Wednesday, October 15, 2014

HUU NDIO UKWELI KUHUSU UTEKAJI WA WATOTO DAR ES SALAAM,KAMISHNA KOVA ATOA TAHADHARI NZITO

Kamishna wa polisi kanda maalum ya Dar es salaam SULEMAN KOVA akizungumza na wanahabari jijini Dar es salaam mapema leo
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linakanusha vikali juu ya uvumi unaoendelea jijini Dar es Salaam kuhusu utekaji nyara wa watoto wadogo wanaosoma shule. Hivi karibuni umezuka uvumi kutoka kwa watu mbalimbali hasa wazazi ambao uvumi huu umewafikia kwamba kuna kundi la wahalifu wanaotumia gari aina ya NOAH rangi nyeusi ambao kazi yao ni kuteka nyara wanafunzi kwa nia ya kutenda uhalifu ikiwa ni pamoja na kuwachuna ngozi na madhara mengine.

 Mpaka sasa Jeshi la Polisi halina taarifa yoyote ya mtoto kutekwa au kufanyiwa madhara yoyote kwa mtindo wa utekaji nyara. Pia Jeshi la Polisi limegundua kwamba huu ni uvumi ambao haujulikani chanzo chake hivyo wananchi wanaombwa kuachana na uvumi huo na kuupuuza kwani unaleta hofu katika jamii bila sababu za msingi.

    Aidha, uvumi huu umeanza kuleta usumbufu ambapo mnamo tarehe 03/10/2014 saa tatu asubuhi huko vingunguti mtu mmoja aitwaye PROSPER MAKAME miaka 34, mfanyakazi wa The Guardian Ltd, mkazi wa Tabata akiwa na mkewe MARYSTELLA MUNIS, Miaka 30, mfanyabiashara wa vyombo vya nyumbani walifika maeneo ya shule ya msingi Kombo iliyopo Vingunguti kwa ajili ya kuchukua pesa za vyombo wakiwa na gari aina ya NOAH yenye namba T252 DAY rangi nyeusi.

        Ghafla walikuja watu wanaokadiriwa kufikia mia moja (100) na kulizingira gari hilo kwa makelele wakidai kuwa ndilo linalowateka wanafunzi. mtoa taarifa alipoona hali inakuwa tete alipiga simu Polisi na hatimaye watu hao waliokolewa na Polisi kisha kufikishwa katika kituo cha Polisi Buguruni wakiwa salama pamoja na gari lao.
Wanahabari mbalimbali wakimsikiliza kwa makini 
Pia mnamo tarehe 13.10.2014 majira ya saa 10:00 hrs huko katika kituo cha polisi Tabata uliibuka uvumi kuwa gari namba T548 BUN aina ya Noah rangi nyeusi ambayo ni mali ya askari polisi aitwaye A/INSP ESTAR wa kikosi cha usalama barabarani kituoni hapo ndani yake kuna vichwa vitano vya watoto wa shule ya msingi Mtambani na kusababisha wazazi wa watoto wanaosoma shuleni hapo na wananchi wengine kukusanyika kituoni hapo ili kushuhudia na kuona hivyo vichwa vitano,na ndipo mkuu wa kituo hicho cha Polisi Tabata aliamuru gari hilo kufunguliwa na kuwathibitishia wananchi kuwa habari hizo ni za uwongo na uvumi.

          Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es salaam linasisitiza kuwa uvumi huu wa kuwepo kwa kikundi cha wahalifu ambao wamekuwa wakiwateka watoto/wanafunzi hao si wa kweli hata kidogo na hivyo wananchi wanatakiwa kuepukana na taarifa hizo ambazo kwani zinaweza kusababisha uvunjifu wa amani.

          Aidha,uchunguzi wa kubaini ni nani aliyeeneza uvumi huo ulifanyika na kubainika kuwa uvumi na habari hizo zimeenezwa na mtu aitwaye GILBERT s/o STANLEY,(32) mhehe,mkulima,na mkazi wa Tabata ambaye alikamatwa muda mfupi tu baada ya tukio hilo na alipohojiwa alikiri kweli kueneza habari hizo na yeye aliambiwa na mtu mwingine ambaye hata hivyo alisema hamkumbuki.

 STORY NYINGINE KALI KUTOKA POLISI LEO ZIPO HAPO CHINI

 WATANO WAFARIKI, 16 WAJERUHIWA KATIKA AJALI YA MOTO BAADA YA LORI LA KUBEBA MAFUTA (PETROLI) KUPINDUKA.

        Kamishana wa Polisi Kanda maalum Dar es Salaam Suleiman H.Kova amethibitisha kutokea kwa vifo vya watu watano na wengine kumi na sita kujeruhiwa katika ajali ya moto iliyotokea juzi mnamo tarehe 13/10/2014 majira ya saa tano usiku huko Charambe round about Mbagala,baada ya lori aina ya Scania lenye namba za usajili T 347 BXG mali ya MOIL TRANSPORTER lililokuwa likisafirisha mafuta kuelekea Kampala Uganda, kuanguka likiwa na kemikali aina ya petrol lita 38,000 thamani yake inakadiriwa kuwa dola 36,000.

          Watu hao waliofariki ni 1.Masoud s/o Masoud (33) mkazi wa Charambe, 2. Hassan s/o Mohamed (25) mkazi wa Mbagala Kibangulile, 3.Mohamed s/o Ismail (19) mkazi wa Mbagala Charambe, 4.Ramadhani s/o Halfan (36) mkazi wa Mbagala Charambe na 5.Maulidi s/o Rajabu mkazi wa Mbagala Charambe.

         Majeruhi katika ajali hiyo ni 1.Hamis s/o Ally (35) mkazi wa mbagala kiburugwa, 2.Rajabu s/o Selemani (28) mkazi wa Tandika, 3.Idd s/o Said (28), 4.Janney s/o Mathayo (25) mkazi wa mbagala kizuiani,5.Mathayo s/o Daniel(21) mkazi wa mbagala charambe,6. Askari E.1028 CPL THOMAS alijeruhiwa na jiwe sehemu ya paji la uso wakati akijaribu kuzuia vibaka kuchota mafuta kabla ya kulipuka, aidha askari huyo alitibiwa na kuondoka, na majeruhi wengine 10 wamelazwa katika hospitali ya taifa ya Muhimbili na hospitali ya Wilaya Temeke wakiendelea na matibabu huku hali zao zikiwa si za kuridhisha.

           Aidha ajali hiyo ilisababisha pia kuungua kwa nyumba ya kulala wageni iitwayo United mali ya Deus Kasigwa (42) mfanyabiashara na mkazi wa Mtoni Mtongani,kuteketea kwa pikipiki saba za madereva wa bodaboda waliogesha karibu na eneo hilo pamoja na kuteketea kwa maduka yapatayo matano  ambapo vitu vilivyokuwemo kwenye maduka hayo  vinakadiriwa kuwa na thamani  ya  shilingi 197,000,000/=

JAMBAZI SUGU LAUWAWA NA POLISI KATIKA MAJIBIZANO YA RISASI LIKIWA NA BASTOLA AINA YA STAR ILIYOFUTWA NAMBA.

        Jeshi la Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam  kupitia makachero wa kikosi kazi mkoa wa Kinondoni(Task Force)_mnamo tarehe 14/10/2014 majira ya saa 06:45 hrs huko Chanika (W) Ilala lilifanikiwa kumkamata jambazi sugu aitwaye Paulo s/o Thomas Milanzi @Chinga,mmakonde,mkristo,hana kazi,miaka 35,mkazi wa Chanika.

           Kabla ya ukamataji jambazi huyo alianza kuwashambulia askari polisi kwa kufyatua risasi kwa bastola huku akikimbia na hatimaye askari polisi walijibizana nae na kumjeruhi kwa risasi maeneo ya mgongoni na baadaye kumkimbiza hospitali ya taifa Muhimbili kwa matibabu na baadaye madaktari walithibitisha kuwa amefariki.

Aidha jambazi huyo alikuwa akitafutwa na polisi kwa muda mrefu kuhusiana na matukio mbalimbali ya mauaji na unyang’anyi wa kutumia silaha jijini Dar es salaam na mikoa ya jirani.

 Baadhi ya matukio aliyowahi kufanya jambazi huyo ni 1. Tukio la tarehe 29/04/2014 lilitokea huko Airport kwenye taa za kuongozea magari akiwa na majambazi wenzake ambapo walimuua kwa kumpiga risasi Ofisa mwandamizi wa Usalama wa taifa SYLIVANUS s/o ADRIAN MZERU na kupora kiasi kikubwa cha fedha,2.Tukio la mnamo tarehe 21/02/2014 lililotokea maeneo ya Oysterbay katika barabara ya Haille sellasie karibu na Jackies Bar ambapo walivunja kioo cha gari aina ya Nissan Patrol iliyokuwa inaendeshwa na SYLIVANUS s/o ADRIAN MZERU na kupora pesa taslimu na laptop computer na wakati wanakimbia walimuua kwa kumpiga risasi ubavuni mlinzi wa kampuni ya KK security aitwaye FRANK s/o SILAYO,3.

            Tukio la mnamo tarehe 17/02/2014 lililotokea Kinondoni studio akiwa na wenzake ambao walishakamatwa wakitumia usafiri wa pikipiki walimvamia mfanyabiashara LUKAS s/o MONGI ambapo walifyatua risasi hewani kwa silaha walizokuwa nazo ambazo ni SMG na Bastola mbili kisha kumpora kiasi cha shilling 20,000,000/=.



KUPATIKANA KWA BHANGI GUNIA MBILI.
Jeshi la Polisi Kanda maalum Dar es Salaam mnamo tarehe 10/10/2014 majira ya saa nane mchana huko maeneo ya Kingugi Mbagala lilifanikiwa kumkamata mtuhumiwa aitwaye TREVER s/o LUCAS (18) mkazi wa Kingugi akiwa na bhangi gunia mbili, Aidha mtuhumiwa huyo anashikiliwa na polisi kwa mahojiano zaidi na pindi upelelezi utakapokamilika atafikishwa mahakamani.

POLISI WAKUSANYA MILIONI 336,450,000/= KWA MAKOSA YA USALAMA BARABARANI
    Jeshi la polisi kanda maalum kupitia kikosi chake cha usalama barabarani limefanikiwa kukusanya kiasi cha T.Shs. 336,450,000.00 (shilingi milioni mia tatu thelathini na sita na laki nne na hamsini elfu) kama tozo kwa makosa ya usalama mbalimbali
Kama ifuatavyo;

 1.Idadi ya magari yaliyokamatwa 3,097
2.idadi ya pikipiki zilizokamatwa 1,463
3.daladala zilizokamatwa 4,184
4.magari mengine binafsi na malori 2,471
5.jumla ya makosa yaliyokamatwa   11,215
Fedha za tozo zilizopatikana   Tsh 336,450,000/=

Aidha madereva wa vyombo vya usafiri wanatakiwa kufuata sheria na taratibu za usalama barabarani ili kuepukana na faini hizo ili waweze kujiendeleza katika familia zao na jamii kwa ujumla.

KUIMARISHA ULINZI MECHI YA YANGA NA SIMBA
Jeshi la Polisi Kanda Maalum limejipanga vyema kuimarisha ulinzi wakati wa mechi ya Simba na Yanga itakayochezwa tarehe 18/10/2014 kama ifuatavyo:-
1.    Mashabiki wanatakiwa kukaa katika sehemu zao kadiri ya tiketi walizokata
2.    Ni marufuku kwa mashabiki kuingia na silaha aina yoyote kwa mfano chupa za maji
3.    Mageti rasmi pekee yatumike kuingia uwanjani
4.    CCTV Camera zitatumika kuangalia na kutunza kumbukumbu kwa matukio yoyote yatakayojitokeza kabla, wakati na baada ya mchezo.
5.    Barabara zote zinazopita uwanja wa Taifa zitafungwa kwa muda mpaka yatakapotolewa maelekezo mengine.
Vitengo mbali mbali vya Polisi vitatumika kuhakikisha kwamba Amani na Utulivu vinatawala wakati wote wa mchezo huo.  Mashabiki wanatakiwa kuwa watulivu wakati wote wa mchezo na waheshimu maamuzi ya mwamuzi na utii wa sheria bila shuruti.




S. H. KOVA
KAMISHNA WA POLISI KANDA MAALUM

DAR ES SALAAM



No comments: