Thursday, October 15, 2015

Pigo kubwa UKAWA--DK MAKAIDI afariki Dunia

Mwenyekiti wa chama cha National League for Democracy (NLD) na Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, Marehemu Emmanuel Makaidi

MWENYEKITI wa Chama cha National League for Democracy (NLD) ambaye pia ni mgombea ubunge Jimbo la Masasi mkoani Mtwara, Dk. Emmanuel Makaidi amefariki dunia mchana huu. Anaandika Pendo Omary … (endelea).

Mke wa marehemu, Modesta Makaidi, amethibitisha kifo cha Dk. Makaidi akisema “kimetokea katika hospitali ya Nyangao, kiasi cha saa 9 mchana.”

Modesta amesema walimpeleka hospitali haraka Dk. Makaidi baada ya hali yake kubadilika ghafla nyumbani kwake mjini Masasi wakati akijaandaa kutekeleza ratiba yake ya shughuli za kampeni ya uchaguzi.

“Ni kweli Makaidi amefariki, kama dakika 45 zilizopita. Mimi ni mke wake naitwa Modesta Makaidi,” amesema alipopigiwa simu na mwandishi wa habari hizi kuulizwa juu ya taarifa zilizopatikana awali kuhusu hali ya Dk. Makaidi.

Modesta amesema “juzi wakati Makaidi akiwa anaenda Kata ya Mbonde, ghafla alijisikia vibaya. Tukampeleka zahanati ya Best ambako ikabainika ana presha kubwa. Akapewa dripu. Jioni akaruhusiwa. Leo akaamka vizuri, lakini hali yake ikabadilika. Ndipo tukampeleka hospitali.”

Aidha, Khamis Hamad, Katibu Mwenezi na msemaji wa NLD, ambaye awali alipopigiwasimu kuulizwa taarifa hizo alishtuka akisema hakuwa na habari, alithibitisha kuwa tayari chama kimepokea taarifa na kwamba walitarajia kufanya kikao jana kujadili namna ya kushiriki katika msiba huo.

“Ni kweli, tumethibitisha kifo cha Mwenyekiti wetu, Dk. Makaidi. Tunajiandaa kuelekea Ngome kufanya kikao pamoja na vyama washirika wa Ukawa, na baadaye kwa familia yamarehemu Dk. Makaidi. Na tutatoa taarifa kadri zitakavyopatikana,” amesema Khamis.

Dk. Makaidi aliteuliwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kugombea ubunge jimbo la Masasi likiwa moja ya majimbo matatu ambayo chama hicho kilipata katika mgao wa viti vya ubunge, uliosimamiwa na muungano huo unaoshirikisha pia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama Cha Wananchi (CUF) na NCCR-Mageuzi.

Majimbo mengine ambayo NLD ilipewa katika mgao wa maridhiano wa Ukawa ni Ndanda na Lulindi yote yakiwepo mkoani Mtwara.
Hata hivyo, ugombeaji wake ulipata kikwazo baada ya wananchi jimboni kumgomea.

Wananchi hao walitamka mbele ya mgombea urais anayewakilisha Ukawa, Edward Lowassa kwamba chaguo lao ni Ismail Makombe (Kundambanda), aliyeteuliwa na CUF kabla ya mgao wa majimbo kutangazwa.

Lowassa ambaye alipita Masasi wiki tatu zilizopita kuomba ridhaa ya wananchi, alitoa fursa kwa wagombea wote wawili kuhutubia wananchi kwenye mkutano huo na akawauliza ni yupi watakaemchagua, wakajibu “tunamtaka Kundambanda.”
Dk. Makaidi aligoma hata Lowassa alipotoa kauli kuwa angeachia uamuzi wa wananchi; aliondoka mkutanoni na akashutumu alichoita mpango wa hujuma unaolenga kunufaisha adui zake Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Aliendelea kufanya kampeni na akaapa kuendelea mpaka siku ya mwisho kwa kuwa anauhakika “nitaiangusha CCM.”
Dk. Makaidi aliungana na viongozi wakuu wa vyama vya UKAWA tangu wakati wa Bunge Maalum la Katiba akiwa amepinga mkakati wa CCM kuvuruga Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kutokana na maoni ya wananchi.

Wakati fulani Dk. Makaidi alisema wazi kuwa ameamua kuungana na UKAWA kwa sababu anaamini Tanzania inahitaji mabadiliko sasa.
Akiwa mmoja wa wenyeviti wenza wa umoja huo, alijijengea umaarufu kwa hatua yake hiyo huku akitajika zaidi kwa kaulimbiu ya chama chake ya “NLD motomoto moto.”

Siku ambayo Lowassa alitambulishwa rasmi kujiunga na Chadema, katika salamu zake za pongezi, Dk. Makaidi alimwambia Lowassa, “sasa umekuja huku kwetu itabidi utufuate sisi kwa haya tunayoyapigania UKAWA, yale ya kule CCM uyaache kule.”

Kifo cha Dk. Makaidi kitasababisha uchaguzi wa jimbo hilo kuhairishwa, na kjuwa jimbo la tano la ubunge uchaguzi wake kuhairishwa baada ya wagombea kufariki. Majimbo hayo ni Lushoto mgombea aliyefariki, Mohamed Mtoi (Chadema), Handeni Mjini mgombea Dk. Abdallah Kigoda (CCM), Ulanga Mashariki mgombea ni Celina Kombani (CCM) na Arusha Mjini, Estomih Malla (ACT).

No comments: