Sunday, June 25, 2017

TAIFA STARS YAIBUKA KIDEDEA BAADA YA KUMPIGA MALAWI

TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, leo imeanza vema michuano ya Baraza la Vyama vya Soka la Nchi za Kusini mwa Afrika (Cosafa) kwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Malawi.

Katika mchezo huo uliopigwa kwenye Uwanja wa Moruleng uliopo Kaskazini Magharibi mwa Afrika Kusini, mabao yote ya Taifa Stara yalifungwa na Shiza Kichuya dakika ya 13 na 18 kipindi cha kwanza.

Kichuya alifunga bao la kwanza akiwa ndani ya eneo la 18 la Malawi akiunganisha kwa umakini krosi ya Simon Msuva, huku bao la pili akifunga kwa shuti kali akiwa nje ya eneo la hatari la Malawi baada ya kuukokota mpira kwa umbali kidogo kabla ya kuachia shuti hilo.
Taifa Stars ambayo inashiriki michuano hiyo ikiwa mgeni mwalikwa kwa kuwa si mwanachama wa Cosafa, imepangwa kundi A na timu za Mauritius, Malawi na Angola, huku Kundi B likiwa na timu za Msumbiji, Shelisheli, Madagascar na Zimbabwe.
Kinara wa kila kundi, atakwenda moja kwa moja hatua ya robo fainali ambapo huko ataungana na Botswana, Zambia, Afrika Kusini, Namibia, Lesotho na Swaziland.

No comments: