Friday, September 16, 2016

Kesi ya Zombe--Mmoja ahukumiwa Kunyongwa,ZOMBE aachiwa Huru




Mahakama ya Rufaa imemhukumu aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kinondoni, Christopher Bageni kunyongwa hadi kufa katika kesi ya vifo vya wafanyabiashara wa madini iliyokuwa ikimkabili yeye pamoja na aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam (RCO) Kamishna Msaidizi wa Polisi Abdallah Zombe na maofisa wenzake wawili.

Katika hukumu hiyo, Zombe na maafisa wengine wawili wameachiwa baada ya kushinda rufani hiyo dhidi yao.

Hukumu hiyo imehitimisha mvutano wa muda mrefu wa kisheria kati ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) na maofisa hao kwani baada ya kimya kirefu hukumu hiyo imetolewa.

Watuhumiwa wengine katika kesi hiyo walikuwa ni, aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Kituo cha Polisi Urafiki, Mratibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Ahmed Makelle na Rajabu Bakari.

Hukumu hiyo imekuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu, wakiwamo ndugu wa marehemu hao, wanasheria na jamii kwa jumla baada ya miezi minne, majuma mawili na siku mbili, tangu rufaa iliposikilizwa.

DPP alikata rufaa akipinga hukumu ya Mahakama Kuu iliyowaachia huru Zombe na wenzake wanane katika kesi ya mauaji ya wafanyabiashara wawili wa madini kutoka Mahenge, Morogoro na dereva wa teksi, mkazi wa Dar es Salaam.

Katika kesi ya msingi, Zombe na wenzake walidaiwa kuwaua kwa kukusudia wafanyabiashara Sabinus Chigumbi, maarufu Jongo na ndugu yake, Ephrahim Chigumbi, Mathias Lunkombe na Juma Ndugu, aliyekuwa dereva wa teksi wa Manzese.

Walidaiwa kutenda makosa hayo Januari 14, mwaka 2006, katika msitu wa Pande, uliopo wilayani Kinondoni baada ya kuwakamata wafanyabiashara hao Sinza, walipokuja Dar es Salaam kuuza madini.

Agosti 17, 2009, Mahakama Kuu iliwaachia huru washtakiwa hao ikisema baada ya kusikiliza ushahidi na hoja za mawakili wa pande zote iliridhika kuwa hawakuwa na hatia ya mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili.

Badala ya kosa la mauaji ambalo adhabu yake ni kunyongwa hadi kufaa, DPP aliiomba Mahakama imtie hatiani Zombe kwa kosa la kuwalinda wahalifu, ambao adhabu yake ni kifungo kisichozidi miaka saba jela.

Wakili wa Serikali Mkuu (PSA), Timon Vitalis alidai DPP alifikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha kuwa hakuna ushahidi wa kumtia hatiani Zombe kwa kosa la mauaji.

No comments: