Wednesday, May 31, 2017

STARS KUANZA KUFANYA MAZOEZI USIKU



Timu ya mpira wa miguu ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inayodhaminiwa na Bia ya Serengeti kutoka Kampuni ya Bia ya SBL, imesafiri salama kutoka Dar es Salaam, Tanzania hadi hapa Alexandria, Misri.

Timu iliyotumia Ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia, ilipaa kutoka Dar es Salaam, saa 10.45 jioni ambako ilipitia Addis Ababa kuunganisha ndege ya kufika Misri.

Stars iliyokuwa na jumla ya watu 30 wakiwamo viongozi, benchi la ufundi na wachezaji kwa ujumla, ilitua Uwanja wa Ndege ya Cairo, Misri majira ya saa 7.45 usiku ambako mbali ya wenyeji Tolip Sports City, pia ilipokelewa na maofisa wa ubalozi wa Tanzania walioko hapa Misri.

Baada ya kupokelewa, timu hiyo ilisafiri kwa gari maalumu kutoka Cairo, Misri hadi Alexandria umbali wa zaidi ya kilomita 180 na kufika alfajiri baada ya mwendo wa takribani saa mbili. Saa za Misri na Tanzania zina tofauti ya dakika 60. Misri wako nyuma kwa saa hiyo moja.

Kwa niaba ya timu nzima, Kocha Mkuu, Salum Shabani Mayanga pamoja na viongozi wengine akiwamo Mkuu wa Msafara, Wilfred Kidao walishukuru Mungu kwa kusafiri salama hadi kufika hapa Alexandria kwa ajili ya kambi ya wiki moja kujindaa kucheza na Lesotho. Pia walishukuru Watanzania wote kwa dua zao kwa kusafiri salama.

Akizungumza mara baada ya kukagua viwanja vya mazoezi leo asubuhi, Kocha Mayanga ambaye alipewa majukumu ya kuifundisha timu hiyo mapema - Januari, mwaka huu, amesema: “Programu ya mazoezi kwa timu hii itaanza leo saa 2.00 usiku. Ingawa siku nyingine nitafanya asubuhi na jioni.”

Kwa msingi huo, alisema kesho Alhamisi Juni mosi, atakuwa na mazoezi kwa vipindi vyote viwili uwanjani - asubuhi na usiku kabla ya kutoa maelekezo darasani kwa siku ya Ijumaa na baadaye mazoezi ya uwanjani tena.

Taifa Stars inayopiga kambi hapa Misri, inajiandaa na mchezo dhidi ya Lesotho utakaofanyika Juni 10, 2017 kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi nje kidogo ya jiji la  Dar es Salaam. Mchezo huo umepangwa kuanza saa 2.00 usiku.

Mchezo dhidi ya Lesotho ni muhimu kwa Tanzania ikiwa ni mechi ya kwanza kwa Taifa Stars katika Kundi ‘L’ kuwania nafasi muhimu ya kucheza fainali za Kombe la Mataiafa ya Afrika (AFCON) za mwaka 2019 zitakazofanyika NCHINI Cameroon.

Mbali ya Lesotho na Tanzania, mataifa mengine katika Kundi ‘L’ ni Uganda na Cape Verde ambao pia wikiendi ya Juni 9, 10 na 11, mwaka huu watakuwa katika mchezo wa kwanza pia kuwania nafasi hiyo.

Wachezaji wanaounda kikosi hicho cha Kocha Salum Mayanga ni makipa Aishi Manula  (Azam FC), Benno Kakolanya  (Yanga SC) na Said Mohammed (Mtibwa Sugar).

Walinzi wa pembeni wako Shomari Kapombe    (Azam FC), Hassan Kessy (Yanga SC), Mohammed Hussein (Simba) na Gadiel Michael.

Walinzi wa kati ni Erasto Nyoni  (Azam FC), Salim Mbonde (Mtibwa Sugar), Abdi Banda (Simba SC) na Nurdin Chona (Tanzania Prisons) ilihali viungo wa kuzuia ni Himid Mao (Azam FC) na Jonas Mkude kutoka Simba SC ambaye kwa sasa anapatiwa matibabu baada ya kupata ajali.

Viungo wa kushambulia Salum Abubakar (Azam FC), Said Ndemla  (Simba SC) na Mzamiru Yassin (Simba) wakati viungo wa pembeni ni Simon Msuva (Yanga SC), Shizza Kichuya (Simba SC) na Farid Mussa (Teneriffe, Hispania).

Washambuliaji wapo Mbwana Samatta (KRC Genk- Ubelgiji), Ulimwengu (AFC Eskilstuna – Sweden), Ibrahim Ajib (Simba SC), Mbaraka Yusufu (Kagera Sugar) na Abdurahman Mussa (Ruvu Shooting).


Wasaidizi wa Mayanga katika benchi la ufundi ni Novatus Fulgence ambaye ni kocha msaidizi Patrick Mwangata - kocha wa makipa pia yumo Meneja wa timu, Danny Msangi; Mtunza Vifaa, Ally Ruvu, Daktari wa timu ni Richard Yomba na Daktari wa viungo ni Gilbert Kigadye.




No comments: