Friday, July 21, 2017

RAIS MAGUFULI - ASIYEFANYAKAZI NA ASILE, NA ASIYE KULA NA AFE

Rais John Magufuli amesema serikali yake imedhamiria kumaliza tatizo la usafiri wa barabara nchini. Aidha amesema serikali yake haitatoa chakula cha msaada kwa wananchi wazembe ambao hawajitumi kufanya kazi.

Hayo aliyasema wilayani Kakonko wakati wa ziara ya uzinduzi wa ujenzi barabara ya urefu wa kilomita 50 kutoka Nyakanazi hadi Kibondo mkoani Kigoma ambayo itajengwa kwa lami.
Vilevile alisema mara zabuni ikitangazwa, serikali tayari ina fedha za kujenga barabara ya Kasulu-Kibondo kwa kiwango hichohicho.

Alitoa onyo pia kwa makandarasi wazembe akiwataka wafanye kazi kufuatana na mikataba na kwa utaalam unaotakiwa na kwamba serikali iko tayari kuwatimizia mahitaji katika majukumu yao. “Nakuomba waziri, kama kuna pesa mkandarasi anadai, mhakikishe wiki ijayo analipwa na hii lami ianze kujengwa usiku na mchana,” alisisitiza rais.

Akigusia suala la ujambazi sehemu hiyo, Magufuli alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Kigoma alishughulikie kwa nguvu zote ili kulikomesha kwa vile, miongoni mwa ukatili unaofanywa na majambazi ni pamoja na kuwatoboa macho wananchi ili kuwazuia wasitoe ushahidi waliouona.

Kuhusu kodi, alisema serikali imefuta kodi 80 kwenye mazao, kodi saba kwenye mifugo na kodi nyingine kwenye uvuvi. Katika suala la chakula alisisitiza kila mtu afanye kazi kwa ajili ya uzalishaji wa chakula chake na nchini kwa jumla.

“Sileti chakula ng’o, asiyefanya kazi na asile, asiiyekula na afe. Mfanye kazi kweli, na huo ndiyo ukweli,” alisisitiza. Akizungumzia uwekezaji katika madini kutoka nje na ndani, Rais Magufuli alisema serikali yake imewaita wawekezaji kutoka nje na iwapo hawatajitokeza mapema migodi yote bora watapewa Watanzania waiendeshe

No comments: