Sunday, April 30, 2017

Sakata la Wafanyakazi Hewa.ACT WAZALENDO watoa neno lao

Juzi tarehe 27 Aprili 2017, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora) Mh. Angela Kairuki alikabidhi rasmi Ripoti ya zoezi la Uhakiki wa Vyeti ambapo iliripotiwa kuwa jumla ya watumishi 9932 wanatumia vyeti feki.

Chama cha ACT Wazalendo kinaunga mkono uamuzi wa serikali kuwachukulia hatua watumishi wote wa umma waliobainika kutumia vyeti feki ikiwemo kuwafukuza kazi na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.

 Bila shaka hatua hii itapanda mbegu ya uwajibikaji, kuchochea uadilifu na kuhakikisha uweledi kwenye utumishi wa umma.

Mbali na kupongeza, yapo masuala kadhaa yaliyoibuka kwenye zoezi hilo ambayo tunadhani hayakwenda sawasawa na hivyo basi sisi kwa nafasi yetu tunao wajibu wa kuyakemea ili kuufanya mchakato huu uende kwa haki:

Mosi, kauli ya Mh. Rais kuwasamehe wale wataojiondosha kazini wenyewe na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria na wale wataoendelea kubaki kwenye nafasi zao ni kinyume cha sheria na katiba ya nchi.

 Kisheria Rais hana mamlaka ya kumsamehe mtu anayetuhumiwa kufanya kosa la jinai iwapo mtu huyo hajafikishwa kwenye vyombo vya sheria na kuhukumiwa.

Madaraka pekee aliyonayo . Rais ni kutoa Msamaha kwa wafungwa wanaotumikia kifungo (President's Prerogative of Mercy) kama alivyofanya hivi karibuni kwenye Sherehe za Muungano.

 Iwapo tutaacha hulka ya viongozi kuchukua hatua wapendavyo hata kama kwa kusigina sheria za nchi basi tujue wazi tunalipeleka taifa kwenye "Utawala wa Mtu Binafsi" badala ya "Utawala wa Sheria".

Pili, madai ya Waziri Kairuki kuwa mchakato wa uhakiki wa vyeti haujawagusa wanasiasa na wateule wa Mh. Rais kwa sababu cheti si sifa ya kupatikana kwao unapotosha mantiki ya zoezi zima na kuweka upendeleo wa dhahiri.

Ikumbukwe kuwa msingi wa zoezi hili ni kuhakikisha kuwa taifa linabaki na watumishi wenye sifa. Waziri Kairuki anasema kuwa sifa pekee ya Kikatiba ya Viongozi wa kisiasa ni kuwa wajue kusoma na kuandika. Jambo ambalo Waziri Kairuki hakutaka kujiuliza ni kuwa iwapo viongozi wa kisiasa watathibitika kughushi vyeti ambalo ni kosa la jinai haitawaondolea sifa yao ya uongozi.

 Kama Waziri mwenye dhamana ya utawala bora hakuona kuwa uhakiki wa vyeti kwa viongozi wa kisiasa na wateule wa . Rais kama vile Mawaziri, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kungehakikisha kuwa viongozi hao wanakwenda sambamba na viapo na matakwa ya kimaadili?

Uamuzi huu wa kutowagusa viongozi wa kisiasa katika zoezi hili la uhakiki wa vyeti ni ushahidi wa dhahiri kabisa wa jinsi serikali inavyohaha kuwalinda baadhi ya wateule wa Mh. Rais na wanasiasa ambao wametuhumiwa na umma kwa makosa ya kughushi vyeti.
ACT Wazalendo tunatoa rai kwa serikali kutanua mawanda ya zoezi hili liguse  viongozi wa kisiasa wa CCM na vyama vya upinzani.

Ado Shaibu,

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mawasiliano.
30 Aprili 2017

No comments: