MAADHIMISHO YA
SIKU YA KIMATAIFA YA KUPINGA UKEKETAJI
FEBRUARI 6,
2018
Tarehe 6
Februari kila mwaka ni siku ya kimataifa ya kupinga Ukeketaji duniani kote.
Historia ya siku hii ilianza mwaka 2003 ambapo Baraza la Umoja wa Mataifa
liliidhinisha kuwa siku rasmi ya kimataifa ya kupinga Ukeketaji duniani kote.
Baraza la Umoja wa Mataifa lilifikia uamuzi huu baada ya kutathimini na kuona
athari kubwa zitokanazo na vitendo vya ukeketaji kwa mtoto wa kike.
Kauli mbiu ya mwaka huu ni:
Pinga Ukeketaji, kwa Maendeleo ya Mwanamke na
Mtoto wa Kike!
Ukeketaji ni nini?
Ukeketaji ni kitendo cha kukata, kuvuta ama kuharibu kwa namna yoyote
ile kiungo cha ndani au cha nje cha uke wa mtoto wa kike. Tendo hili hufanywa
pasipokuwa na sababu zozote za kisayansi/kiafya. Ni kitendo kinachomdhalilisha
mtoto wa kike na kumwondolea utu wake kama mwanandamu aliyeumbwa kamili.
Historia ya utekelezaji wa mila hii potofu inasadikika kuanza yapata miaka 2000
iliyopita. Ukeketaji mara zote hufanyika kwa sababu ya misukumo ya kibinadamu,
ikiwemo kupata mali kwa kumwozesha binti aliyekeketwa, kutii masharti ya mila
kama ya kutambika mizimu, kuondoa mikosi katika familia, kumvusha mtoto rika na
nyinginezo nyingi. Hata hivyo sababu hizo zote hazina maana zaidi ya kuendeleza
tamaduni kandamizi kwa wanawake na watoto wa kike.
Madhara ya Ukeketaji
Yapo madhara mengi
yanayosababishwa na ukeketaji; madhara hayo yanaweza kuwa ya kiafya au hata
kisaikolojia. Madhara yanayosababishwa na ukeketaji yanaweza kuwa ya papo kwa
papo kama maumivu makali wakati wa ukeketaji, mshtuko, homa kali, kumwaga damu
nyingi na mara nyingine hata kupelekea kifo, kuambukizwa magonjwa kama Virusi
Vya UKIMWI na msongo wa mawazo. Yapo pia madhara ya muda mrefu kama vile; kuathirika
kisaikolojia, ulemavu/kovu la kudumu katika uke, fistula, kupata shida wakati
wa kujifungua na muda mwingine kupelekea kupata ugumba.
Jitihada za wadau
Pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali, Mashirika na
Taasisi mbalimbali bado ukeketaji umeendelea kutekelezwa katika baadhi ya jamii.
Kwa mujibu wa Takwimu za Taarifa ya Demographia na Afya ya 2012 zinaonyesha
kuwa pamoja na jitihada za kutokomeza vitendo hivyo, bado kuna mikoa mitano
inayoongoza kwa ukeketaji nchini ikiongozwa na Manyara wenye asilimia (58)
ukifuatiwa na Dodoma (47), Arusha (41), Mara (32) na Singida yenye asilimia
(31). Ziko sababu nyingi zinazosababisha, kuendelea kwa ukeketaji moja kati ya
hizo ni usiri mkubwa uliopo katika jamii husika. Jamii kwa kuamini kuwa
kukeketa ni mila na desturi zao, wameendelea kuhifadhi na kutunza siri za wale
wanaoendeleza vitendo hivyo, ili kuwaepusha wahusika na mkono wa dola. Hali hii
hupelekea watoto wa kike na wanawake kuendelea kunyanyasika bila msaada
Mtandao wa mashirika yanayopinga ukeketaji hapa nchini umeendelea
kusimama imara katika kuhahikisha kuwa ukeketaji unakoma ifikapo 2030 ili
kuendana na mikakati ya maendeleo endelevu ya kidunia ya kuondoa aina zote za
ubaguzi na ukatili dhidi ya wanawake na watoto na vilevile kuendana na mikakati
ya kitaifa kama ilivyoainishwa katika mpango kazi wa kitaifa wa kupinga vitendo
vyote vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto. Zipo juhudi kubwa zimefanyika
katika wilaya mbalimbali nchini ikiwemo miradi ya kutoa elimu na kusaidia
watoto wa kike kukabiliana na mila ya ukeketaji katika mikoa iliyotajwa. Kazi
ambazo zimekuwa zikifanywa na wanamtandao ni pamoja na Mafunzo kwa wazee wa
mila, ngariba, jeshi la polisi, mhimili wa mahakama, walimu, watoto, wazazi na
jamii kwa ujumla ambayo yameleta chachu katika kukuza na kuimarisha uelewa wa
kila mtu katika mapambano dhidi ya ukeketaji kwa watoto wa kike na wanawake..
Sambamba na hilo mtandao unafanya kazi kuwezesha wahanga wa ukeketaji kufikia
vyombo vya kisheria ikiwemo polisi na mahakama ili kuwachukulia hatua wale wote
wanaendeleza mila hii kandamizi.
Serikali imeendelea kuboresha sheria na sera mbalimbali ili kupanua wigo wa
adhabu kwa wale wanaoendelea kutekeleza kitendo hicho cha kikatili. Kwa mfano mabadiliko ya Sheria ya
Mtoto (2009) yamelenga pamoja na mambo mengine kupanua adhabu na kutengeneza
mnyororo mpana wa washiriki. Maboresho ya Sheria ya Kanuni ya Adhabu (2002)
nayo yamepanua uwanda wa kutoa adhabu na kubaini kipimo cha ushiriki wa
mtuhumiwa katika kufanya ukeketaji.
Sera mbalimbali za kitaifa ikiwemo Sera ya Elimu ya 2015 inapinga kila
aina ya unyanyasaji kwa mtoto wa kike na inaweka na kutambua misingi ya haki na
usawa kwa watoto wote wa kike na wa kiume. Sera hii pia imelenga kuondoa
ubaguzi na unyanyasaji kwa mtoto wa kike.
Serikali ya Jamhuri ya Mungano pia imeendelea kuridhia na kutekeleza
sera na sheria mbalimbali za kimataifa zinazolenga kutokomeza ukeketaji na
unyanyasaji kwa mtoto wa kike. Tanzania imeridhia mkataba wa kimataifa wa
Kupinga aina zote za Ukatili kwa wanawake CEDAW wa mwaka 1979 na mikataba mingine
mingi. Kuendelea kutumika kwa sheria hizi za kimataifa na kikanda kumezidi
kutanua wigo wa sheria na uwajibikaji wa kitaasisi katika kulinda masilahi ya
mtoto wa kike dhidi ya ukeketaji.
Wadau wengine kama Jeshi la Polisi, Mahakama, taasisi za kidini na
viongozi wa kimila wameonyesha nia na jitihada kubwa katika kuunga mkono
kampeni za kutokomeza ukeketaji nchini.
Nini kifanyike ili kutokomeza kabisa
ukeketaji?
Mbali na jitihada kubwa zinazochukuliwa na wadau kutokomeza ukeketaji
nchini, bado kuna mambo kadhaa ya kufanya ili kuondosha kabisa mila hii potofu
katika jamii zetu.
1.
Serikali
kusimamia kikamilifu sheria kuhakikisha watekelezaji wa vitendo vya ukeketaji
wanakamatwa na kuwajibishwa kwa mujibu wa sheria za nchi. Serikali ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania idumishe ushirikiano na taasisi zisizo za kiserikali
pamoja na mashirika rafiki ya kimataifa ili kwa pamoja tuweze kutokomeza
ukeketaji na ukandamizaji kwa mtoto wa kike na wanawake.
2.
Jamii
inapaswa kuungana na kukemea kwa nguvu vitendo vya ukeketaji na kutoa
ushirikiano kwa vyombo vya dola ikiwemo kutoa taarifa na ushahidi ili
kufanikisha vita dhidi ya ukeketaji na ukatili wa kijinsia kwa ujumla.
3.
Wadau
waongeze juhudi katika kuzifikia jamii zinazotekeleza mila ya ukeketaji kwa
elimu na kwa msaada wa moja kwa moja ili kutokomeza janga hili.
Imetolewa na Mtandao wa Kupinga Ukeketaji
Tanzania
Mtando wa mashirika yanayopinga ukeketaji Tanzania unaundwa na
mashirka yafuatayo:
1.
Children
Dignity Forum (CDF)
2.
Tanzania
Media Women’s Association (TAMWA)
3.
Tanzania
Women’s Lawyers Association (TAWLA)
4.
Legal and
Human Rights Center (LHRC)
5.
Christian
Council of Tanzania (CCT)
6.
World Vision
Tanzania (WVT)
7.
Baraza Kuu
la Waislamu Tanzania (BAKWATA)
8.
Network
Against Female Genital Mutilation (NAFGEM)
9.
Women Wake
Up (WOWAP)
10.
Anti-Female
Genital Mutilation Network (AFNET)
11.
Dodoma
Inter - African Committee (DIAC
No comments:
Post a Comment