Tuesday, June 25, 2013

NGASA NI MCHEZAJI WA SIMBA----TFF



Siku chache baada ya mchezaji Mrisho Khalfan Ngasa kusajiliwa na klabu ya Yanga akitokea klabu ya Simba ambako alikuwa anacheza kwa mkopo toka klabu ya Azam fc shirikisho la soka Tanzania limeubatilisha mkataba uliopo baina ya Ngassa na Yanga ikisema kuwa haujasajiliwa kwenye ofisi zake . 

             

           Shirikisho limezungumza hayo mwishoni mwa wiki hii kupitia kwa msemaji wake ambaye ni Afisa habari wa TFF Boniface Wambura ambaye alisema kuwa TFF inautambua mkataba uliopo baina ya Simba na Ngassa na si wa Ngassa na Yanga kwa kuwa haujasajiliwa na uliosajiliwa TFF ni mkataba wa Simba unaoonyesha kuwa Ngassa ataitumikia Simba msimu ujao kwa muda wa mwaka mmoja . 

             Ngassa amekuwa akizua gumzo kwenye masuala ya usajili tangu aliposajiliwa toka Yanga kwenda klabu ya Azam na baada ya hapo akahamia Simba kwa mkopo kabla ya kurudi Yanga . 

    Viongozi wa Simba awali walisikika wakisema kuwa Ngassa ni mchezaji wao halali na sheria za usajili za TFF zitachukua mkondo wake jambo ambalo linaonekana kudhihirika . Kanuni za TFF kuhusiana na masuala ya usajili wa wachezaji zinasema kuwa lazima mkataba wa mchezaji husika usajiliwe kwenye ofisi za TFF . 

            Ofisa habari wa TFF Boniface Wambura alisema kuwa mkataba wa Ngassa na Yanga haujafika TFF na ndio maana hata kwenye timu ya Taifa , Taifa Stars ameorodheshwa kama mchezaji wa Simba. Bado viongozi wa Yanga na Simba pamoja na mhusika mkuu kwenye sakata hili Mchezaji mwenyewe hawajatoa tamko lolote juu ya taarifa hii ya Tff kutotambua mkataba wa Ngassa na Yanga.

No comments: