Wednesday, May 14, 2014

EXCLUSIVE---MWENDELEZO WA UFISADI MKUBWA BANDARI YA DAR--RAIS KIKWETE AINGILIA KATI.SOMA HAPA



Habari hii Imeandikwa  na Karoli Vinsent wa Mwandishi wa Mtandao huu na Kusaidiwa na Deodatus Balile Mhariri wa Gazeti la Jamhuri

        Siku za Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Mzee Madeni Kipande (58), kuendelea kuwa madarakani zinazidi kuyoyoma baada ya Rais Jakaya Kikwete kukerwa na tabia yake ya kutumia jina la Rais kuhalalisha matendo yake yenye kukiuka sheria za utumishi wa umma.
Habari za uhakika kutoka Ikulu na kwa baadhi ya mawaziri waandamizi, zinasema Rais Kikwete baada ya kupata taarifa za Kipande kutumia vibaya jina lake, alichukia na kuamua kumwita Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, na kumpa maagizo mazito.

      “Tena wala haikuwa siri, Rais alimwita Dk. Mwakyembe kama wiki mbili zilizopita mbele yetu mawaziri kama wanne hivi akamfokea,” kimesema chanzo chetu. “Alimpa maagizo ya wazi kuwa hafurahishwi na hataki jina lake litumiwe vibaya na Kipande kukandamizi watu wengine.


     “Alimtaka Dk. Mwakyembe kufuatilia na kumpa taarifa juu ya utendaji wa kipande, na iwapo alidanganya kiwango cha mapato kuwa kimeongezeka, unyanyasaji wa wafanyakazi, kukaidi maagizo ya Bodi akidhani ana kinga ya Rais na kutamba kwenye corridor (viambaza) kuwa hakuna anayemueza yeye ana mizizi mizito.

      “Baada ya maagizo hayo, Dk. Mwakyembe hakubisha, bali alimwambia Rais kuwa atatekeleza. Ninachokwambia hiki wala hakitiliwi shaka, hata Mwakyembe mwenyewe hawezi kujitokeza akasema hajaelekezwa, na iwapo hatatekeleza aliyoelekezwa na Rais basi ni wazi naye atakuwa anakaidi maelekezo halali ya Mheshimiwa Rais sawa na Kipande anavyokaidi maelekezo ya Bodi,” mmoja wa mawaziri waandamizi ameumbia Gazeti moja la wiki ilinalofuatilia Sakata hilo, mwishoni mwa wiki.

       Habari za uhakika kutoka Ikulu zinasema baada ya gazeti hilo la wiki kuchapisha taarifa za unyanyasaji anaofanya Kipande bandarini na vifo vya wafanyakazi watatu --  Peter Gwamaka Kitangalala, Dotto Mbega  na mwingine aliyefahamika kwa jina la Oluwochi -- kuwa wamefariki dunia katika kipindi cha miezi mitatu kutokana na shinikizo la damu lililozaa kiharusi baada ya vitisho vya Kipande, Rais Kikwete amesikitika mno na kusema hilo halipaswi kutokea.

      “Rais alisema mtu anapofika mahala akasababisha kifo cha mtu, ama moja kwa moja au kwa njia yoyote, basi hiyo haivumiliki,” amesema mfanyakazi wa Ikulu, akisisitiza kuwa vyombo vya dola vinapaswa kuchunguza hali hiyo na ikibainika ni kweli hatua za kisheria zichukuliwe dhidi ya waliosababisha vifo hivyo.

        “Baada ya Mtawa na Shaaban Gurumo kuona moto umewaka, wakaamua kuwaita wahariri wa gazeti linalomilikiwa na kuhaririwa na wazawa wa Bagamoyo, kwa nia ile ile ya kuendeleza ukabila kama mlivyoandika, akatumia gazeti linalohaririwa na mhariri anayetoka kijijini kwao kuthibitisha tuhuma dhidi yake bila kujua,” kimesema chanzo chetu.

        Katika gazeti hilo la wiki, chapisho la Aprili 16 -22, 2014 Kipande hakukanusha tuhuma kuwa alimtukana Balozi wa Japan, Masaki Okada, au kuwa alimdanganya Waziri wa Uchukuzi, Dk. Mwakyembe, kwamba mapato ya Bandari yamefikia Sh bilioni 50.

       Wiki mbili zilizopita, Madeni Kipande amemtukana Balozi wa Japan nchini, Okada. Balozi Okada alikwenda ofisini kwa Kipande kumweleza nia ya Japan kutoa msaada wa kukarabati gati Na. 1-7 kama msaada, lakini kinyume cha matarajio kwamba Kipande angepokea msaada huo, aliishia kumrushia matusi Balozi wa Japan.
       
         “Kwanza alikuwa amekataa kumuona huyo Balozi, akisema aonane na wasaidizi wake, lakini Balozi aliposisitiza msaidizi wa Kipande akamwambia protokali zinamtaka amuone, akakubali kumuona. Kilichotokea baada ya hapo kilikuwa kituko. Balozi alimweleza kuwa anataka nchi yake isaidie kukarabati gati Na. 1-7 la bandari. Kipande akamwambia Bandari ilitangaza zabuni, na Japan kama ilikuwa inataka kufanya hivyo ilipaswa kuomba zabuni na kuingia kwenye ushindani.
        
     “Balozi alisisitiza kuwa nia yake ni kutoa msaada si kufanya biashara, Kipande akasema huo ni uongo kwani amezoea kauli za aina hiyo na ni ujanja wa kupenyeza rushwa na kuzipatia kazi kampuni za Kijapani kwa njia za panya, hivyo yeye hatakubali kama Japan inataka kutoa msaada wa ukarabati wa bandari basi isubiri zabuni ijayo.

          “Kauli kwamba Japan inataka kutumia mkondo wa ubalozi kwa njia ya rushwa kuzipatia kampuni za nchini kwake kazi wakati nchi hiyo ililenga kutoa msaada ilimuuma mno Balozi, na taarifa zilizopo anataka au tayari ameandika barua kwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kutaka ufafanuzi kwanini nchi yake ya Japan ihusishwe na rushwa kwa kutaka kuisaidia Tanzania,” kimesema chanzo chetu.
    
          Afisa Mwandamizi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ameiambia Gazeti hilo la wiki kuwa wizara yake inalishughulikia kwa nguvu suala hilo kunusuru uhusiano wa Tanzania na Japan.

       “Tanzania na Japan zimekuwa nchi marafiki na taifa hili limekuwa msaada mkubwa kwetu. Leo kumtukana Balozi na nchi yao ni utovu wa nidhamu wa hali ya juu. Tunalishughulikia hili na Kipande ni lazima ataondolewa angalau kwa kosa hili linaloweza kuigharimu Tanzania katika dunia ya diplomasia tusipochukua hatua,” amesema afisa huyo.

          Kuhusiana na kifo cha Mbega, gazeti hilo likimnukuu mtu waliyemwita mtaalamu au daktari wa binadamu, lilikiri uwezekano wa kifo cha Mbega kutokana na shikizo la Kipande, liliposema: “Kwa hili [la kifo cha Mbega] naweza kukubaliana na wewe kitaalamu, maana huyu alikuwa ni mtu wa karibu na hazina ya Bandari na sasa fedha zimeibwa kwa mamilioni, wewe ndiye uliyekuwa mlinzi wa lango la fedha sasa zimepotea, iwe umeiba wewe au umeibiwa na hasa kama umeibiwa ni lazima uchanganyikiwe na hata kupata shinikizo la damu linaloweza kukusababishia kifo,” mtaalamu alifafanua kupitia gazeti hilo.


No comments: