Tuesday, November 29, 2016

ACT WAZALENDO WAMSHTAKI RC MAKONDA TUME YA MAADILI


TUME YA MAADILI IMUWAJIBISHE RC MAKONDA KWA   UDHALILISHAJI    WA WATUMISHI    NA WANANCHI.                 

                                     
NGOME  ya Wanawake ya Chama cha ACT Wazalendo imeshtushwa na kuhuzunishwa na kauli zisizo za kiuongozi na zsizozingatia kanuni za Maadili ya Utumishi wa Umma zinazoendelea kutolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda.

Jana, katika mkutano anaouita wa kutatua kero kwa wakazi wa Dar esSalaam , Bwana Makonda ameendelea kushindwa kutatua kero na badala yake kuongeza kero ya kudhihaki, kudhalilisha kukejeli na kutukana hadharani wananchi anaowaongoza na watumishi anaowasimamia kitendo ambacho ni kinyume na maadili ya Watanzania.

Kitendo cha Mkuu wa Mkoa Makonda  akiwa katika eneo la Mabwepande, Wilaya ya Kinondoni Mkoani Dar es Salaam kumtolea lugha ya udhalilishaji Afisa Ardhi wa Manispaa ya Kinondoni Bi Rehema Mwinuka kwa kumtamkia kuwa; *"Hawa ndio vichaa tunaohangaika nao, toka hapa".* hakikubaliki na kimetusikitisha Sana na tunakilaani kwa nguvu zetu zote.


Kauli kama hii sio tu haikupaswa kutolewa na kiongozi mkubwa katika ngazi ya Mkoa lakini pia ni kauli mbaya ambayo ililenga kumdhalilisha na kumvunjia heshima yake mbele ya umma Bi Rehema Mwinuka.

Kutokana na udhalilishaji huo uliofanywa Mkuu wa mkoa wa Dar esSalaam, sisi  Ngome ya Wanawake wa Chama cha  ACT Wazalendo, Leo Jumanne, Novemba 28/2016 tumepeleka mashtaka rasmi dhidi ya Mkuu wa Mkoa huyo mbele ya Tume ya maadili ya viongozi wa umma na utawala bora kuwataka wamuwajibishe kwa kitendo chake hicho cha utovu wa nidhamu na maadili ya utumishi wa umma.

Ngome ya Wanawake ACT Wazalendo inamtaka pia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam atambue kuwa kwa kuzingatia Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2002 pamoja na Kanuni za Maadili ya Utumishi wa Umma, kanuni ya 65(1) inamtaka mtumishi wa umma;

_"kuepuka kufanya vitendo viovu au kutamka maneno yanayolenga kuwaaibisha watumishi wa ngazi moja, za chini yao au wa vyeo vya juu"._

Alichofanya Mkuu wa Mkoa ni kumuaibisha na kumtolea lugha ya udhalilishaji Bi Rehema Mwinuka kinyume cha Sheria na Kanuni za Utendaji katika Utumishi wa Umma.
Ngome ya Wanawake ACT Wazalendo inaitaka Tume ya Maadili na Utawala Bora ifanye uchunguzi na kuchukua hatua dhidi ya matamshi mbalimbali yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ambayo yalikiuka sheria ya Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma.

Ngome ya Wanawake ACT Wazalendo inayataka pia Mashirika na Asasi mbalimbali zinazosimamia Haki za Binaadamu, Haki za Jinsia na Utawala Bora kupaza sauti dhidi ya kauli isiyo ya kiuongozi iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa dhidi ya Afisa Ardhi wa Manispaa ya Kinondoni Bi Rehema Mwinuka.

Kadhalika,  Ngome na Chama kwa ujumla tutaendelea kuwasemea wanyonge wote popote walipo kwa kadri ya uwezo wetu.
Imetolewa na:
Esther Kyamba,
Katibu,
Ngome ya Wanawake 
ACT Wazalendo.

No comments: