Thursday, June 2, 2016

MADIWANI TEMEKE WAHIMIZA UKUSANYAJI WA KODI

MADIWANI, watendaji wa kata na wananchi wametakiwa kuhakikisha ukusanywaji wa kodi unafanywa unavyostahili ili Halmashauri ya Manispaa ya Temeke iweze kutoa fedha za mikopo ya kutosha.


Hayo yamesemwa leo na Abdallah Chaurembo, Mstahiki Meya wa halmashauri hiyo wakati wa kikao cha kupokea taarifa zilizotekelezwa katika robo tatu ya mwaka uliohudhuriwa na watendajki wa kata pamoja na madiwani.

“Fedha zinazokwenda katika mfuko wa akinamama na vijana ni asilimia kumi ya mapato ya ndani ya halmashauri, na kwamba kama ukusanyaji mapato utaongezeka ndivyo fedha za mikopo zitakapotolewa kwa wingi,” amesema Chaurembo na kuongeza;


“Ili fedha za mikopo zipatikane kwa wingi ni jukumu la watu wote kuhakikisha kuwa kodi inakusanywa, na kama kata haitakusanya mapato mengi haitapewa kipaumbele za kupata fedha nyingi za mkopo.”
Baraza la Madiwani wameridhia fedha hizo za mikopo kupitia katika Benki ya Bijamii ya Dar es Salaam (DCB) na kwamba, mikopo hiyo itatolewa kwa vikundi vya akina mama na vijana vya muunganiko wa watu watano.

Edmund Mkwawa, Meneja Mkuu wa DCB amesema kuwa, Manispaa ya Temeke imefanya jambo la muhimu kupitisha fedha hizo kwenye benki yao kwa kuwa itasaidia kuiboresha.
“DCB itahakikisha inatoa fedha kwa watu wanaostahili, pia tunaishukuru Manispaa ya Temeke kushirikiana na benki yetu ya jiji kwa kuwa ilianzishwa ili kuhochea maendeleo ya Dar es Salaam,” amesema.

No comments: