Friday, August 9, 2013

HAWA NDIO WANACHAMA WA FREEMASON TANZANIA


Tanzania ina wanachama hai zaidi ya 600 wa kundi la watu wenye imani ya siri ya Freemasons wakiwa wanatokana na watu wa kada mbalimbali wakiwemo maarufu, huku ikielezwa kwamba miongoni mwao hakuna viongozi wakuu wa serikali.

           Hayo yalibainishwa na Kiongozi wa kundi la Freemasons katika eneo la Afrika Mashariki, Jayantilal Keshavji Chande maarufu kama Sir Andy Chande.
Kiongozi huyo Mtanzania mkazi wa Dar es Salaam mwenye asili ya Kiasia, alisema licha ya Tanzania kuwa na wanachama hao, kwa sasa idadi ya wanachama duniani inapungua tofauti na inavyoonekana sasa kuwa wanaongezeka kutokana na kuibuka maneno mengi kuhusu kundi hilo.

      Alisisitiza kuwa si rahisi kumjua mwanachama wa kundi hilo, bali wenyewe ndio wanaofahamiana, akisema ni siri na kwamba wenyewe wanakutana katika vikao mbalimbali mara moja kwa mwezi au zaidi.

         Alisema nchini kuna wanachama zaidi ya 600 wakiwemo wafanyabiashara, watumishi serikalini, walimu pamoja na wanataaluma mbalimbali wanaoheshimika sana na kusisitiza kuwa kuna maneno mengi yanayosemwa kuhusu kundi hilo, ambayo siyo ya kweli.
Alisema idadi ya wanachama wake duniani inazidi kupungua kutoka milioni nane hadi sasa wako milioni sita, tofauti na wengi wanaodhani kuwa idadi hiyo inaongezeka.

         Chande alizungumza na mwandishi wa habari hizi katika Shule ya Sekondari ya Shaaban Robert ambako yeye ni Mwenyekiti wa Bodi ya shule alipozungumzia maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
Alisema duniani kuna watu wazito wengi ambao ni wanachama wa kundi hilo kama majaji wakubwa na hata Binamu wa Malkia Elizabeth wa Uingereza ni kiongozi mkubwa wa kundi hilo.

       Akizungumzia masharti ya kujiunga na kundi hilo, Chande alisema ni lazima mwanachama huyo awe anaamini katika Mungu bila kubagua iwapo ni Mkristo au Muislamu.

      Alisema pia ni lazima anayetaka kujiunga awe na umri unaozidi miaka 21 na walio chini ya umri huo hawaruhusiwi kujiunga na lazima familia ya anayetaka kujiunga na wanandugu wafahamu kuwa umejiunga na kundi hilo.
“Unajua katika imani hii kuna michango mbalimbali ambayo unatakiwa kutoa ambayo ni zaidi ya dola milioni sita (karibu Sh bilioni 10), hivyo ni lazima ndugu wafahamu ili kuepuka matatizo utakapotakiwa kutoa,” alisisitiza.

          Alisema si kweli kuwa wenye fedha wengi ni wanachama wa kundi hilo huku akikanusha wanachama wanajiunga kwa ajili ya kupata fedha, bali ni dini kama imani nyingine.

       Alisisitiza kuwa hakuna ukweli kwamba wanaopata mafanikio katika maisha wakiwa ndani ya imani ya Freemasons kuwa wanatoa kafara watu wao wa karibu kwa lengo la kupata utajiri.
Chande pia alisema hairuhusiwi kutumia jina la kundi hilo kwa nia ya kujipatia nafasi sehemu mbalimbali au kuongeza nafasi katika chuo au shule.

No comments: