Wednesday, June 25, 2014

EXCLUSIVE--WALIOMKASHFU MBOWE NA VIONGOZI WA CHADEMA JUU YA UFISADI WAJIBIWA--SOMA TAMKO LOTE HAPA


 Ndugu wanahabari,wanachama na wapenzi wa chama cha Demokrasia na maendeleo kanda ya magharibi na nchini kwa ujumla.

       Tumewaalika leo hii ili kuja kuweka sawa kwa kile kinachoendelea kwa baadhi ya wanachama wa CHADEMA ambao hawana mapenzi mema na chama kwa kile walichokitoa mbele ya wanahabari huku wakiwa wamejivika vyeo ambavyo ama havipo au wamekaimishwa au wamekwishavuliwa hapo awali. Taarifa iliyopewa kichwa 

    ”TAARIFA YA WAJUMBE WA BARAZA KUU NA MKUTANO MKUU WA CHADEMA KWA UMMA” iliyotolewa tarehe 23/06/2014 katika Hoteli ya Lamada iliyopo jijini Dar es Salaam.

                              Ndugu wanahabari.
Mtindo huu umezuka sana hivi karibuni ambao kwa namna moja ama nyingine unaratibiwa na viongozi wa CCM kwa mgongo wa waliokuwa viongozi wa CHADEMA ambao kwa sasa ni viongozi wa chama kipya cha Alliance for Change and Transparence – Tanzania (ACT - Tanzania). Tunasema ni viongozi wa ACT - Tanzania kwa sababu ushahidi wa kimazingira, wa kimuonekano, wa kimwenendo na vidhibitisho visivyokuwa na shaka vipo!


     USHAHIDI WA KIMAZINGIRA

                   Ndugu wanahabari.
Viongozi wote waliotajwa/kujitaja kuhusika na utoaji wa Tamko lililotolewa tarehe 23/06/2014 katika Hoteli ya Lamada jijini Dar – es – Salaam linaloelezea vipengere vikuu vitatu vya tamko hilo ambavyo ni;

KUSHINDWA KWA UONGOZI WA KITAIFA
UBADHILIFU WA FEDHA NA MALI ZA CHAMA
UVUNJIFU WA KATIBA NA KANUNI ZA CHAMA

    Viongozi waliotajwa/kujitaja ni watu walioonekana kushiriki shughuli za ACT zaidi kuliko za CHADEMA tokea mchakato wa kuanzishwa kwa chama hicho hadi hivi leo.

      USHAHIDI WA KIMUONEKANO

               Ndugu wanahabari.
Katika hali ya kawaida tu ambayo haihitaji kuumiza kichwa kuelewa kuwa hawa si wenzetu ni kitendo cha kuwashutumu viongozi wa kitaifa kuwa wameshindwa kiuongozi na wao kujinadi kuwa ndio waliopambana kwenye uchaguzi wa 2010 sehemu mbalimbali. Kwa hali ilivyo sasa kama uongozi wa kitaifa wangekuwa wameshindwa kiuongozi CHADEMA isingekuwa na wanachama imara ambao ni wengi wasioteteleka kama ilivyo hivi sasa.

           Ndugu wanahabari.
Anayejiita katibu wa CHADEMA ndugu Athumani Balozi wakati hakuna mkutano uliofanyika na kumchagua, pia anajiita mjumbe wa baraza la mashauriano Kanda ya Magharibi wakati baraza hilo halipo kwa mujibu wa muundo wa chama ngazi ya kanda, huu ni ushahidi tosha wa kimuonekano kuwa mjumbe hajui mfumo wa chama kwa sasa hivyo kuuaminisha umma kuwa anachokifahamu yeye ni labda mfumo uliopo katika chama chake kipya cha ACT – Tanzania na sio CHADEMA.

           USHAHIDI WA KIMWENENDO
Ndugu wanahabari.
Katika hali ya kawaida ukiwa kiongozi lazima uwe mtu wa mfano ili unaowaongoza waige kutoka kwako. Wajumbe waliojiita wawakilishi wa mawazo ya wanachadema wa mikoa walikotoka ni wazi kabisa kimwenendo wametenda kosa la kusema uongo na kuendeleza unafiki wa kitoto wa kusema kuwa wanawakilisha mawazo yetu kwanza tulikaalini ili kuazimia na kuwatuma wao wafikishe mawazo hayo. 

    Tunachokumbuka ni kuwa tulikuwa na kikao kilichokuwa kinajadili uhai wa chama katika mkoa wa Tabora ambapo Kaimu Katibu ndugu Athumani Barozi alishutumiwa kurudisha nyuma jitihada za uenezaji wa chama na pia kushiriki vitendo vya kupandikiza chuki kwa wanachadema ili wahamie ACT - Tanzania. Baada ya shutuma hizo ndugu Athumani Barozi alihamaki na kutoka katika kikao huku akitoa maneno ya vitisho vya kupiga wajumbe.

           Ndugu wanahabari.
Vitendo hivyo walivyovifanya ndugu Athumani Barozi, Halima Katundu, Jorum Mbogo na Hussein Kundecha vya kuudanganya umma wa Watanzania kuwa tumewatuma kufikisha mawazo yetu wakati hakuna kikao wala muhtasari unaozungumzia agizo hilo ni unafiki, uzandiki na ni mchezo wa kitoto kwani kitendo cha kusema uongo ni kosa la jinai.

        USHAHIDI WA VIDHIBITISHO VISIVYOKUWA NA SHAKA
Ndugu wanahabari.
Mbali na upatikanaji wa kadi za ACT – Tanzania zilizokuwa zikisambazwa na wajumbe hao ambapo kila walipowaona vijana wa CHADEMA waliingiwa na hofu na kushindwa kuendelea na zoezi hilo. Lakini pia kitendo cha kuhamasisha uteremshwaji wa bendera za CHADEMA kwenye mawe ya Msingi yaliyojengwa kwa nguvu za wanachadema kisha kupandishwa bendera za ACT - Tanzania. 

         Kitendo hiki kimetokea katika kata ya Ng’ambo ambapo ndugu Athuman Barozi anaishi. Hata pia ushahidi unazidi kujidihirisha kwenye orodha ya wajumbe walioshiriki kwani watu walioandika katika orodha hiyo (nakala imeambataniswa) si sawa na idadi ya wajumbe thelathini na nane (38) walioorodheshwa katika hali ya ushahidi wa kimaandishi. Mwandiko wa kutumia mkono hauwezi kuwa sawa kwa watu 38 kama inavyoonekana katika orodha hiyo. 

            Hata hivyo mjumbe aliyetambulishwa kuhudhuria katika zoezi la utoaji tamko kutoka Tanga ndugu Khalid Hassan (Imeandikwa Halid Halfan) kuwa ni katibu wa wilaya ya Tanga amejitokeza kukanusha uwepo wake kusema kuwa, “kwa sasa yeye si katibu kwani alikwisha simamishwa nyazifa hiyo na alikubali kutii amri”. Pia hata jina lake lilivyoandikwa kwenye orodha si sahihi na yeye anavyoliandika inaonekana kuna mtu aliyeliandika.

        Ndugu wanahabari.
Hali hii inajidhihirisha kuwa huu ni unafiki na kutangatanga kwa watu wanaotaka kuondoka CHADEMA kwa njia ya kufukuzwa ili wapate pa kutafutia huruma ya Watanzania.

MAADHIMIO YA WAJUMBE DHIDI YA TUHUMA TATU ZILIZOTOLEWA KATIKA TAMKO LA AKINA ATHUMANI BAROZI NA WENZAKE.
KUSHINDWA KWA UONGOZI WA KITAIFA

             Ndugu wanahabari.
Kwa kuwa kwenye tamko limetaja kuwa waliolitoa wanatuwakilisha sisi wanachadema tuliobaki mikoani, hatutambui uwakilishi wao kwani hali hiyo iliyozungumziwa katika kipengele hiki hatuiafiki hata mara moja.
Ifahamike kuwa aliyetajwa katika kipengele hiki (Zitto Kabwe) kuwa zimetumika kiasi cha mabilioni kwenda kumshambulia na wakaongeza kuwa haya ni matendo ya unafiki wa kisiasa. 

          Tunapenda watambue kuwa Zitto Kabwe hakuzaliwa ili awe kiongozi wa CHADEMA, kuwa kiongozi ni mtu anayekubalika na anaowaongoza na sio kuandaa kikundi cha watu ambao ni wachumia tumbo ili kukulinda pindi utakapokosea.

                 Ndugu wanahabari.
Wanaotajwa kushindwa katika kipengele hiki ambao ni Mwenyekiti Mh. Freeman Mbowe na Katibu Mkuu Dkt. Wilbrod P. Slaa si kweli kwa sababu kwa sasa CHADEMA imeenea sehemu kubwa hii ni kutoka na ubunifu wa kushusha madaraka katika ngazi ya kanda hali inayowanyima kupata mwanya wa kufanya udanganyifu ulioozoeleka kwa baadhi ya viongozi wa mikoani kudanganya kuwa wanafanyakazi ya kueneza chama kumbe wanadidimiza chama. Sasa wamebanwa na viongozi wa ngazi ya kanda hivyo kupeleka tuhuma kwa uongozi wa Kitaifa.

           UBADHILIFU WA FEDHA NA MALI ZA CHAMA
Ndugu wanahabari.
Kinachotajwa katika kipengele hiki kwenye tamko la akina Athumani Barozi na wenzake ni muendelezo wa riwaya za kinafiki ambazo zinatungwa na wafitini waliomo ndani ya chama na washirika wao ambao kwa namna moja au nyingine mianya ya wao kujinufaisha na fungu la fedha za ruzuku zilizokuwa zinakuja kutoka makao makuu na kuwafikia imefungwa.

          Haingii akilini Mwenyekiti Mh. Mbowe kujilipa shilingi MILLIONI 700 kila siku kama walivyodai kwenye tamko lao, basi mtu huyu angekuwa tajiri wa kupindukia.

               Ndugu wanahabari.
Akina Athumani wanaendelea kusema kuwa Dkt. Slaa analipwa kiasi cha shilingi million 130 kwa mwaka na wao makatibu na viongozi wa mkoa wanalipwa zero (0). Wanatoa hoja dhaifu na ni mfu bila ya kuangalia kazi zinazofanywa na katibu mkuu za kujenga chama huku wao wanataka walipwe kwa kazi wanazozifanya za kubomoa chama. Huu ni ujinga!

            Ndugu wanahabari.
Akina Athumani na wenzake wanatolea macho ruzuku ya chama ambayo kwa mujibu wa tamko lao ni shilingi million 239 kisha wanasema chama hakina jengo la ofisi hata moja mikoani na kuishia kupanga kwenye fremu za maduka. Hali hii ya kupanga kwenye fremu za maduka zimesababishwa na viongozi wenye njaa ya kutegemea fedha za pango la ofisi ili waweze kuponea hapo. 

           Mbona uongozi wa Kanda umeweza kupata ofisi yenye hadhi ya kuitwa ofisi? Hapa naomba mjiulize kwa nini yeye Athumani ambaye amejitambulisha kuwa ni katibu wa Mkoa wa Tabora apange kwenye fremu ya duka ili hali ruzuku ilikuwa inamfikia? Kwa kuthibitisha hili ni taarifa za kibenki ambazo zilionesha fedha kuingia na hata michango ya wanachama ambazo hazijawahi kutolewa ufafanuzi wa matumizi yake.

                 Ndugu wanahabari.
Kundi hili la akina Athumani linajitokeza na kumtetea kiongozi aliyeingiza fedha kwenye akaunti ya chama mkoa wa Tabora kiasi cha shilingi million mbili (2,000,000/) tarehe 09/05/2013 ambazo zilitumika bila hata mhasibu wa mkoa kujua! Sasa wajumbe tunamuuliza Athumani Barozi na wenzake fedha hizo zililetwa kwa kazi gani na kwa nini ziliingia kwa jina la mtu na si chama?

           UVUNJIFU WA KATIBA NA KANUNI ZA CHAMA
Ndugu wanahabari.
Katika kipengele hiki wajumbe hao wakiongozwa na Athumani Barozi katika tamko lao, wametaja vipengele vitatu vya katiba ya chama vilivyovunjwa, na tunazitolea ufafanuzi kama ifuatavyo:

       Kitendo cha kutoka na kususia kwenye Bunge maalum la Katiba
Ndugu wanahabari.

          Hakuna mtanzania hata mmoja awe anatoka Tanganyika au Zanzibar ambaye hakushuhudia kilichokuwa kinatendeka ndani ya Bunge hilo, kilichofanywa na WanaCCM na washirika wao dhidi ya wapenda mabadiliko. Hali iliyopelekea wapenda mabadiliko kuungana na kuunda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA). 

        Kitendo cha kuendelea kukaa ndani ya bunge hilo viongozi wetu wangekuwa wamebariki matusi, kejeli na vijembe vilivyokuwa vikitolewa na walioitwa INTARAHAMWE. Kwa hali hiyo yeyote anayeshabikia na kuwalaumu waliotoka bungeni na yeye ni mmoja wa kundi la INTARAHAMWE.

         Kitendo cha kuunda baraza kivuli la mseto.
Ndugu wanahabari.
Ukiona ndugu yako anachukia wewe kupatana na adui yako basi ujue yeye ni adui yako mara mia.

    Hakuna asiyejua mbinu wanayoitumia CCM kutugawa hasa sisi tunaoitwa vyama pinzani. CCM waliwahi kusema CUF ni chama cha Kiisilamu, CHADEMA ni chama cha Wakristo ila NCCR-MAGEUZI wao waliambiwa mkiwachagua hawa vita itatokea. Sasa viongozi wa vyama hivi wameona ni busara kuungana ili kuunganisha nguvu kwa lengo la kumkomesha na kumuondoa adui wa Watanzania ambaye ametunyonya kwa miaka 50 sasa. Leo hii mawakala wa CCM wanakuja na hoja dhaifu na mfu eti kwa nini tumeungana!

        Kutokuitishwa kwa mkutano mkuu wa Baraza kuu
Ndugu wanahabari.
Mawakala hao wa CCM hapa hawana hoja zaidi ya kuendeleza riwaya iliyotungwa na Ndugu Nape Nnauye na Katibu wake Kinana ya kutaka kuitishwa kwa mkutano mkuu ili waweze kutimiza azma yao ya kupenyeza virusi na kisha kutimiza maneno ya Wasira kuwa CHADEMA itakufa kabla ya 2014.

          MWISHO.

            Tunawashukuru sana wanahabari na tunaomba mfikishe taarifa hii kwa umma ili itambue kuwa kile kilichotolewa na kundi la mawakala wa CCM linaloongozwa na Athuman ambaye ameamua kujitokeza rasmi na hata wale waliopo nyuma yake ni UNAFIKI na UDHAIFU wa hoja ambazo hutolewa na mtu aliyebanwa au kukatiwa mirija ya kujipatia fedha kwa njia haramu.
IMEANDALIWA NA KUSOMWA leo tarehe 25/06/2014
CHRISTOPHER M.M.NYAMWANJI
MRATIBU KANDA YA MAGHARIBI


No comments: