Thursday, November 16, 2017

WANAHARAKATI WA GDSS KUPEWA ELIMU YA NAMNA YA KUSHIRIKI NA KAWEKA VIPAUMBELE KATIKA BAJETI KUU YA TAIFA

Wakazi wa jiji la Dar es salaam wametakiwa kuhudhuria na kushiriki kikamilifu katika mikutano inayoitishwa na serikali zao za mitaa hasa katika kipindi hiki cha kuahinisha vipaumbele katika bajeti kuu ya taifa.
Hayo yamesemwa mapema jana jijini Dar es salaam na muwezeshaji ambae pia Mchumi kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Ilala Bi. Lucy Kayombo alipokuwa akiwasilisha mada katika semina ya jinsia na maendeleo iliyofanyika makao makuu ya mtandao wa jinsia Tanzania(TGNP).

Bi. Lucy alisema kuwa ni vema kwa wananchi kujitolea kushiriki kwa wingi kwani ni haki yao ya msingi na mfumo wa sasa siyo kama wa zamani ambapo kila kitu kilikuwa kinaamuliwa na serikali kuu na huku chini zinakadiliwa fedha kwa ajili ya utekelezaji tu.
Lakini kwa sasa mfumo huo umekuwa shirikishi kwa kuwapa wananchi fursa ya kupanga vipaumbele vyao kuanzia ngazi ya mtaa, kata, halmashauri mpaka serikali kuu na kuhoji kwa viongozi wao pale wanapoona vipaumbele vyao vinapuuziwa au hawapewi nafasi ya kushiriki katika mipango ya kuunda bajeti.

Aidha mchumi huyo aliwataka washiriki wa semina hiyo kwenda kuuliza katika ofisi za mitaa yao kuwa wataanza lini zoezi hilo kwani muda ndio huu kuanzia mwezi novemba mpaka februari zoezi hilo linatakiwa kuwa katika ngazi ya mitaa na baada ya muda huo linaama na kwenda ngazi ya kata hivyo wanatakiwa kuhoji lini litaanza.
Na mpaka kufikia mwezi marchi zoezi hilo linahama kutoka serikali za mitaa na kwenda Kata na kufikia april linaondoka kutoka kata na kwenda katika ngazi ya Halmashauri ambapo wananchi muda wao unakuwa umekwisha wanachosubiri ni kuona vipaumbele gani vilivyopitishwa na kusubiri waone bajeti ya mwaka husika imetenga kiasi gani katika kutatua matatizo yao.

Muwezeshaji huyo aliendelea kusema kuwa tatizo kubwa na hasa kwa maeneo ya mijini ni kwamba kila mtu anajikuta ana mambo mengi hali inayosababisha kutohuhuria na walio wengi ukiwauliza mchakato umeanza hawajui au kwa mwaka uliopita mliweka vipaumbele gani anakosa jibu kutokana kwamba hana muda wa kushiriki katika zoezi muhimu kama hilo.
Lakini pia washiriki wa semina hiyo wamedai kuwa swala la uwajibikaji kwa viongozi wao limekuwa ni dogo kwani hawaitishi mikutano kama hii kwa kuwa wanajua watu wa mijini hawana utamaduni wa kuhoji, lakini pia hata wakiitisha hawatoi taarifa vizuri watu wote wakajua na kwamba wakiitisha vikao basi unakuta ni mchango wa taka taka au ulinzi shirikishi.

Na jambo lingine lililoonekana kuwa tatizo kubwa ni kuhama hama, kwani unakuta mtu kwa mwaka amehama kata mbili au zaidi  hali inayofanya ashindwe kwenda kuhoji katika mtaa aliotoka na kuwa vipaumbele vyao vimefanyiwa kazi au wasubiri katika awamu ijayo ya fedha.


No comments: