Thursday, March 5, 2015

WALICHOKIFANYA WALEMAVU WA NGOZI (ALBINO) IKULU LEO,KIKAO CHAO CHASHINDWA KUAFANYIKA

Vurugu zilizofanywa na baadhi ya walemavu wa ngozi Albino katika Ikulu ya Tanzania zimesababisha kuahirishwa kwa kikao kati ya viongozi wao na Rais Jakaya Kikwete.
Rais Kikwete alikuwa akitarajiwa kufanya mkutano na viongozi wa Albino Tanzania TAS aliowaalika kuzungumzia hoja zao kutokana na mauaji ya walemavu hao yanayoendelea nchini humo.

Lakini heka heka iliyotokea katika eneo la mapokezi iliwalazimu maafisa wa Ikulu kuwatawanya walemavu hao.

Ni muda mfupi baada ya ukaguzi kuanza kufanyika katika moja ya lango la kuingilia Ikulu, kundi moja la walemavu hao waliokuwa katika moja ya chumba wakaanzisha malalamiko kwa sauti huku viongozi wao wakiwa wanajiandaa kuruhusiwa na kuingia ndani.

Kelele hizo na mabishano hayo miongoni mwa walemavu hao kwa mbali ikaanza kuonekana ni dosari namba moja hasa baada ya kupandisha mori na kila mtu kuanza kusema lake kupinga ushiriki wa viongozi hao. 

Kutokana na vurugu hizo maafisa wa Ikulu waliwatawanya Walemavu hao kutoka nje ya Geti, na hapo ikawa mwanzo wa sakata jipya baada ya kuanza kulumbana na viongozi wao na hatimaye kuanza kupigana na mambo yakawa hivi.

Baada ya kutulizwa ugomvi kilichofuata ni nyimbo za kupinga uhalali wa viongozi wao. Hata hivyi vurugu hizi zinatazamwa tofauti na baadhi ya walemavu hao, ambao wanasema ni vurugu hizo zimepoteza fursa ya kuwasilisha matatizo yao kwa Rais

Chanzo: BBC swahili

No comments: