Wednesday, November 15, 2017

MAGUFULI ATOA AGIZO JENGO LA TANESCO KUVUNJWA

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amemwagiza Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kuweka alama ya X kwenye jengo la Shirika la Umeme (Tanesco) na sehemu ya jengo la Wizara ya Maji na Umwagiliaji ili kupisha ujenzi wa daraja la juu katika eneo la Ubungo (Ubungo Interchange).

Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo Jumatano baada ya kuwasili jijini Dar es Salaam akitokea Chato alikokwenda baada ya kumaliza ziara ya siku tatu nchini Uganda.
  Majengo aliyoagiza JPM kupigwa alama ya X
Amewataka Tanroads kuwapa taarifa wahusika kuhusu kubomolewa kwa majengo yao ili wapate eneo la kutosha kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo unaolenga kupunguza foleni katika jiji la Dar es Salaam.

“Sasa mimi nataka ikiwezekana leo au kesho muweke X jengo la Tanesco…muweke X sehemu ile ya mwanzo ya Wizara ya Maji,” amesema Rais Magufuli huku akishangiliwa na wananchi waliojitokeza katika eneo hilo.

Kiongozi huyo Serikali amesema kwamba Sheria ya Hifadhi ya Barabara ilianza tangu mwaka 1932, ikafanyiwa mabadiliko mwaka 1959, 1964 na 1967.

“Sheria ni msumeno, Serikali ikifanya kosa inasulubiwa, Rais akijenga kwenye Road Reserve (hifadhi ya barabara) anachukuliwa hatua hizo hizo,” amesema Rais Magufuli wakati wa ziara hiyo.

Wakati wa Serikali ya Awamu ya Nne, Rais Magufuli akiwa Waziri wa Ujenzi wakati huo aliagiza kubomolewa kwa jengo la Tanesco, hata hivyo, aliyekuwa waziri mkuu, Mizengo Pinda alizuia kubomolewa kwa jengo hilo na mengine yaliyokuwa kwenye hifadhi ya barabara.

No comments: