Tuesday, September 27, 2016

Naibu Waziri wa Afya Dk.Kigwangalla afanya ziara Hospitali za Wilaya ya Mlele na Mpanda Mkoani Katavi

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Dk. Hamisi Kigwangalla amefanya ziara ya kikazi katika Wilaya ya Mlele na kutembelea Hospitali ya Mlele ya Wilaya hiyo pamoja na Hospitali ya Mpanda iliyopo Wilaya ya Mpanda Mkoani Katavi huku akitoa maagizo mbalimbali ya kiutendaji.

Katika ziara yake katika Hospitali ya Mlele, Dk.Kigwangalla amewaagiza viongozi wa Serikali wa Wilaya na ule wa Hospitali hiyo kuhakikisha wanakamilisha mambo muhimu ikiwemo ujenzi wa chumba cha upasuaji, jengo la kuhifadhia mahiti  na vitu vingine huku akitaka ndani ya miezi mitatu view vimekamilika.


Akiwa katika Hospitali hiyo ya Mlele, Dk.Kigwangalla ameweza kutembelea sehemu mbalimbali za hospitali pamoja na kukagua ujenzi wa majengo ya Chumba cha upasuaji, chumba cha kuhifadhia maiti na majengo mengine ambapo amemtaka Mkuu wa Wilaya kuhakikisha wanafanya juhudi wanakamilisha kwa wakati majengo hayo ili wananchi wapate huduma bora.

Kwa upande wa ziara yake hiyo katika Wilaya ya Tanganyika yaliyopo makao makuu ya Mkoa wa Katavi, Dk. Kigwangalla ameweza kutembelea Hospitali ya Mpanda ambayo kwa sasa inahudumia kama Hospitali ya Mkoa ambapo napo ameagiza kufanyiwa marekebisho mbalimbali  ikiwemo kuzingatia masuala  usafi.

Aidha, ametoa maagizo kuhakikisha wanafunga mfumo wa malipo wa kisasa katika vyanzo vyote vya mapato ili kukusanya pesa nyingi zaidi zitakazoweza kuendesha huduma za Afya ndani ya Hospitali hiyo.

No comments: