Thursday, November 27, 2014

MBOWE ALIPOMTAKA PINDA AACHIE NGAZI LEO SIKILIZA NA SOMA ALICHOJIBIWA





Kikao cha Bunge leo Novemba 27 kimeanza kwa maswali mawili kuulizwa na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni Freeman Mbowe kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
…Chini ya uongozi wako kama Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ukiwa kiongozi wa shughuli za Kiserikali Bungen, tumeiona Serikali ikikumbana na matatizo na vikwazo vingi ikiwemo ‘Operesheni Tokomeza’ ambayo ilipelekea wananchi wengi kupoteza maisha na wengine kupata vilema…“– Mbowe.
Tumeona mauaji ya raia yakiendelea Kiteto, kashfa kubwa ambayo iko current sasa hivi ikiwa ni pamoja na kauli zako ulizowahi kuzisema kwamba fedha zilizopotea za akaunti ya Escrow hazikuwa fedha za umma bali zilikuwa fedha za watu binafsi…“– Mbowe.
Baada ya Ripoti ya CAG kutolewa hadharani kuhusiana na fedha za Escrow na baada ya Ripoti ya PCCB kutolewa na hatimaye jana hapa Bungeni kusomwa taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, nini msimamo wako kuhusu kauli yako ya awali kwamba fedha zile zilikuwa ni za watu binafsi na sio fedha za umma?– Mbowe.
Kwa uzito huo ukichanganya na matukio mengine mbalimbali ambayo yamepelekea fedheha kubwa kwa taifa letu, huoni kama ingekuwa muafaka kwako binafsi na taifa kupumzika kidogo ili kupisha nafasi kwa watu wengine kuweza kumalizia ngwe hii ya utawala wenu?”– Mbowe.
Akijibu maswali hayo, Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema; “…Inawezekana Mheshimiwa Mbowe una shauku ya kutaka litokee hilo lakini mambo haya yanategemea kama ndivyo Mungu kapanga au hapana…
Ningeweza nikajaribu kukujibu lakini sina sababu ya kufanya hivyo, sina sababu ya kufanya hivyo kwa sababu suala lenyewe ndiyo subject ya mjadala hapa Bungeni ambao unaanza leo.. Tusubiri mjadala utakavyokwenda naamini na mimi nitapata nafasi ya kusema mawili matatu, kwa hiyo nadhani mwisho wa yote Bunge litakuwa limefikia mahali ambapo tunaweza tukasema kwa uhakika ni hatua stahiki namna gani inaweza kuchukuliwa…” Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Baada ya majibu hayo, Mbowe alipata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa Waziri Mkuu; “…Pamoja na kwamba jambo hili litajitokeza baadaye katika mijadala ya leo, bado haiondoi ukweli kwamba una wajibu wa kulijibu swali langu. Naomba kwa heshima sana nikuulize tena kwa mara nyingine, taifa limepata fedheha kubwa sana kutokana na sakata hili, nchi nzima inasikiliza tatizo hili…“– Mbowe.
…Una heshima kama kiongozi wa Serikali lakini heshima ambayo itakuwa imethibitishwa zaidi kama utaamua kujiwajibisha mwenyewe ili kuweka heshima yako na heshima ya Serikali, je kwa mara nyingine huoni ingekuwa vema kama basi utujibu kama unafikiri bado zile fedha ni za umma kama hutaki ku-declare kujiuzulu katika hatua ya sasa?”–Mbowe.
Akijibu swali hilo, Waziri Mkuu amesema; “…Naomba nirudie nilichosema, suala la kujiuzulu si jipya lakini maadam jambo hili liko hapa Bungeni, unatanguliza hili jambo kwanini? Tungoje tujadili tufikie mwisho halafu tutaamua…”– Mizengo Pinda.
Nimekurekodia sauti ya wakati maswali hayo yakiulizwa na kujibiwa Bungeni leo Dodoma, unaweza kusikiliza kwa kubonyeza play.

No comments: