Friday, November 4, 2016

Majibu ya Rais Magufuli Baada ya Kuulizwa kama Yeye Ni Dicteta


Rais John Magufuli ameyatolea majibu malalamiko yaliyokuwa yakitolewa na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani nchini kuwa amekuwa akikandamiza demokrasia tangu alipoingia madarakani.


Akijibu swali lililoulizwa na mmoja kati ya wahariri wa vyombo vya habari leo Ikulu jijini Dar es Salaam, aliyetaka ufafanuzi kuhusu malalamiko hayo, Rais Magufuli alisema kuwa hajawahi kukandamiza demokrasia nchini na kwamba anachofanya ni kuihuisha.

“Katika kazi yoyote, critic ni kitu cha kawaida na pongezi ni kitu cha kawaida. Lakini ukweli ni kwamba katika muda wote ambao nimechaguliwa kuwa Rais sija-suppress democracy (sijakandamiza demokrasia) na bahati nzuri ninapromote demokrasia,” alisema Rais Magufuli.

“Na ndio maana unaona Bunge linaendelea vizuri. Na ndio maana unaona uchaguzi unafanyika hata hapa Dar es Salaam kuna maeneo wamechagua Ukawa na kuna maeneo wamechagua CCM. Hiyo ni demokrasia. Mikutano yao ya ndani ya vyama mmekuwa mkishuhudia, na hivi juzijuzi kumekuwa na mkutano wa chama fulani, wakagombana wenyewe na wakafukuzana wenyewe,” aliongeza.

Aidha, akijibu swali la nyongeza lililoulizwa na mwanahabari mkongwe, Tido Mhando (Azam TV) kuhusu mtazamo wa baadhi ya watu kuwa huenda anaendesha mambo kidikteta bila kufuata taratibu zilizowekwa, Rais Magufuli alisema hiyo ni tafsiri ya mtu ambayo inatokana na uhuru wa kufikiria.

“Kila mmoja anaweza akatafsiri vyovyote… wewe(Tido) ulipokuwa BBC ukahama ukaenda TBC, ukahama leo uko Azam, mtu mwingine anaweza akatafsiri kuwa huenda huo ni udikteta wa namna fulani wa kuhamishwahamishwa. Kwa hiyo kila mmoja ana uhuru wa kufikiria anavyofikiria,” alisema.

Rais Magufuli leo amefanya mkutano na Wahariri wa vyombo vya habari kwa lengo la kujibu maswali yao

No comments: