Tuesday, July 18, 2017

Benki ya KCB Tanzania yaendelea kuwapatia ushauri wa kibiashara wanachama wa KCB 2jiajiri


Afisa Sheria Bi. Doris Mugarula (wakwaza kushoto) na Afisa Fedha Bi. Happiness Kisanga (wapili kushoto) wa Benki ya KCB wakimsikiliza mjasiriamali Bi. Batula akielezea maendeleo ya biashara yake ya nguo mkoani Arusha. 
Afisa Masoko wa Benki ya KCB Bi. Ghati Muhere (kulia) akimpatia ushauri wa kibiashara mjasiriamali Bi Hafsa Ali (kushoto) katika duka lake la nguo za kiume, H&D Collection Shop, Kariakoo, jijini Dar es Salaam.
Afisa Sheria, Bi. Doris Mugarula (wakwanza kulia) na Afisa Fedha Bi. Happiness Kisanga (wapili kulia) wa Benki ya KCB wakimpatia ushauri wa kibiashara mjasiriamali Bi Shamsa Ally (kushoto) katika duka lake la vifaa vya magari makubwa mkoani Morogoro.
Afisa Fedha wa Benki ya KCB Bi. Happiness Kisanga (wakwanza kulia) akimpatia ushauri wa kibiashara mjasiriamali Bi Hawa Mabrouk (katikati) katika ofisi yake ya Video production, Ilala, jijini Dar es Salaam.
Afisa Masoko, wa Benki ya KCB, Bi. Ghati Muhere (kulia), akimpatia ushauri wa kibiashara mjasiriamali Bi Jac Bazaar (kushoto) katika duka lake la vifaa vya umeme mkoani Morogoro

Afisa Masoko Bi. Ghati Muhere (aliyechuchumaa) na Afisa Fedha Bi. Happiness Kisanga (aliyesimama) wa Benki ya KCB wakimpatia ushauri wa kibiashara mjasiriamali Bi Violeth (aliyeinama) katika biashara yake ya kilimo mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro.
Afisa Masoko wa Benki ya KCB Bi. Ghati Muhere (kushoto) akimpatia ushauri wa kibiashara mjasiriamali Bi Selina (kulia) katika duka lake la bidhaa za watoto Jijini Mwanza.
Afisa Sheria wa Benki ya KCB Bi. Doris Mugarula (kushoto) akimsikiliza mjasiriamali Bi Fatma (katikati) akielezea kuhusu biashara yake ya vipodozi na mikoba ya kike Jijini Mwanza.

KCB 2jiajiri ni programu inayolenga kumkomboa mwanamke mjasiriamali kutoka katika matatizo yanayosababisha biashara yake ishindwe kukua na kuwa endelevu. Matatizo yanayolengwa kutatuliwa kutoka kwa wanawake wajasiriamali hawa ni elimu ya kifedha, kufikiwa na huduma za kifedha, ukosefu wa dhamana, kutokujua vizuri masuala ya kisheria, uelewa finyu wa sera za serikali na kiuchumi, njia hafifu za kuendesha biashara endelevu, ukosefu wa mtaji, utaalamu wa kuanzisha biashara kubwa n.k.Benki ya KCB Tanzania inaendelea kuwapatia wanawake wajasiriamali waliopitia mafunzo ya ujasiriamali ya KCB 2jiajiri ushauri wa kibiashara kwa vitendo ofisini kwa wafaidika wa 2jiajiri. Maafisa watatu ambao ni; afisa fedha, sheria na masoko wanawatembelea wafaidika hao wajasiriamali waliomaliza mafunzo ya KCB 2jiajiri katika mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Moshi, Morogoro na Zanzibar.


“Programu hii ilizinduliwa rasmi Desemba, 2016, ambapo hadi sasa tumewapa stadi za biashara endelevu wanawake wajasiriamlai 258 kutoka mikoa 6 ya Tanzania.” Alisema Christine Manyenye, Mkuu wa Masoko na Mahusiano wa benki ya KCB.


Akielezea kuhusiana na programu ya KCB 2jiajiri Bi. Manyenye alieleza kuwa, wafaidika wa KCB 2jiajiri baada ya kumaliza mafunzo ya siku tatu darasani, kwa sasa wananufaika kwa kupata ushauri wa kibiashara na kitaalamu kutoka kwa washauri watatu katika nyanja za Kifedha Kisheria na Masoko.

aliishukuru Benki ya KCB kwa kutoa mafunzo ya kibiashara ambayo yamepanua ufahamu wa jinsi yakuendesha biashara. “kupitia KCB 2jiajiri nimeweza kujua umuhimu wa kurasimisha biashara, kuwa na leseni ya biashara, kuweka kumbukumbu katika biashara na jinsi ya kuendesha biashara kiujumla” alisema Bi. Kipangula.

Benki ya KCB kimsingi inatambua mchango mkubwa wa wanawake wanaoutoa katika sekta binafsi hususani katika Ujasiriamali mdogo na wa kati (SMEs) hivyo lengo kwa ujumla ni kuwezesha wafanyabiashara wanawake wa Kitanzania kuandaa mikakati ambayo inaboresha stadi zao na uwezo hivyo kuunda fursa nyingi za kibiashara kwa ajili yao.

Bi. Manyenye alimaliza kwa kusema kuwa programu ya KCB 2jiajiri ni endelevu na kwa wanawake wajasiriamali ambao bado hawajajiunga na KCB 2jiajiri wajiulize kwa nini wahangaike wakati KCB 2jiajiri ipo kwa ajili yao.

Kuhusu Benki ya KCB

Benki ya KCB ni benki kubwa zaidi katika Afrika Mashariki na Kati iliyoanzishwa mwaka 1896 kisiwani Zanzibar. Toka hapo benki imekua na kuenea katika nchi za Tanzania, Kenya Sudani ya Kusini, Uganda, Rwanda, Burundi na Ethiopia. Leo hii ina mtandao mkubwa zaidi katika kanda hii ikiwa na matawi zaidi ya 250, mashine za kutolea fedha (ATM) 962, na wakala 13,562.
KCB Bank Group pia inamiliki kampuni ya bima ya KCB, KCB Capital na KCB Foundation.
Nchini Tanzania, KCB ilifungua milango yake mwaka 1997 na toka hapo imekuwa mdau mkubwa katika kukuza sekta ya fedha nchini. Kwa sasa benki ina matawi 14 Tanzania bara na visiwani Zanzibar. Matawi hayo ni Samora, Mlimani, Uhuru, Msimbazi, Lumumba ,Buguruni, Oysterbay, Pugu jijini Dar es Salaam; Moshi, Zanzibar, Arusha Main na TFA, Mwanza na Morogoro

No comments: