Thursday, September 14, 2017

ZIJUE GHARAMA ZA MATIBABU YA LISSU KWA SIKU MOJA,CHADEMA WAOMBA MSAADA MATAIFA YA NJE

Chadema imetangaza kuanzisha kampeni maalumu kuchangisha fedha kwa ajili ya kumgharimia mbunge wake, Tundu Lissu anayeendelea kupata matibabu mjini Nairobi huku matibabu yake yakigharimu Sh 10 milioni kwa siku.

Kutokana na ukubwa wa gharama hizo chama hicho tayari kimeziomba jumuiya za kimataifa ikiwamo Ujerumani na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya(EU) kuangalia kama inaweza kusaidia matibabu ya mwanasiasa huyo.

Makamu Mwenyekiti wa Chadema, Profesa Abdalah Safari amesema leo Ijumaa kuwa pamoja na gharama za kumtibu Lissu kuwa kubwa lakini chama kitaendelea kumpigania ili kuokoa maisha yake.

“Unajua chama tumepoteza watu wengi sana, kama vile Ben Saanani, Dk Slaa ( Willbroad) lakini tuna mahaba makubwa na ndugu yetu Lissu hivyo tunaendelea kupigania maisha yake. Gharama  anazotumiwa kutibiwa ni kubwa mno maana kwa siku inagharimu kiasi cha Sh10 milioni sasa sisi peke yetu hatuwezi ndiyo maana tumeamua kuomba msaada toka kwa rafiki zetu,” amesema.

Amesema chama kimeunda kamati maalumu ambayo inaratibu michango ya Lissu na moja ya eneo ambalo wamewasilisha maombi yao ni kwa Serikali ya Ujerumani na Umoja wa Ulaya.

“Siwezi kusema hadi sasa nini tumejibiwa ila ninachojua kamati inaendelea kufuatilia... unajua wale Wajerumani ni ndugu zetu maana chama cha CDU ni marafiki zetu na tumewaandikia,” amesema.

Chama cha Christian Democratic Party (CDU) kinachoongozwa na Angela Merkel kwa sasa kipo kwenye kampeni za kumchangua Kansela katika uchaguzi utakaofanyika baadaye mwaka huu. Vyama hivi, Chadema na CDU vimekuwa na uhusiano wa kisiasa kwa muda mrefu na mara kwa mara viongozi wake wamekuwa wakitembeleana.

“Chadema inaamini kuwa kutokana na kufikwa na tatizo hilo huenda kikapata msaada kutoka miongoni mwa vyama rafiki.” Pia, alidokeza kuwepo uwezekano wa kuiandikia Uingereza katika juhudi zake za kuomba usaidizi.

Profesa Safari amesema chama kimejaribu kukusanya michango kutoka kwa kanda zake pamoja na wananchi wengi lakini kadri siku zinavyoenda gharama zimekuwa zikiongezeka hivyo wameamua kupiga hodi pia katika jumuiya za kimataifa.

“Wananchi wetu ni maskini na Serikali hadi sasa haijataka kuchangia gharama zozote hivyo lazima tuendelee kutafuta njia nyingine za kumwokoa ndugu yetu,”amesema.

No comments: