Wednesday, July 20, 2022

Chuo kikuu cha Arusha chawashauri vijana kusoma kozi zitakazowawezesha kujiajiri.

Chuo Kikuu cha Arusha kinachomilikiwa na kanisa la Waadventista (Wasabato)kimewashauri wanafunzi wote wanaotarajia kujiunga na Elimu ya  juu kusoma huku wakitambua changamoto ya ukosefu wa ajira siyo ya Tanzania pekee bali ya dunia nzima hivyo wanapswa kupata maarifa ya kujiajiri kupitia fursa za masomo wanazozipata.

Mwenyekiti wa jimbo Kuu la Kusini mwa Tanzania Askofu Mark Malekana ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Arusha akizungumza na wanahabari kwenye banda la chuo hicho katika maonesho ya 17 ya Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU).
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Chuo hicho ambaye pia ni Mwenyekiti wa jimbo Kuu la Kusini mwa Tanzania Askofu Mark Malekana wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye  Maonesho ya 17 ya Elimu ya Juu,Sayansi na Teknolojia yaliyoandaliwa Wizara ya Elimu Sayansi na teknolojia kupitia tume ya vyuo vikuu Tanzania (TCU) yanayoendelea kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es  salaam. 

"Chuo chetu kina  falsafa yakipekee katika utoaji wa Elimu, tunamtayarisha Mwanafunzi  kiroho,kisaikolojia,kiuchumi na katika nyanja zote za maisha  kwa kufanya hivyo tunategemea mhitimu hata akikosa ajira atajiajiri mwenyewe bila kutegemea kuajiriwa"amesema Askofu Malekana.

Aidha amesema kwamba kupitia maonesho hayo wameamua kuzungumzia kwa kina na wazazi au walezi wanaofika kwenye Banda la chuo hicho kwenye viwanja vya Mnazi ili kuwashauri waweze kujiunga na masomo chuoni hapo wapate maarifa mazuri yatakayoweza kuwasaidia kujiajiri.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko wa Chuo Kikuu cha Arusha Elisha Lomay ( wa kwanza kulia) akiwa na maafisa udahili wa chuo hicho katika Banda la Maonesho la chuo hicho .
Awali Mkuu wa Kitengo Cha Masoko wa Chuo hicho  Elisha Lomay  amewambia waandishi wa habari kwamba chuo hicho kinatumia falsafa ya kumjenga mwamanafunzi akue katika maadili ya kiroho ,Kimwili, pamoja na kitaaluma ambapo wahitimu wengi wamekuwa wakifanikiwa kufanya kazi Kwa weledi mkubwa.

Amendelea kufafanua kuwa  chuo hicho ambacho kipo Wilayani Meru Mkoani Arusha kimekua kikidahili wanafunzi bure kupitia njia ya mtandao,nakwamba baada ya wanafunzi kujiunga na chuo hicho wanalipia ada ambazo Wanaweza kuzimudu ambapo zinalipwa kwa awamu.

" Chuo chetu kinatoa ufadhili( Scholarship ) Kwa wanafunzi wanaotaka kusoma nje ya nchi kwa kushirikiana na wasabato wenzetu wanaoishi nje ya nchi ikiwemo Marekani,hivyo tunawakaribisha wazazi na walezi kuwaleta watoto wao kujiunga na chuo chetu kwani kina mazingira rafiki yakujisomea na gharama za ada na malazi ni nafuu" amesema Lomay.

Aidha amesema kwamba program wanazofundisha chuoni hapo ni pamoja na  Shahada za kidini,Utawala wa Biashara na Uhasibu,Sanaa ,Ualimu  pamoja na ngazi ya cheti na Astashahada ya Elimu ya Dini(Diploma) katika nyanja mbalbali.

No comments: