Friday, October 9, 2015

TANZIA--Mgombea ubunge Arusha Mjini Afariki dunia


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
 Ofisi ya Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, imepata msiba wa kuondokewa  na mmoja wa viongozi wake Estomih Jonas Mallah (Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Raslimali Taifa) aliyefariki  usiku wa kuamkia Oktoba 9 mwaka huu katika  Hospitali ya KCMC mkoani Kilimanjarao  alipokuwa akipatiwa matibabu.

Kiongozi wa Chama Ndugu Zitto Zuberi Kabwe anatoa  pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa, marafiki na wanachama  kwa ujumla kwa kuondokewa na kiongozi mchapakazi, mwadilifu, mzalendo na aliyekuwa na mapenzi mema na nchi yake.

Amemuelezea Marehemu Mallah kuwa mbali na kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Raslimali Taifa pia alikuwa mgombea Ubunge wa jimbo la  Arusha mjini  kwa tiketi ya Chama cha ACT-Wazalendo, Mwenyekiti wa kwanza wa Ngome ya wazee  Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Taifa.

Kutokana na Msiba huo Kamati ya Uongozi Taifa, imeagiza  kusimama kwa kampeni za ACT-Wazalendo kwa muda wa siku tatu kuanzia leo tarehe 09 Oktoba hadi Jumapili tarehe 11 Oktoba 2015. Aidha bendera za chama kwa nchi nzima zitapepea nusu Mlingoti kwa siku tano kuanzia leo Oktoba 9 – 13, 2015.

Akimuelezea   Marehemu Mallah,Zitto, alisema “Nilimtambua Mzee Estomih Mallah kwa misimamo yake ya kupigania usawa na amani tokea akiwa katika CHADEMA na hakuogopa kupoteza nafasi ya udiwani aliyokuwa akiishikilia kwa sababu ya kukataa kuyumbishwa”

Amesema Mallah amefariki akiwa anapigania ukombozi wa watu wa jimbo la Arusha mjini na kwamba ACT-Wazalendo itamuenzi   kwa kukemea yale maovu yote aliyoanza kukemea na  kuendeleza mema yote aliyoyaacha.

“ACT-Wazalendo  itaendelea kumkumbuka daima kwa busara zake na uongozi wake uliotukuka, alijitoa kulitumikia taifa bila ubaguzi wala upendeleo wowote, hivyo Chama kitamuenzi kwa kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni, 

Taratibu na Miongozo mbalimbali aliyoshiriki kuiasisi wakati wa uhai wake”
Oktoba 6 mwaka huu,  Mzee Mallah alishindwa kupanda jukwaani katika mkutano wa kampeni za mgombea Urais wa Chama cha ACT-Wazalendo, katika eneo la Ngaramtoni baada ya kujihisi kizunguzungu na kichwa kumuuma.
Baada ya hali hiyo alipelekwa katika hospitali ya St. Thomas alipopata mapumziko hadi jana Oktoba 8 alipohamishiwa hospitali ya KCMC.  

Mzee Mallah alifariki dunia wakati madaktari na wauguzi wakiendelea kumpatia huduma. Taratibu za mazishi zinaendelea nyumbani kwa marehemu.
Bwana ametoa, Bwana ametwaa, Jina la Bwana lihimidiwe.



Samson Mwigamba,
   KATIBU MKUU.

No comments: