Thursday, June 20, 2013

WAKATI TUKIMSUBIRI KUJA BONGO OBAMA AACHA GUMZO BERLINI UJERUMAN

Akikumbushia historia kali ya mji wa Berlin uliyogawika wakati mmoja, rais Barack Obama amezitahadharisha Marekani na Ulaya dhidi ya kuridhika kunakosababishwa na amani, huku akiapa kupunguza silaha za nyuklia.Rais Obama pia alitangaza kuwa programu yake ya udukuzi wa mawasiliano iliyozua zogo duniani, imenusuru maisha katika pande zote za Atlantiki. Akihutubia umati uliokusanyika katika lango kuu la Brandenburg, Obama alisema ipo haja ya kupunguza kwa sana tu, silaha za nyuklia za Marekani na Urusi, ili kuondoka katika hali ya kivita inayoendelea kuchochea kutoaminiana baina ya serikali za mataifa hayo."Tunaweza tusiishi katika hofu ya maangamizi ya nyuklia, lakini maadam silaha za nyuklia bado zinaendelea kuwepo, hatuna usalama wa kweli," alisema Obama wakati akihitimisha ziara ya siku tatu barani Ulaya, ambayo ndiyo ya kwanza tangu aliposhinda muhula wa pili. Obama anakabiliwa na migogoro ya ndani pamoja na changamoto za sera ya kigeni, ambavyo vinamvurugia malengo yake ya muhula wa pili. Masuala mawili - vita vikali vinavyoendelea nchini Syria, na program ya udukuzi wa mawasiliano - vilimzonga Obama wakati wa ziara yake nchini Ujerumani, na vile vile katika mkutano wa kundi la mataifa nane yalioendelea kiviwanda, G8 mjini Belfast, Ireland ya Kaskazini mapema wiki hii.
Ujerumani, nchi inayolinda sana faragha, ilitaka hasa majibu kutoka kwa Obama kuhusiana na Programu hiyo inayoendeshwa na shirika la usalama wa taifa la Marekani NSA. Kansela Angela Merkel, alitumia mkutano wake na Obama kwa waandishi wa habari, kutaka kuwepo na uangalifu, katika kutathmini wasiwasi kuhusu faragha, inagwa aliepuka kukwaruzana hadharani na rais.
"Kunahitajika kuwepo uwiano, haya ni mapambano ambayo yataendelea," alisema Merkel. Obama alitoa utetezi mrefu wa programu hiyo iliyoidhinishwa na mahakama, akiielezea kama juhudi makhsusi ambayo imesaidia kunusuru maisha. "Tunafahamu kuhusu mashambulizi yasiyopungua 50 ya kigaidi yaliyozuiwa kwa kutumia taarifa hizi, si tu nchini Marekani, bali pia katika maeneo mengine kama hapa Ujerumani."Tukio kuu la ziara ya Obama lilikuwa hotuba ya mchana katika lango la Brandenburg, ambako kulikuwa na ukuta wa Berlin uliyougawa mji huo kati ya mashariki na magharibi. Obama, aliesimama nyuma ya kidirisha cha bilauri isiyopita risasi, alizungumza kutoka upande wa mashariki wa lango hilo, eneo ambalo enzi hizo haikuwa rahisi kwa rais wa Marekani kukanyaga.

No comments: