Sunday, November 13, 2016

SABA WA MAJARIBIO WAPIMWA AZAM FC

KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, jioni ya leo imefungwa mabao 2-0 dhidi ya JKT Ruvu katika mchezo maalumu wa kirafiki wa kuwapima nyota wa timu hiyo, uliofanyika Uwanja wa Azam Complex.

Azam FC tayari imeanza mchakato wa kukiimarisha zaidi kikosi chake ili kufanya vizuri, kuelekea mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) na michuano ya Kimataifa.
Hivyo mchezo wa leo ulikuwa ni sehemu ya benchi la ufundi kuwatathimini wachezaji na wala si kuangalia matokeo ya uwanjani, baadhi ya wachezaji ni wale saba waliokuja kwenye majaribio wanaogombea nafasi za kusajiliwa kwenye usajili wa dirisha dogo, ambao wote wamepata nafasi ya kucheza.

Wachezaji hao ni mabeki wa kati Nkot Mandeng Eric (Coton Sport De Garoua, Cameroon), Kone Nabil Ibrahim (Asec Mimosa, Ivory Coast), kiungo mkabaji Kingue Mpondo Stephane (Coton Sport Garoua, Cameroon).
Washambuliaji ni Yaya Anaba Joel (Coton Sport Garoua, Cameroon), Samuel Afful (Sekondi Hasaacas, Ghana), Bernard Ofori (Medeama, Ghana) na Konan Oussou (Tala’ea El-Gaish SC, Misri).
JKT Ruvu imepata mabao yake, moja katika kila kipindi cha mchezo huo yakifungwa na washambuliaji Samwel Kamuntu dakika ya 18 na Abdulrahman Mussa, anayekipiga Ruvu Shooting, akitupia bao la pili dakika ya 54.

Mara baada ya mchezo huo, kikosi cha Azam FC kesho Jumapili kitapumzika kabla ya Jumatatu kucheza mchezo mwingine wa kirafiki dhidi ya Ruvu Shoooting utakaofanyika Uwanja wa Azam Complex saa 1.00 usiku.
Kikosi kilikuwa hivi leo:

Mwadini Ally, Ismail Gambo/Ofori dk 35, Gadiel Michael, Kone Nabil Ibrahim, Nkot Mandeng Eric, Kingue Mpondo Stephane, Ramadhan Singano/Jean Mugiraneza dk 59, Frank Domayo/Salum Abubakar dk 46, Konan Oussou/Yaya dk 46, Samuel Afful/Francisco Zekumbawira dk 59, Enock Atta Agyei/Gonazo Ya Thomas dk 59

No comments: