Friday, April 7, 2017

TIZAMA KWA UREFU JINSI NCHI NZIMA LEO ILIVYOUNGANA KUMSAKA ROMA NA MONI

JESHI LA POLISI DAR LAFUNGUKA KUHUSU KUPOTEA KWA MSANII ROMA MKATOLIKI

Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam, Simon Sirro amesema kuwa tayari wameshapata taarifa za kupotea kwa Msanii wa Bongo Fleva hapa nchini, ‘Ibrahim Mussa’ maarufu kwa jina la Roma Mkatoliki na kuongeza kuwa tayari timu yake ya upelelezi imeshaanza kazi.


Ameyasema hayo mapema hii leo wakati akizungumza na Katibu wa Chama cha Wanamziki wa Kizazi Kipya Tanzania, Samweli Mbwana alipotaka kujua kama Jeshi la Polisi lina taarifa ya kupotea kwa mwanamziki huyo.

Sirro amesema kuwa taarifa za kupotea kwa msanii huyo tayari wameshazipata na Jalada la upelelezi tayari limeshafunguliwa kwa ajili ya upelelezi.

Ameongeza kuwa timu yake ya upelelezi iko mtaani kwa ajili ya kujua kinachoendelea, na amewaomba wasanii na baadhi ya watu kutokuwa wepesi wa kusambaza uvumi usiokuwa na ukweli ndani yake.

“Jamani mambo ya uvumi yaacheni, sio kitu kizuri unamvumishia mtu kitu ambacho hakijui na wengine wanasema kuwa Serikali inahusika kitu ambacho si cha kweli”,amesema Kamanda Sirro.

Aidha, Sirro amesema kuwa amepanga kukutana Waandishi wa Habari kesho saa tano Ofisini kwake ili kuweza kutoa ripoti kamili kuhusu kupotea kwa msanii huyo wa Bongo fleva kwani timu ya upelelezi tayari iko kazini.


Hata hivyo, amewatoa hofu wasanii na wananchi kwa ujumla kwamba suala hilo linafanyiwa kazi, hivyo hakuna haja ya kuogopa na kuendelea kuvumisha vitu visivyokuwa vya msingi.
NAPE NAYE AKALONGA---

Ikiwa leo ni siku ya pili tangu ilipotolewa taarifa kuwa msanii Roma Mkatoliki alitekwa na watu wasiojulikana akiwa pamoja na Moni Centrozone, mtayarishaji wa muziki wa Tongwe Records, Bin Laden katika studio za Tongwe Records, Waziri wa zamani wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amemlilia msanii huyo.

Nape emetoa kilio chake kupitia ukurasa wake wa Twitter, akitumia maneno matatu pekee yanayosomeka kwa hisia za ndani kuwa ni mtu anayemlilia mpendwa wake.

“Roma! Oooooh No!” ametweet Nape.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa jana na uongozi wa Tongwe Records, watekaji walifika katika studio hizo na kuwahoji waliokuwepo, kisha kuondoka nao wote pamoja na baadhi ya vifaa vinavyotumika kurekodia muziki, kwenda kusikojulikana.

Mke wa Roma, Nancy ameeleza kuwa alifika katika vituo kadhaa vya polisi jijini Dar es Salaam kuulizia taarifa za mumewe, lakini alielezwa kuwa taarifa za Roma hazikuwepo.

Akizungumza kwa uchungu kwenye vyombo mbalimbali vya habari, Nancy aliwaomba Watanzania kwa ujumla pamoja na vyombo vya usalama kusaidia kufahamu alipo mumewe.

Leo mchana, wasanii wamekutana katika studio za Tongwe Records kwa lengo la kuzungumzia suala hilo zito ambalo limevunja mioyo ya wadau wa muziki, familia na ndugu wa Roma na wenzake.

MBUNGE BASHE ALIA KUTEKWA KWA MSANII ROMA MKATOLIKI


Jana usiku taarifa za kukamatwa kwa msanii wa hip hop Roma Mkatolikia zilianza kuenea katika mitandao ya kijamii kwa kuripotiwa kuwa Roma Mkatoliki na Moni wakiwa studio za Tongwe Records walikuja kukamatwa na watu wasiojulikana na kuwapeleka kusikojulikana.


Watu mbalimbali ikiwemo wasanii mbalimbali wamekuwa wakionesha hisia zao juu ya tukio hilo kwa kutumia kurasa zao za mitandao ya kijamii kuoneshwa kuguswa na tukio hilo, mbunge wa Nzega Hussein Bashe ni miongoni mwa watu waliyotumia kuraza zao za instagram kuandika anachowaza kuhusu Roma.

"Who is behind all this? Ni genge ambalo limejipa mamlaka ya kupandikiza woga na chuki miongoni mwa jamii na kuharibu Taswira ya CCM. Tunawajibu wa kukataa woga ,Tunawajibu wa kutoruhusu Misuse ya vyombo vya Ulinzi na usalama, Tunawajibu wa kulinda Taifa letu

“Tunawajibu wa kupigania Values zilizopiganiwa na waasisi wa Taifa letu kama Mzee Karume na Mwl Nyerere, Tunawajibu wa kukataa ukandamizaji tukikaa kimya kwa kufikiri kuwa hayanihusu mimi yanamhusu yule yatakapokufika wewe hatakuepo mtu wa kukutetea na halitakuepo Taifa la Tanzania

“Sote tusimame tuseme hapana kwa mfumo huu unaoanza kuota mizizi kama mtu Ana makosa ufuatwe utaratibu wa kisheria kumkamata na sio utekaji tunakabiliwa na vita kubwa ya kupambana na Umasikini na kujenga Taifa huru la kiuchumi . 

"Umasikini ni hatari kwa usalama wa taifa sio nyimbo

#FreeRoma"
WASANII WAKAJITOKEZA
Wasanii wa muziki wa Bongo Fleva nchini kwa pamoja wameungana na kuviomba vyombo vya usalama nchini kufanya juhudi za kumtafuta msanii mwenzao Roma Mkatoliki na wenzake wanaodaiwa kutekwa na kupelekwa kusikojulina.

Wasanii hao, leo wamekutana COCO Beach na kulaani kitendo cha Roma kutekwa, huku wakiitaka serikali iwasaidie kumtafuta na kumpata akiwa salama.

==> Hii ni video ya mazungumzo yao na vyombo vya habari leo

No comments: