Friday, May 12, 2017

ACT WAZALENDO WATANGAZA MRITHI WA KITILA MKUMBO

Chama Cha ACT- Wazalendo leo kimemtangaza rasmi Mwanasheria Albert Msando kuwa mrithi wa nafasi ya Mshauri Mkuu wa Chama hicho iliyoachwa wazi na Prof Kitila Mkumbo aliyeteuliwa na Rais Magufuli kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji.

Akiongea na waandishi wa habari Kaimu Katibu Mkuu wa chama hicho Dorothy Semu, amesema Kamati Kuu ya Chama hicho ilikutana tarehe 7 Mei na kufanya mabadiliko ya kiuongozi ndani ya chama.

"Kama mnavyofahamu, mnamo tarehe 07 Mei, 2017 Kamati Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo ilikutana katika mkoa wa kichama Kahama na kufanya kikao chake cha kawaida. Katika kikao hicho, pamoja na mambo mengine yaliyojadiliwa na kufikiwa maamuzi, Kamati Kuu ilifanya mabadiliko kadhaa ya safu ya Uongozi wa juu Makao Makuu ikiwemo kuthibitisha uteuzi wa Mshauri wa Chama wa masuala ya kisheria. Lengo kuu la mabadiliko yaliyofanywa na Kamati Kuu ni kuleta ufanisi wa utekelezaji wa kazi na majukumu ya Kamati za kisekta Makao Makuu ya Chama na mikoani" alisema Dorothy Semu

Mbali na hilo Dorothy Semu anasema kwa kauli moja Kamati kuu ilikubaliana na mapendekezo ya kiongozi wa chama.

"Kwa dhamana aliyonayo kikatiba kwa mujibu wa ibara ya 29(25)(vii), Kiongozi wa Chama aliona umuhimu wa Chama kuwa na Mshauri wa Masuala ya Sheria na akapendekeza jina la ndugu Albert Msando kuwa Mshauri wa Chama juu ya mambo ya Sheria na kuliwasilisha mbele ya Kamati Kuu. Kamati Kuu kwa kauli moja ilikubaliana na mapendekezo hayo na ikapitisha uteuzi huo kwa mujibu wa Katiba ibara ya 29(13)(ii). Uteuzi wa Ndugu Msando umeanza rasmi tarehe 08 Mei 2017" alisisitiza Dorothy Semu

No comments: