Viongozi wa upinzani, akiwemo Edward Lowassa wa Chadema, wametangaza hatua hiyo kwenye kikao na wanahabari Dar es Salaam.
Wamesema wameahirisha maandamano hayo kwa kipindi cha mwezi mmoja baada ya kusikia ombi la viongozi wa kidini na wadau wengine waliowaomba kukumbatia na kuyapa muda mazungumzo.

Viongozi wa chama hicho walikuwa wameitisha maandamano na mikutano ya kisiasa Septemba Mosi kupinga walichosema kuwa ni ukandamizaji unaoendelezwa na serikali.
Baada ya mkutano wa kikao cha Kamati Kuu ya chama Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) mwishoni mwa Julai, viongozi walisema: “Yapo Matukio ambayo yamekua yakifanywa na kukandamiza demokrasia na misingi ikipuuzwa na kudharauliwa.”
“Si nia ya Chadema kugombana na Serikali bali ni kazi ya Chama Pinzani kuisaidia Serikali iongoze kwa kufuata misingi ya Katiba,” chama hicho kilisema.
Maandamano hayo yalipewa jina Ukuta, ikisimamia Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania
Serikali ilipiga marufuku mikutano yote ya kisiasa, ya hadhara na ya ukumbini. Baadhi ya viongozi wa upinzani wamekamatwa na kuzuiliwa kwa muda