Thursday, June 20, 2013

BAADA YA KUACHIWA NA POLISI WABUNGE WA CHADEMA WASIMULIA MKONG'OTO WALIOPATA

Lissu

Lissu, ambaye pia ni Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alilalamikia kitendo cha polisi kumwagia maji ya kuwasha baada ya kumkamata.

“Walinimwagia maji ya kuwasha kwa mfululizo nikalazimika kulala chini kifudifudi huku nikiwa nimefunika macho kukwepa yasiingie maji. “Kuna askari walitaka kunipiga lakini niliokolewa na mwenzao mmoja aliyenikinga nisishambuliwe. Kwa kweli ilikuwa hali ya hatari,” alisema.

Alisema polisi hao waliomkamata walivunja miwani yake kwa makusudi akisema aliikabidhi kaunta ikiwa haijavunjika.

“Wakati naingia mahabusu nilikabidhi miwani yangu lakini ajabu wakati tukiachiwa ilikuwa imevunjika.” Alilalamikia hatua ya polisi kuwashambulia kwa mabomu, kuwamwagia maji ya kuwasha walipokuwa wakiwatawanya watu waliokusanyika Soweto akisema awali, waliwaruhusu.
Kwa maoni yangu na maoni ya wenzangu, hakukuwa na sababu ya polisi kupiga mabomu, risasi na kumwagia watu maji ya kuwasha kwani ni wao ndiyo walituomba tubebe dhamana ya uongozi kwa kwenda kuwaomba wananchi waliokusanyika pale uwanjani kutawanyika,” alisema Lissu.

Alisema Mkuu wa Polisi Wilaya ya Arusha (OCD), Gilles Mroto ndiye aliyewaruhusu kuzungumza na wananchi ili watawanyike baada ya viwanja hivyo kuzuiwa kutumika kwa shughuli ya kuaga miili ya waliopoteza maisha kwenye tukio la bomu.

Alisema pamoja na ruhusa hiyo, polisi waliwaruhusu Chadema kuchukua magari yao yenye vipaza sauti ili wavitumie kuwatawanya wananchi hao lakini ajabu polisi ikawapiga mabomu mara baada ya Arfi kuwataka wananchi watawanyike kwenda Hospitali ya Mount Meru kutoa heshima za mwisho kwa marehemu.

“Kama ule mkusanyiko haukuwa halali, kwa nini polisi haohao walikaa na wananchi wale tangu asubuhi na wakaturuhusu kuzungumza nao ili watawanyike?”

Alisema kisheria, mkusanyiko usio halali unastahili kusambaratishwa kwa mabomu baada ya polisi kutoa ilani kwa wahusika kutawanyika tofauti na juzi akisema hawakutoa ilani yoyote.

Akunaay


Akunaay alisema polisi wanapaswa kubadilisha mbinu za kukabiliana na watu wanaodhani wamevunja sheria badala ya kukimbilia kupiga mabomu na kufyatua risasi.

“Mabomu na risasi ni kukomaza watu na kuwafanya wazoee milipuko. Itafikia hatua wananchi watajenga usugu na kuanza kupambana na polisi,” alisema na kuongeza:

“Polisi baada ya kutukamata na kutuweka chini ya ulinzi walitupiga hadi tukiwa kituoni bila sababu yoyote. Nadhani askari wetu wanapaswa kuacha kumalizia hasira zao za magumu yao yanayowakabili kwa kuwapiga watuhumiwa.”

Mukya
Mukya amelalamikia kitendo cha polisi kukataa kumpa fursa ya kumnyonyesha mtoto wake mchanga akisema malaika huyo alilazimika kushinda njaa kutwa nzima ya juzi na usiku kucha.

“Niliwaomba polisi wanikubalie kujidhamini au wanisindikize nikamnyonyeshe mtoto lakini walinikatalia kama vile ninakabiliwa na kesi ya mauaji,” alisema Mukya.

Akizungumzia suala hilo, Mwenyeki wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Susan Lyimo alisema: “Ni kinyume cha taratibu za haki za binadamu kwa mwanamke kunyimwa nafasi ya kunyonyesha mtoto wake.”

Polisi wajibu

Akizungumzia malalamiko ya wabunge hao, Kamishna Chagonja alisema hakuna mtuhumiwa ambaye anaweza kutoka mahabusu akaimwagia sifa kwa sababu siyo mahali pa kusifiwa, bali ni mahali penye kizuizi cha muda ili kuwezesha mkondo wa sheria kuchukua nafasi yake.

“Hatuna (polisi), roho ya Adolph Hitler (dikteta wa zamani wa Ujerumani), tupo kwa ajili ya kulinda wananchi na mali zao,” alisema.

Aidha, alikanusha madai ya Mukya ya kunyimwa ruhusa ya kumnyonyesha mwanaye akisema: “Siku hizi kuna dawati la jinsia katika vituo vyetu vya polisi kwa hiyo kama ni kunyonyesha lazima wangesimamia utaratibu wa kumwezesha kufanya hivyo, siyo kweli kwamba amekataliwa, haya ni maneno ya kulichafua jeshi.”

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema wanaojihusisha na uhalifu wowote huwa na imani kuwa watafanikiwa kujificha au kukwepa mkono wa dola na inapotokea wamekamatwa na kuchukuliwa hatua, huanza kujitetea kwa kuwashushia lawama polisi.

“Hasa wanasiasa na wanaharakati wakikamatwa na kuwekwa rumande, wengi hutoa manung’uniko mengi yakiwamo ya uongo, ilimradi kuchafua polisi mbele ya wananchi. Hatupo kwa ajili ya kusifiwa, bali kutimiza wajibu wetu,” alisema Sabas.



No comments: