Friday, January 9, 2015

TAIFA STARS MABORESHO NA RWANDA KUCHEZA MWANZA JAN 22


                                                                                                            


Kikosi cha Taifa Stars Maboresho kitacheza mechi ya kirafiki na timu ya Taifa ya Rwanda itakayofanyika Januari 22 mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mechi hiyo ni sehemu ya programu ya Kocha Mart Nooij kuiandaa timu hiyo kwa ajili ya mechi za mchujo michuano ya Afrika kwa Wachezaji wanaocheza Ligi za Ndani (CHAN). Mechi za mchujo za michuano hiyo ambayo fainali zake zitafanyika mwakani nchini Rwanda zinaanza Mei mwaka huu.

Kocha Nooij anatarajia wakati wowote kutangaza kikosi cha timu hiyo inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ambacho kitakusanyika Januari 18 mwaka huu jijini Dar es Salaam, na siku moja baadaye kwenda jijini Mwanza.
STORY ZINGINE KUTOKA TFF LEO ZIKO CHINI

TAIFA CUP WANAWAKE KUPIGWA JUMAMOSI
Mechi za kwanza za raundi ya kwanza za mashindano ya Taifa ya mpira wa miguu kwa wanawake (Taifa Cup Wanawake) zinachezwa kesho (Januari 10 mwaka huu) kwenye miji 11 tofauti nchini.

Katika mashindano hayo yanayodhaminiwa na kampuni ya Proin, Geita itakuwa mwenyeji wa Kagera (Uwanja wa Geita), Tabora itacheza na Kigoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, Simiyu na Shinyanga (Uwanja wa Simiyu), Arusha na Manyara (Sheikh Kaluta Amri Abeid), na Kilimanjaro na Tanga (Uwanja wa Ushirika).

Mechi nyingine ni Lindi itaikaribisha Mtwara kwenye Uwanja wa Ilulu, Ruvuma na Njombe (Uwanja wa Majimaji), Mbeya na Iringa (Uwanja wa Sokoine), Katavi na Rukwa (Uwanja wa Katavi), Dodoma na Singida (Uwanja wa Jamhuri) na Pwani itakuwa mwenyeji wa Morogoro katika Uwanja wa Mabatini.

Timu hizo zitarudiana Januari 13 mwaka huu, ambapo baada ya matokeo ya nyumbani na ugenini timu iliyoshinda ndiyo itakayoingia hatua inayofuata ambayo pia itashirikisha mikoa ya kisoka ya Ilala, Kinondoni na Temeke.

Hatua hiyo, mechi zake za kwanza zitachezwa Januari 17 mwaka huu wakati zile za marudiano zitafanyika Januari 21 mwaka huu.

Baada ya hapo, hatua itakayofuata ni robo fainali, nusu fainali na fainali ambayo ndiyo itakayotoa bingwa wa michuano hiyo inayofanyika kwa mara ya kwanza nchini.

KILUVYA UTD, NJOMBE BADO ZAKIMBIZA SDL
Kiluvya United ya Pwani na Njombe Mji ya mkoani Njombe ndizo timu pekee zilizomaliza mzunguko wa kwanza wa Ligi Daraja la Pili (SDL) kwa kushinda mechi zote katika makundi yao, hivyo kujipatia pointi 15 kila moja.

Njombe Mji imeongoza kundi D lenye timu za Mkamba Rangers ya Morogoro iliyofikisha pointi nane, Wenda ya Mbeya pointi sita, Volcano FC ya Morogoro pointi sita, Town Small Boys ya Ruvuma pointi tano na Magereza ya Iringa yenye pointi moja.

Katika kundi C, Kiluvya United inafuatiwa na Mshikamano ya Dar es Salaam yenye pointi kumi, Abajalo pia ya Dar es Salaam pointi saba, Cosmopolitan na Transit Camp za Dar es Salaam ambazo kila moja imemaliza mzunguko huo ikiwa na pointi tano. Kariakoo ya Lindi haina pointi.

Mji Mkuu (CDA) ya Dodoma na Singida United ya Singida ndizo zinazochuana katika kundi A kila moja ikiwa na pointi nane. Mvuvuma FC ya Kigoma yenye pointi tano ndiyo inayofuatia, wakati Milambo ya Tabora ina pointi nne huku Ujenzi Rukwa ikikamata mkia kwa pointi moja.

Pia mchuano mkali uko katika kundi B ambapo JKT Rwamkoma ya Mara na Mbao FC ya Mwanza ziko kileleni kila moja ikiwa na pointi tisa. AFC ya Arusha inafuatia kwa pointi sita, Bulyanhulu FC ya Shinyanga ina pointi nne wakati Pamba FC ya Mwanza iko mkiani kwa pointi moja.

Mzunguko wa pili wa ligi hiyo itakayotoa timu nne zitakazopanda daraja kucheza Ligi Daraja la Kwanza msimu ujao (2015/2016) utaanza kutimua vumbi Januari 24 mwaka huu.


IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)

No comments: