetu wa kuzunguka
mikoa mbalimbali nchi nzima kufanya mikutano ya hadhara, hivyo zuio hili kwa
kiasi kikubwa limesaidia kutupa sababu dhidi ya ukata wetu.
Lakini hiyo haipaswi kuwa
sababu ya kuacha haki hii ya vyama vya siasa kuzuiwa, maana ni kinyume na
Katiba na inaviza ukuaji wa Demokrasia yetu pamoja na uenezaji wa Sera za chama
chetu katika mikoa na wilaya mbalimbali nchini.
3.
Hali
Ya Uchumi: Wananchi Wana Hali Ngumu Sana
Eneo jengine muhimu la waraka
huu ni juu ya hali ya uchumi ya nchi, eneo hili serikali ya awamu ya tano
imefanya vibaya sana. Kiashiria kikuu ni utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2016/17
ambao mpaka mwezi machi mwishoni bajeti katika wizara nyingi utekelezaji wake
haukuzidi hata 50%. Hata Bajeti ya mwaka huu wa fedha uwasilishwaji wake
umeonyesha kuwa matumaini ya uchumi kuwa mzuri hayapo tena, kuna hali kubwa ya
kukata tamaa miongoni mwa wananchi.
Maeneo mengi ya nchi kuna
uhaba mkubwa wa chakula na badala ya Serikali na hasa Rais kuwa matumaini Kwa
wananchi akiwa Comforter In Chief, kumekuwa na maneno makali ya kuwakatisha
tamaa wananchi. Bei za vyakula nchini zimepanda mno kiasi cha wananchi
kushindwa kumudu chakula ili waweze kufanya kazi na kukuza Uchumi. Vyakula
vikuu kama mahindi, sukari, mafuta ya kupikia, ngano nk bei imekuwa juu mno.
Taarifa za Serikali kupitia
ripoti za Benki Kuu zilizopo kwenye tovuti yake juu ya hali ya Uchumi ya nchi
yetu (Quartely Economic Review na Monthly Economic Review) kwa mwezi wa Disemba
2016 zinaonesha kuwa kuna mfumuko mkubwa mno wa bei za Vyakula, hasa Chakula Kikuu
kwa Watanzania - Mahindi, ambapo bei ya chakula hicho kikuu nchini imepanda kwa
zaidi ya 30% na kupandisha mno gharama za maisha za wananchi wote nchi nzima.
Leo bei ya kilo moja ya
mahindi nchini iko sawa au ni zaidi ya bei ya kilo moja ya mchele kwenye miji
mbalimbali nchini, sukari bei juu, mafuta ya kula bei juu nk. Kwa wakati wa
mjini hata bei ya gesi kwaajili ya kupikia majumbani imepanda, wananchi
wamerudia matumizi ya mkaa, tujiandae na uharibifu wa misitu nchini. Ofisi ya
takwimu ya Taifa imetoa Taarifa ya kuonyesha kuwa Mfumuko wa Bei umepanda kwa
kasi na sasa umefika asilimia 6.4 Kwa mwaka unaoishia Machi, 2017.
Ukuaji wa sekta binafsi
umedorora na kushuhudia biashara maelfu kwa maelfu zikifungwa na kusababisha
ajira nyingi kupotea na ajira chache kutengenezwa. Manispaa ya Ilala peke yake
imefunga biashara 2900 na hivyo kupoteza chanzo cha mapato ya Manispaa. Lakini
hata mikopo ya Kibenki kwa sekta binafsi imepungua mno, ikiwa ni kiashiria cha
mdororo wa sekta binafsi. Jana kulikuwa na mkutano wa baraza la biashara la
Taifa, uliofanyika ikulu jijini Dar es salaam, wawakilishi wa wafanyabiashara
na wale wa sekta binafsi walilieleza hili kwa upana.
Kwenye uwekezaji nako hali si
nzuri, uwekezaji wa mitaji kutoka nje ya nchi umepungua sana. Matamko ya
viongozi wakuu wa Serikali kuhusu mwelekeo wa Uchumi yanatuma ujumbe hasi
kuhusu uwekezaji wa mitaji nchini, na hivi sasa kila mwekezaji kwenye macho ya
Serikali anaonekana mpiga dili (katika mkutano wa jana Ikulu, ndugu Mengi – kwa
niaba ya sekta binafsi, alilieleza hili). Juhudi zote za kuhamasisha uwekaji wa
mitaji nchini zilizofanywa tangu Serikali ya awamu ya tatu, zimefutwa katika
mwaka Mmoja na nusu tu wa Serikali ya awamu ya tano. Hali ni ya kusikitisha
sana.
Tatizo jengine kubwa ni suala
la ajira, ukiondoa ajira zilizopotea kwa mdororo wa sekta binafsi, lakini pia
hakuna ajira mpya serikalini tangu awamu ya tano iingie madarakani. Vijana
mbalimbali waliomaliza masomo yao ya Ualimu, Utabibu, Maafisa Kilimo, Mifugo na
Uvivu bado wako mtaani bila ajira kwa mwaka sasa. Hata walioajiriwa mwanzoni
ajira zilisitishwa kwa kisingizio cha uhakiki wa watumishi wa Umma. Kukoleza
maumivu kwenye kidonda ni hatua ya kufukuza wafanyakazi 10,000 waliodaiwa
kughusi vyeti.
Serikali imeajiri walimu 3000
tu wa ualimu wa masomo ya sayansi na madaktari wasiozidi 300, japo kwenye mei
mosi imejitapa kuwa itaajiri watumishi 52,000 mwaka huu (jambo ambalo
haitafanya), kuongeza mishahara na kupandisha watumishi vyeo. Hatua zote hizo
hazitoshi katika kupunguza tatizo la ajira nchini.
Kwenye Kilimo (ambayo ndiyo
sekta inayohusisha wananchi wengi zaidi nchini) hali ni mbaya zaidi. Taarifa ya
ya robo mwaka ya Benki Kuu nchini, BOT quarterly economic bulletin ya Disemba
2016 inaonyesha kuwa sekta ya Kilimo ilikua kwa kasi ya 0.6% tu kutoka ukuaji
wa 2.5%. Asilimia 75 ya Watanzania wote wamejiajiri katika sekta ya Kilimo,
hivyo mdororo huu ya sekta ya Kilimo kutoka ukuaji wa 2.5% mpaka ukuaji wa 0.6%
ni ishara mbaya mno kwa ustawi wa zaidi ya robo tatu ya Watanzania.
Kwa Vijijini 78% ya Watanzania
wanajihusisha na Kilimo. Hii maana yake ni kwamba wananchi wengi vijijini
hawafanyi uzalishaji, jambo hili ni hatari sana, ni dalili kuwa ufukara wa watu
wetu unazidi. Ni kwa sababu hii, pamoja na uchumi wetu kukua kitakwimu, 7% kwa
mwaka, lakini bado wananchi wetu walio wengi wanaishi kwenye dimbwi la ufukara.
Maana ukuaji huo wa Uchumi hauhusishi kilimo, hauhusishi zaidi ya robo 3 ya
Watanzania.
Ukuaji huu mdogo wa Kilimo
unapaswa kutushtua, kwani ni hatari sana, ni hatari mno. Maana unajenga uchumi
unaowaacha karibu zaidi ya robo 3 ya Watanzania kwenye ufukara, ni uchumi
unaopanua matabaka ya mafukara na matajiri.Ukuzaji wa viwanda, ambayo ndiyo
sera kuu ya msingi ya Serikali ya awamu ya tano nao umeshuka mno, taarifa za
serikali zinaonyesha juu ya kushuka kwa uzalishaji wa bidhaa za viwandani,
ikiwa ni athari pia ya kushuka kwa uwezo wa manunuzi wa watanzania (purchasing
power). Jambo hilo limefifisha matumaini ya Tanzania ya wiwanda.
Athari kubwa zaidi iko kwa
wakulima, maana ndoto yao ya kuongeza thamani ya mazao yao ya kilimo kupitia
viwanda vidogo vya usindikaji na uzalishaji bidhaa haionekani kutimia, hata
korosho ambalo ndio zao lililotuingizia fedha za kigeni zaidi tumeziuza zikiwa
hafi, hatukufanya ubanguaji nchini na hivyo kuongeza thamani. Hali iko hivyo
pia kwenye pamba yetu na mazao mengine ya kibiashara kama Karafuu na mkonge.
Mazao hayo, kungekuwa na sera nzuri yangewezesha mamilioni ya ajira nchini
kwenye sekta ya nguo, ubanguaji korosho na uzalishaji wa bidhaa zitokanazo na
mkonge. Si huko tu, uvunaji nao wa samaki katika bahari na maziwa yetu
haujaonekana kuzalisha ajira za kutosha zenye tija.
Sekta za huduma nazo
hazikufanya vizuri, bado kuna changamoto kubwa sana kwenye sekta ya elimu
pamoja na juhudi kiasi za serikali,changamoto ambazo zinazorotesha ndoto ya
ubora wa elimu inayotolewa. Kwenye elimu ya juu hali ndio ni mbaya zaidi,
vijana wengi wa kitanzania wamekosa fursa na haki yao ya elimu kwa kukosa
mikopo.Sekta ya afya nayo halikadhalika, bajeti ya dawa kwa mwaka 2016/17
iliyopangwa haikufikiwa hata nusu, hivyo kuchangia hali ya ukosefu wa Dawa
katika vituo vya afya mbalimbali nchini, urari wa madaktari wanaohudumia
wagonjwa bado umebaki vile vile kuwa ni mara mbili ya Kiwango kinachotakikana
duniani, hata Bajeti ya mwaka huu ya Wizara ya afya haionekani kutatua
changamoto hizi.
Yote hayo yana athari kwenye
uchumi wa nchi, yamepunguza kipato cha wananchi, yamechangia ugumu wa maisha.
Yamefuta matumaini waliyokuwa nayo watanzania na yamewakatisha tamaa.
Chama chetu kikikazania
kuyasemea masuala haya (ambayo ni masuala ya wananchi) kitajipambanua kwa
upekee. Kwenye Mpango Mkakati wa miaka 5 wa Chama chetu tumesema dhahiri kuwa
tunataka Siasa za Maendeleo. Hivyo kibwagizo cha Demokrasia Ni Maendeleo au
Demokrasia na Maendeleo Ni muhimu sana katika Siasa za Zama hizi za sasa.
4.
Kigoma
Ujiji: Nafasi Ya ACT Wazalendo Kuonyesha Utofauti Wa Kiuongozi
Hali hiyo ya kiujumla ya
uchumi wa Taifa inatupa nafasi kubwa sana ya kuonyesha mapungufu ya Serikali
hii ya sasa ya CCM, inatupa nafasi nzuri ya kuonyesha ubaya wa sera zao na
ubaya wa usimamizi wao wa sera husika, ni jambo linatupa fursa ya kujinadi kwa
kuonyesha mapungufu ya Serikalia pamoja na kuainisha njia mbadala za utatuzi wa
hali hiyo kwa Watanzania.
Lakini kufanya hayo tu hakutuhakikishii
ushindi kwenye Uchaguzi 2020 (ushahidi tuliuona kwenye chaguzi ndogo mbalimbali
za udiwani nchini), suala la kuchaguliwa halina mahusiano sana na uzuri wa
kukosoa tu na kutoa njia mbadala, ni muhimu sana nasi tuonyeshe mfano kwa
kuongoza vizuri katika maeneo ambayo tumepewa dhamana ya uongozi. Pamoja na
kuisimamia Serikali kwenye uendeshaji wa nchi kiujumla, Chama chetu kina ridhaa
ya kuendesha Halmashauri ya Kigoma Ujiji. Kwa kiasi flani kipimo tunachokitumia
kupima Serikali kuu ya masuala mbalimbali ya uongozi ndicho hicho kitatumika
kutupima nasi katika uendeshaji wetu wa mambo ya kiuongozi kwenye maeneo
mbalimbali ya nchi ambayo sisi tumepewa dhamana ya kuyaongoza – hasa hasa
Halmashauri ya Kigoma Ujiji.
Kwa kiasi kikubwa tumefanikiwa
sana katika kuendesha Serikali kwa uwazi, utaratibu wetu wa kuainisha mapato
yote ya halmashauri kwa kila mwezi ni hatua njema sana ya kuanzia. Hati chafu
ya Halmashauri ya Kigoma Ujiji, kwa mwaka wa fedha wa 2015/16 ni jambo
linalotutia doa (hasa kwa kuwa pia katika kipindi hiko chama pia kimepata hati
chafu), ni jambo ambalo linatuondolea uhalali kama chama wa kuionyoshea kidole
serikali kuu ya matumizi mbalimbali mabaya ya fedha za umma.
Ni muhimu chama chetu
kihakikishe kuwa jambo hilo la hati chafu halijirudii ndani ya chama na kwenye
Halmashauri katika mwaka wa fedha wa 2016/17 na kuendelea. Ni muhimu tuonyeshe
mfano kwa kuongoza kwa ufanisi, uwazi na uadilifu (kwa kuhakikisha Sera zetu za
Kijamaa zinaleta Uchumi Shirikishi unaongeza Ajira, kunakuwa na huduma bora za
kijamii za maji, afya na elimu, na kuwa watu wetu wanakuwa na akiba kwa
kuwaingiza kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii na hivyo kuboresha uwezo wa o wa
kiuchumi).
Uongozi wetu mzuri katika eneo
dogo tulilopewa dhamana sasa inapaswa kuwa ndio shabaha ili iutupe uhalali wa
kuomba ridhaa ya kuongoza eneo kubwa zaidi mwaka 2020.
5.
Athari
za Yote Haya Kisiasa: Umaarufu wa Serikali Dhidi ya Ukuaji wa Chama
Kuna mabadiliko kiasi kwenye
hili tangu miezi 6 iliyopita (Kamati Kuu ya Septemba 5, 2016) nilipowasilisha
waraka juu ya hali ya kisiasa nchini. Nilieleza kuwa juu ya matendo yote kidikteta
ya serikali ya awamu ya tano, bado imani ya wananchi kwa serikali na kwa rais
Magufuli ilikuwa kubwa mno (ukubalikaji wa Rais Magufuli ulikuwa ni kwa 94% ya
Wananchi wote waliohojiwa). Propaganda ya Serikali juu ya maendeleo (pamoja na
husda iliyozalishwa kutokana na utumbuaji majipu) iliwaingia sana wananchi na
kuamsha matumaini yao.
Hali hiyo ilikuwa kikwazo mno
kwetu kuikosoa Serikali, ilifanya kazi yetu ya kutoa sera mbadala iwe ngumu mno
kueleweka kwa wananchi kwa kuwa matumaini yao kwa serikali yalikuwa makubwa
mno. Fursa iliyoko kwetu ni kuwa hali hiyo haipo sasa, utafiti wa mwisho
(uliofanyika disemba 2016 – Januari 2017) wa taasisi hiyo hiyo iliyoonyesha Rais
Magufuli anakubalika kwa 96% (Juni 2016) uilonyesha kuwa umaarufu wake umeshuka
kwa zaidi ya 18% - mpaka 76% (Januari 2017).
Lakini ushukaji wake huo
haukuvisaidia vyama vya upinzani pia, mfano Chadema umaarufu wao ulishuka pia
kwa zaidi ya nusu, kutoka 32% (Juni 2016) mpaka 16% (Januri 2017),
halikadhalika CUF na UKAWA kwa ujumla. Jambo hilo linaonyesha kuwa wananchi
pamoja na kuanza kuichukia serikali lakini pia wamepoteza matumaini na siasa,
maana umaarufu wa vyama vyote vikuu vya siasa nchini unashuka.
Sisi ACT tumepata faida ndogo,
ukuaji wa ufuasi wetu ulipanda kwa asilimia 1, kutoka 1% (Juni 2016) mpaka 2%
(Januari 2017), upandaji huo wa ufuasi na kupendwa si mkubwa, lakini ni jambo
la kujipongeza sana. Wakati wa tathmini na utengenezaji wa mpango mkakati wa
chama (Januari 2016) changamoto kubwa ambayo tuliazimia kuikabili ilikuwa ni
‘Uwepo’ (Visibility) zaidi kabla ya Ufuasi, kwenye hili la ‘Visbility’
mafanikio yetu si mabaya, changamoto yetu ni kuongeza Ufuasi.
Chaguzi ndogo mbalimbali za
Serikali za Mitaa zinaonyesha bado lipo tatizo la uwepo wetu, maana
hatukushiriki kabisa kwenye chaguzi ndogo za Serikali za Mitaa za Lindi Mjini,
Uyui mkoani Tabora na hata Kawe jijini Dar es salaam. Tuna wajibu wa
kuhakikisha tunatatua hiyo changamoto ya uwepo wetu. Kushiriki chaguzi hizi ni
kuonyesha uwepo wetu. Imani yangu ni kuwa tunayo fursa ya kufanya vizuri zaidi
katika kuwafikia watanzania wengi zaidi ili kupanua wigo wa wafuasi, kuongeza
uwepo (visibility) yetu na kupanua nafasi yetu katika ushiriki wa siasa nchini.
6.
Mitandao
ya Kijamii: Njia Mbadala ya Uenezi wa Chama
Kamati ya Itikadi, Uenezi na
Mawasiliano ya Umma imefanya kazi nzuri sana katika miezi hii 6 tangu Kikao cha
Kamati Kuu cha Septemba 5, 2016. Kwa kiasi kikubwa vyombo vya habari (Magazeti
na Televisheni) vya nchi yetu vimehodhiwa na vyama vikuu nchini (hasa CCM na
Chadema), hivyo kuifanya kazi ya kutangaza uwepo wetu kuwa ngumu mno.
Hivyo kamati ilijitahidi
kujikita katika usambazaji wa kazi na taarifa za chama kupitia mitandao ya
Kijamii, zaidi Facebook (ambapo makadirio ni uwepo wa Watanzania zaidi ya
milioni 4 kwenye mtandao huu wa Kijamii – Ikikadiriwa watafikia milioni 7 - 8
mwaka 2020), naweza kusema kwa dhahiri kuwa ACT Wazalendo ndio chama
kinachofanya uenezi zaidi kuliko vyama vyote kwenye Mitandao ya Kijamii, hili
ni jambo zuri sana, linapaswa kuendelezwa maana imeongeza mno Visibility ya
chama.
Pamoja na mafanikio hayo, zipo
changamoto kwenye njia hii ya uenezi wa chama. Kwanza wananchi wengi wa
vijijini hawapo huku, pili mafukara na masikini wengi hawapo huku. Hivyo ni
muhimu kujua kuwa huku kwenye mitandao ya kijamii sehemu kubwa ya wananchi
tunaowafikia ni tabaka la kati na wananchi wa mjini ambao ni theluthi moja tu
ya wapigakura wote nchini.
Changamoto nyengine kuu ni
kuwa Viongozi wetu wengi wa chama hawajajikita kwenye njia hii ya uenezi wa
chama, wao wanaamini zaidi kwenye njia za asili za uenezi (Mikutano ya hadhara)
ambazo zimezuiwa na serikali. Changamoto ya mwisho ni kuwa njia hii ya mitandao
ya Kijamii ina gharama kiasi, hasa kifedha, ili kufikia watu wengi zaidi njia
hii inahitaji udhamini wa matangazo (sponsorship) ambao kwa mwezi si chini ya
dola 200 (wastani wa shilingi laki 5).
Pamoja na njia hiyo, Utafiti
unaonyesha njia kuu ya kuwafikia watanzania wengi zaidi (hasa mafukara,
masikini na waishio vijijini) ni kupitia redio, mitandao ya Kijamii ni njia ya
pili ya kuwafikia watanzania wengi zaidi na si njia kuu. Njia kuu ni redio
(hasa redio za Kijamii zilizoko katika mikoa na wilaya mbalimbali nchini).
Hivyo basi, ni muhimu Kamati
yetu ya Uenezi kulitazama hili kwa undani, na kujitahidi kuja na mpango mkakati
mzuri zaidi kuhakikisha tunazitumia zaidi redio nchini katika uenezi wa chama
ili kuhakikisha tunalifikia kila kundi la Watanzania. Pamoja na hatua zote
hizo, ni muhimu sana kupanua nguvu yetu katika Magazeti na televisheni
mbalimbali nchini..
7.
Tathmini
Juu ya Mwongozo wa Msingi wa Maamuzi Mbalimbali ya Chama
Tunapaswa kujitathmini upya
kwa lengo la kuwa na njia nzuri ya kufanya maamuzi kwenye utendaji wa chama,
tathmini husika itasaidia kutoa muongozo wa namna ya kuenenda katika kufikia
maamuzi mbalimbali ya chama katika ngazi zote za uongozi wa Chama. Tathmini hii
itatusaidi kuweka msingi na kuepusha sintofahamu katika masuala yote
yatakayohitaji muongozo wa chama katika ufikiaji wa maamuzi yake. Napendekeza
tathmini husika ijikite kwenye makundi matatu yafuatayo:
Ni
masuala gani tunayasimamia bila soni kwa maslahi ya umma hata kama ni ya
Serikali?
Masuala yote ambayo yana faida
kwa jamii ambayo yanafanywa na Serikali basi tutakuwa nayo pamoja. Kwa mfano
yafuatayo:
I.
Masuala
yote yanayohusu kusimamia Uwajibikaji wa Viongozi na kupinga Rushwa na Ufisadi:
Jambo hili tunapaswa kuwa pamoja na Serikali, japo ni muhimu kuhakikisha Uimara
wa Taasisi za Kidemokrasia na kiuwajibikaji Kama Bunge, Vyama vya Siasa, Ofisi
ya Ukaguzi ya Taifa (NAOT), TAKUKURU, Sekretariat ya Maadili ya Viongozi nk
LAZIMA viwe Ni ajenda zetu za kudumu hata kama Serikali nayo itasimamia mambo
hayo.
II.
Miradi
mikubwa ya Maendeleo ya Nchi na Wananchi: Ni Masuala ambayo hatupaswi
kuona soni kuyasimamia hata kama watawala wanayasemea pia. Wajibu wetu Kama
chama cha upinzani utakuwa ni kuhakikisha mambo hayo yanafanyika bila chembe ya
Ufisadi hata kama ni Ufisadi unaofanywa na Ikulu au walio Karibu na Ikulu.
Mathalani - Serikali imenunua Ndege mpya za ATCL, nii jambo la kupongezwa.
Lakini ndege hizi zimelipiwa bei ya ndege mpya wakati inasemekana ni ndege
zenye tatizo na wenzetu waliuziwa kwa bei ya chini zaidi. Hili lazima tuhoji na
kupata majibu ya Serikali. Miradi mikubwa kama ya SGR, ni muhimu tuhakikishe inafanyika
kwa ufanisi na bila ufisadi, kwa kusaidia hata ushauri wa njia mbadala za
kupata fedha za utekelezaji wake, kushauri njia bora za utekelezwaji wake ili
mradi husika uzalishe faida kwa haraka nk.
III.
Utu na
Udugu wa Kitanzania: Imani yetu ni kuwa Watanzania wote ni wamoja,
vyama vya siasa ni njia tu za kuifikia Tanzanianjema zaidi.
Masuala
gani tunaungana mkono na Wapinzani wenzetu kwa ajili ya kuimarisha taswira yetu
kama Upinzani?
Masuala yote ambayo yana faida
kwa jamii ambayo yanaminywa na Serikali basi tutakuwa pamoja na wenzetu wa
Upinzani kuyapigania. Kwa mfano masuala yafuatayo:
I.
Uhuru
wa Bunge: kuendesha mambo yake bila kuingiliwa lazima iwe Wajibu
wetu MKUBWA.
II.
Uhuru
wa Mahakama: kuendesha mambo yake bila kuingiliwa lazima
iwe Wajibu wetu MKUBWA.
III.
Utawala
wa Sheria na Katiba: Ni dhahiri ni lazima kuungana na vyama
vingine vya Upinzani kuhakikisha tunalinda Uhuru wa kufanya siasa, habari na
mikusanyiko kama maandamano. Hizi ni Haki za Kikatiba na Kisheria. Chama hakiwezi kukaa pembeni na
kuacha wenzetu wakipigania haki hizi peke yao na kusubiri matokeo. Hatuwezi
kuwa ‘Free Riders!’ (kuwepo wakati wa mafanikio tu wakati hatutaki kupambana
kuondoa vikwazo vya kidemokrasia). Hata hivyo Ni muhimu sana kutumia njia za
kikatiba na kisheria kudai haki hizi huku tukihakikisha Amani na utulivu wa
Nchi unatamalaki.
IV.
Kupigania
Uimara wa taasisi za Uwajibikaji na za Kidemokrasia: kama
Bunge, Vyama vya Siasa, Ofisi ya Ukaguzi ya Taifa (NAOT), TAKUKURU, Sekretariat
ya Maadili ya Viongozi nk. Hili LAZIMA liwe Ni ajenda yetu za kudumu kwa
kuhakikisha tunashirikiana na wapinzani wenzetu kuibana serikali.
V.
Uhuru
wa kujiendesha wa Serikali za Mitaa na Halmashauri:
Dhidi ya matishio yoyote ya kiuchumi, kisheria na kidemokrasia kutoka serikali
kuu.
VI.
Uhuru
wa Vyama vya Siasa: Mfano Katazo dhidi ya Mikutano ya hadhara,
maandamano nk.
VII.
Uhuru
wa Habari: Kwa mfano vitisho dhidi ya wanahabari, wamiliki wa vyombo
vya habari na ufunguajia wa vyombo vya habari.
VIII.
Uhuru
wa Kujieleza: Tishio dhidi ya Uhuru wa kujieleza nchini
liko dhahiri kabisa, kwenye suala hili tutasimama na wenzetu wote wa upinzani
katika kuhakikisha tunapigania haki ya watanzania kujieleza kwa uhuru bila
vitisho kwa kupiganiwa kufutwa kwa sheria mbalimbali mbaya ambazo ni kikwazo
dhidi ya uhuru huo.
IX.
Ushirikiano
katika chaguzi mbalimbali kwa kadiri haja itakavyojitokeza.
Ni
masuala gani hatusimami na mtu kwa sababu ya kusimamia misingi ya chama chetu?
Masuala yote ya Kisera na
Kiitikadi ya chama tutapaswa kuyasimamia hata kama tutabaki peke yetu kwenye
kuyasimami. Kwa mfano masuala yafuatayo:
I.
Muungano
na Umajumui wa Afrika: Hususan Utangamano wa Afrika Mashariki ni
moja ya Msingi wa Chama chetu. Uimara wa Muungano wetu wa Tanzania na umuhimu
wa Afrika kuwa moja, ni mambo ambayo hata tukibaki peke yetu lazima tuendelee
kuyasemea.
II.
Uzalendo
na Nafasi ya Nchi yetu Kimataifa: Kanuni kuu ya Kizalendo ni
‘wrong or right, my country first’. Tukishindwa kusimamia hili basi tunapaswa
kukaa kimya tu kwenye jambo husika bila kutoa kauli ambayo itaathiri Taifa.
III.
Sera
za Kijamaa katika masuala ya Kimataifa ya Kiuchumi na Kikodi: kama
vile kubana mianya ya kikodi kwa makampuni makubwa ya Kimataifa, kuwa mstari wa
mbele katika kampeni ya kupambana na uhamishaji wa mitaji kutoka nchi masikini.
IV.
Hifadhi
ya Jamii ili kuongeza uwezo wa kuweka akiba na kuongeza mtaji wa
ndani katika uwekezaji nchini.
V.
Sera
za Kijamaa juu ya Masuala ya Kilimo: Kusimamia Fao la Bei, huduma
za Hifadhi ya Jamii kwa Wakulima, Uhakika wa Ruzuku ya Mbolea, Viwanda vya
Kuongeza thamani ya Mazao ya Kilimo (Agro-processing Industires), na masuala ya
masoko ili kuinua kipato cha wakulima.
VI.
Ushirikishwaji
wa wananchi wenyewe katika Uvunwaji wa rasilimali za nchi
(hasa madini, mafuta na gesi asilia) na pia Matumizi ya mapato yatokanayo na
Uvunwaji husika.
VII.
Kupigania
Uchumi – Shirikishi na wa Kijamaa unaozalisha ajira kama
ilivyoainishwa kwenye azimio la Tabora linalohuisha Azimio la Arusha.
VIII.
Azimio
la Tabora: Hili ni tamko la Kisera na Kiitikadi la Chama, jambo
lolote la kisera na kiitikadi lililoainishwa kwenye Azimio la Tabora tutapaswa
kulisimamia.
8.
Hitimisho
Naomba Kamati Kuu ya Chama
inayokutana leo hii hapa mjini Kahama katika maazimisho haya ya miaka mitatu ya
chama chetu itafakari kwa kina juu ya Hali ya Siasa nchini na kutoa maelekezo ya
hatua za kuchukuliwa na Chama.
Asanteni sana kwa kunisikiliza.
Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto (Mbunge)
Kiongozi wa Chama – ACT Wazalendo
Kahama – Shinyanga
Mei 7, 2017
No comments:
Post a Comment