Thursday, June 2, 2016

UPINZANI WAWASILISHA HOJA RASMI YA KUMNGOA NAIBU SPIKA BUNGENI


Wabunge wa upinzani wamewasilisha kwa Spika wa Bunge hoja ya kumwondoa madarakani Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kwa kutokuwa na imani naye. 



Hatua hiyo imefikiwa na wabunge hao kufuatia kutoridhishwa na mwenendo wa uongozi wa Dk Tulia anapokalia kiti cha Spika. 

Tangu Jumanne wiki hii, wabunge hao wamekuwa wakisusa vikao vinavyoongozwa na kiongozi huyo kwa madai anaminya demokrasia. 

Walifikia uamuzi huo baada ya Dk Tulia kuzuia kujadiliwa hoja ya kufukuzwa kwa wanafunzi zaidi ya 7,000 wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) iliyowasilishwa na Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari na kukatisha mjadala wa bajeti ya maji. 

Kitendo hicho kiliwafanya wabunge wote wa upinzani kupingana na maamuzi ya Dk Tulia, jambo lililosababisha watolewe bungeni. 

Kutokana na hali hiyo wabunge hao kupitia Mbunge wa Simanjiro, James Ole Millya akisindikizwa na Mbunge wa Kibamba, John Myika wa Chadema na Mbunge wa Konde wa CUF, Khatibu Said Haji waliwasilisha hoja hiyo kwa Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilillah baada ya Spika, Job Ndugai kutokuwapo bungeni. 

Hoja hiyo iliwasilishwa kwa mujibu wa Kanuni ya 138 (1) ambayo inaeleza utaratibu wa jinsi ya kumwondoa Naibu Spika. 

Kanuni hiyo inasema, “Utaratibu wa kumwondoa Naibu Spika madarakani chini ya Ibara ya 85(4)(c) ya Katiba utakuwa kama ule wa kumwondoa Spika, isipokuwa tu taarifa ya kusudio la kumwondoa Naibu Spika madarakani inayoeleza sababu kamili za kuleta hoja hiyo, itapelekwa kwa Spika ambaye ataiwasilisha kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa ajili ya kuijadili.” 

Fasili ya pili ya Kanuni hiyo inasema: “Endapo Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge itaridhika kuwa zipo tuhuma mahususi dhidi ya Naibu Spika zinazohusu uvunjaji wa Katiba, Sheria au Kanuni zinazoongoza Shughuli za Bunge, basi Kamati hiyo itaidhinisha kuwa hoja hiyo ipelekwe bungeni ili iamuliwe.” 

Kwa mujibu wa Ibara ya 85(4)(c), Naibu Spika atakoma kuwa Naibu Spika na ataacha kiti cha Naibu Spika endapo ataondolewa kwenye madaraka ya Naibu Spika kwa azimio la Bunge. 

Akizungumzia uwasilishwaji wa hoja hiyo, Millya alisema taarifa zaidi watatoa leo kuhusu msimamo wao huo. 

Dk Tulia aliwataka wabunge wenye malalamiko juu ya utaratibu wa uendeshaji wa shughuli za Bunge kukata rufaa kwa kufuata Kanuni za Bunge. 

Alisema kanuni ndogo ya 5(2) inasema Spika atawajibika kutilia nguvu kanuni zote za Bunge na 5(3) inasema Spika anaweza kumtaka mbunge yeyote anayekiuka kanuni hizi kujirekebisha mara moja. 

Alisema kwa hiyo mbunge yoyote asiyeridhika, kanuni za Bunge zinamruhusu kukata rufaa na zinamweleza nini cha kufanya.

No comments: