Friday, August 4, 2017

KUKOSEKANA USAFIRI KWA MAOFISA UGANI KUNAWAFANYA WASHINDWE KUWAFIKIA WAKULIMA KWA WAKATI

Mtafiti kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Mikocheni jijini Dar es Salaam (MARI), Christina Kidulile (kushoto), akimuelekeza jambo mkulima, Ablali Mohamed kuhusu matumizi ya mbegu bora, alipotembelea banda la COSTECH , lililopo chini ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika Maonyesho ya Kitaifa ya Wakulima Nanenane yanayoendelea Viwanja vya vya Ngongo mkoani Lindi leo. Katikati Mtafiti, Ismail Ngolinda kutoka  Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ilonga Kilosa mkoani Morogoro na Bestina Daniel kutoka COSTECH.


Mtafiti kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Mikocheni jijini Dar es Salaam (MARI), Christina Kidulile, akimkabidhi moja ya kipeperushi mkulima Bendera kutoka wilayani Ruangwa baada ya kutembelea banda la COSTECH.
Mtafiti kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH),  Bestina Daniel (kushoto), akimwelekeza jambo Ofisa Ugani, Mligo Eisen (kulia), alipotembelea banda la COSTECH katika maonyesho hayo, alipotembelea banda la COSTECH , lililopo chini ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika Maonyesho ya Kitaifa ya Wakulima Nanenane yanayoendelea Viwanja vya vya Ngongo mkoani Lindi leo. Kushoto ni Mtafiti kutoka Kituo cha Utafiti cha Mikocheni, MARI, Christina Kidulile.
Mtafiti kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ilonga Kilosa mkoani Morogoro, Ismail Ngolinda (katikati) akitoa maelezo maelezo kwa Ofisa Ugani kutoka Halmshauri ya Manispaa ya Lindi, Mligo Eisen kuhusu matumizi sahihi ya mbegu bora. Kulia ni Mtafiti kutoka COSTECH, Bestina Daniel na Mtafiti kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Mikocheni jijini Dar es Salaam (MARI), Christina Kidulile.
Ofisa Ugani, Kumi Rashid Kumi akipata maelekezo kataika banda la COSTECH kuhusu kilimo bora.

Na Dotto Mwaibale, Lindi

KUKOSEKANA kwa usafiri kwa maofisa ugani kunachangia kwa kiasi kikubwa kushindwa kuwafikia wakulima kwa wakati.

Hayo yamebainishwa na Ofisa ugani wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi, Mligo Eisen  wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini leo alipotembelea banda la Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kwenye maonyesho ya kitaifa ya wakulima maarufu Nanenane yanayoendelea viwanja vya Ngongo mkoani hapa.

"Maofisa ugani tunashindwa kuwafikia wakulima katika maeneo mbalimbali kwa sababu ya kukosa usafiri na hii ni changamoto kubwa kwetu" alisema Eisen.

Eisen alisema katika idara ya mifugo kuna pikipiki tatu na idara yote ya kilimo kuna gari moja ambalo tangu lipatikane halina zaidi ya miezi sita na vifaa hivyo vya moto ndivyo vinavyotegemewa na maofisa ugani na maofisa mifugo ili kuwafikia wakulima hali ambayo ni changamoto kubwa.

Aliongeza kuwa changamoto nyingine ni uhaba wa maofisa ugani jambo linalochangia wakulima kupata elimu ya kilimo kwani ofisa ugani mmoja anatakiwa kutembelea vijiji vitatu na kukutana na wakulima wa aina tofauti ambao wanalima mazao tofauti.

Alisema hali hiyo inamfanya ofisa ugani husika kushindwa kuwafikia wakulima wake wote hivyo kuwa chanzo cha wao kukosa elimu ya kilimo na kupata chakula kidogo na mazao ya biashara.

Mkulima Ablali Mohamed alisema changmoto kubwa waliyonayo ni kukosekana kwa mbegu bora na kuwa ni muhimu kwa vituo vya utafiti wa kilimo kuzalisha kwa wingi mbegu hizo ili wakulima waweze kuzitumia na kuachana na mbegu za zamani.

Mkulima Bendera kutoka Wilaya ya Ruanga alisema ni ili kufanikisha kilimo chenye tija ni muhimu kukawa na mawasiliano ya karibu kati ya watafiti, wakulima na maofisa ugani kwani bila ya mawasiliano hakuna kitakachoweza kufanyika.

COSTECH inafanya maonyesho hayo kupitia Wizara ya Kilimo,Mifugo na Uvuvi.

No comments: