Wednesday, October 28, 2015

TANGAZENI MATOKEO YA WABUNGE HARAKA KUEPUSHA FUJO--TACCEO WATOA RAI

Mwenyekiti wa mtandao wa asasi zaidi ya 17 zinazoangalia chaguzi TACCEO Bi MARTINA KABISAMA akizungumza na wanahabari mapema leo Jijini Dar es salaam
 Mtandao wa asasi za Kiraia wa kuangalia chaguzi nchini Tanzania TACCEO ambao unaratibiwa na kituo cha sheria na haki za binadamu LHRC ambao ni waangalizi wa ndani wa uchaguzi  unaoendelea nchini wamewataka wasimamizi wa uchaguzi ambao bado hawajatangaza matokeo ya wabunge katika majimbo mbalimbali kufanya hivyo mara moja kwa kuwa ucheleweshaji wa matokeo hayo unaweza kusababisha vurugu na uvunjifu wa amani katika maeneo hayo.

Rai hiyo imetolewa leo Jijini Dar es salaam kupitia kwa mwenyekiti wa mtandao huo wa TACCEO Bi MARTINA KABISAMA wakati wakitoa tathmini ya uchaguzi huo hadi sasa ambapo amesema kuwa ucheleweshwaji wa kutangazwa kwa matokeo ya ubunge katika maeneo mbalimbali umekuwa ni changamoto kubwa ambayo imekuwa ikisababisha kutumika kwa nguvu ya polisi pamoja na vurugu kubwa kutokana na wananchi kukosa uvumilivu wa matokeo hayo.

Amesema kuwa kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi sura namba 343 ya sheria za Tanzania katika kifungu cha 8(a) inatamka kuwa msimamizi wa uchaguzi analazimika kutangaza matokeo ya uchaguzi mara moja pasipo kuchelewa baada ya kukamilisha kujumlisha kura hizo,huku akisema taarifa walizonazo kutoka kwa waaangalizi wao zinaonyesha kuwa kucheleweshwa kutangazwa kwa matokeo ni katika majimbo zaidi ya 21.
Kaimu Mkuruhenzi wa kituo cha sheria na haki za Binadamu LHRC Bi IMELDA LULU URIO akizungumza wakati wa kutoa report ya maendeleo ya uchaguzi wa mwaka huu nchini kwa mujibu wa waangalizi wao mbalimbali nchi nzima
Ametolea mfano baadhi ya majimbo ambayo tatizo hilo lilijitokeza na kusababisha taharuki kubwa kuwa ni Temeke,Ilala,Simanjiro,na Zanzibar ambapo kumekuwa na sababu mbalimbali zinazochangia ikiwemo wagombea kudai kurudiwa kuhesabu kura,wagombea kukataa kusaini,kupotea kwa baadhi ya nyaraka husika,kupotea kwa baadhi ya masanduku ya kura,kuchelewa kupokea vifaa kutokana na changamoto za kijografia,ambapo hali ya kuchelewa huko kumesababisha wananchi kukosa uvumilivu na kuhisi kuwa kuna mbinu chafu zinazofanywa na kuamua kufanya fujo ikiwemo kuchoma baadhi ya ofisi za serikali.


Aidha katika hatua nyingine mtandao huo umebaini kuwepo kwa matumizi makubwa ya nguvu za dola kutoka kwa polisi kwa wananchi wasio na hatia wanaofurahia matokeo yao ya ushindi,huku wakisema matumizi hayo ya nguvu yanawafanya hata raia wema kuzoea vurugu na fujo na kuona kama mchakato wa democrasia ni mchakato wa fujo na vurugu,ambapo amelitaka jeshi la polisi kuhakikisha linatenda haki kipindi hiki.

No comments: