Monday, May 8, 2017

LHRC WASIKITISHWA NA ONGEZEKO LA AJALI ZA BARABARANI NCHINI

TAARIFA KWA UMMA
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinasikitishwa kuona kiwango cha vifo vitokanavyo na ajali za barabarani nchini Tanzania kinazidi kupanda kulinganisha na nchi ambazo zipo salama zaidi na zenye magari mengi duniani. Kwa mujibu wa Ripoti ya Haki za Binadamu ambazo huchapishwa kila mwaka inakadiriwa kuwa watu 3,000 hupoteza maisha na 30,000 wanajeruhiwa vibaya barabarani kila siku duniani, huku kiwango kikubwa zikiripotiwa kutoka nchi zenye uchumi wa kati na wa chini ikiwemo Tanzania.  Tatizo la ajali za barabarani limekua tatizo kubwa la kiafya duniani kote, nchini Tanzania ajali za barabarani ni chanzo namba mbili cha jumla vifo vya watu ikiongozwa na ugonjwa wa malaria.

Mwenendo wa Takwimu za vifo vitokanavyo na ajali za barabarani sio wa kuridhisha hata kidogo, mwaka 2009 iliripotiwa jumla ya ajali 3,406 zilizosababisha vifo vya watu 502, mwaka 2010 kulikua na jumla ya ajali 4,363 zilizosababisha vifo vya watu 683, kwa kipindi chote hadi kufikia mwaka 2015 idadi ya vifo kwa mwaka imepanda kufikia vifo vya watu 3, 468 katika jumla ya ajali 8,337 kwa mwaka huo. Mwaka 2016 jumla ya watu 3,256 walipoteza maisha kwenye jumla ya ajali zote zilizotokea nchini. Idadi hiyo imepungua kwa jumla ya vifo vya watu 212 ukilinganisha na mwaka jana.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kupitia tafiti zake za kila mwaka huainisha sababu zinazochangia kukithiri kwa ajali za barabarani pamoja na kutoa mapendekezo kwa serikali kukabili tatizo la ajali za barabarani.  

Hatua mbali mbali zimechukuliwa kimataifa kwa kupitisha mikataba inayoweka vigezo vya kiusalama ili kupunguza tatizo la ajali za barabarani, kwa mujibu wa ibara 6(3) ya Mkataba juu ya Usafirishaji, Mawasiliano na Hali ya Hewa katika Kanda ya Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, 1996 ili inchi iweze kuyafikia malengo ya usalama barabarani nchi wanachama zilikubaliana kuanzisha sera itakayolenga kuoanisha sheria za usalama barabarani, kuchukua hatua za udhibiti kuhusiana na magari, madereva, na shuguli za barabarani pia kuonanisha na kutekeleza viwango husika vya utaalamu.
Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu kinatoa rai kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupita Wizara ya Mambo ya Ndani kuangalia upya na kufanya tathimini ya makubaliano ya mkataba huo kwa kuangalia Sheria, Sera na Kanuni za usalama barabarani ili kupunguza idadi ya  vifo vinavyoendelea kukithiri kutokana na ajali za barabarani.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinaendelea kusisitiza Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha usalama barabarani kusimamia misingi ya usalama wa magari pamoja na vyombo vingine vinavyotumia barabara kuzingatia kanuni za usalama barabarani.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinatoa mapendekezo yafuatayo kwa Jeshi la polisi kitengo cha usalama barabarani;
·         Kusimamia kanuni zinazoainisha idadi salama ya abiria kulingana na uwezo wa gari husika. Kwa mfano, ajali ya iliyotokea Arusha ilihusisha zaidi ya watu 30 kwenye gari aina ya coaster ambalo halina uwezo wa kubeba idadi hiyo kiusalama.
·         Kusimamia kanuni zinazotaka abiria na dereva kufunga mikanda ya usalama ndani ya gari.
·         Kutoa tahadhari za kiusalama wa mfumo wa usafirishaji kwa kuzingatia taarifa ya hali ya hewa. Ikiwemo kuzuia baadhi ya magari kusafiri kipindi ambacho hakuna uhakika na usalama wa barabara kwa sababu za hali ya hewa.
·         Kuhakikisha magari ya watu binafsi na ya abiria yanafuata taratibu za kuwa na bima ili kuweza kufidia abiria yanapotokea majanga ya ajali.
·         Kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kuhakiki ubora na usalama wa magari.
·         Kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kuhakiki weledi wa madereva wa magari.
·         Kusimamia kanuni zinazoweka taratibu za udhibiti wa mwendo kasi.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinatoa wito kwa Kamishna wa Bima kutengeneza hifadhi ya kanzidata kwa mambo yanayohusu bima za magari na kuanzisha mfuko wa kuwalipa fidia waathirika wa magari yasiyokatiwa bima.
Pia, serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kuboresha mifumo ya usafirishaji ikiwemo barabara kwa kuweka alama za tahadhari kwenye maeneo hatarishi. Maeneo hayo yanahusisha maeneo yenye kona kali, maeneo yenye miinuko mikali, maeneo yenye matuta ya barabarani, maeneo yenye madaraja, na maeneo yenye barabara mbovu au zinazoendelea kutengenezwa pamoja na maeneo yote hatarishi kwa usafirishaji wa abiria na mizigo.
Kupitia msiba huu mzito kwa taifa LHRC inaendelea kuungana na wananchi wote kwa kutoa pole kwa waathirika (majeruhi) wa ajali, familia, ndugu na Taifa kwa ujumla kwa ajali iliyotokea na zilizotokea kabla na baada ya ajali ya Arusha ndani ya kipindi hiki.
Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi.
Amina
Imetolewa leo tarehe 08/05/2017 na,           

Anna Henga,
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji
Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu

No comments: