Sunday, February 26, 2017

RAIS MAGUFULI AMTEUA NUNDU KUWA MWENYEKITI WA BODI YA TTCL,AMWAPISHA ANDENGENYE KUWA KAMISHNA JENERALI JESHI LA ZIMAMOTO NA UOKOAJI

SeeBait
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, amemteua Bw. Omary Rashid Nundu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL).

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi imeeleza kuwa uteuzi wa Bw. Omary Rashid Nundu umeanza tarehe 24 Februari, 2017.

Bw. Omary Rashid Nundu anachukua nafasi ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL Prof. Tolly Salvatory Augustine Mbwete.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amemuapisha Thobias Emir Andengenye kuwa Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Kamishna Jenerali Thobias Emir Andengenye anachukua nafasi ya Kamishna Jenerali Pius M. Nyambacha ambaye amestaafu.

Pia, Mhe. Rais Magufuli amewaapisha Mabalozi wanne walioteuliwa kuiwakilisha Tanzania katika nchi mbalimbali kama ifuatavyo;

Mhe. Dkt. Pindi Hazara Chana ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Nairobi, Kenya ambako anachukua nafasi ya Mhe. John Haule ambaye amestaafu.

Mhe. Silima Kombo Haji ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Khartoum, Sudan ambako anakwenda kufungua Ubalozi.

Mhe. Abdallah Abas Kilima ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Muscat, Oman ambako anachukua nafasi ya Mhe. Ali Ahamed Saleh ambaye amestaafu.

Mhe. Matilda Swila Masuka ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Seoul, Korea Kusini ambako anakwenda kufungua Ubalozi mpya

Aidha Mhe. Rais Magufuli ameshuhudia Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Mabalozi wote wanne wakila kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa ummakilichoongozwa na Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Mstaafu Harold Nsekela.

Hafla ya kuapishwa kwa viongozi hao imehudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Pindi Chana kuwa Balozi wa Tanzania nchini Kenya, tukio lililofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Silima Kombo Haji kuwa Balozi wa Tanzania nchini Sudani, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Abdallah Kilima kuwa Balozi wa Tanzania nchini Oman, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Matilda Masuka kuwa Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Thobias Andengenye akila kiapo cha Ahadi ya Uadilifu pamoja na Mabalozi Pindi Chana, Balozi Silima Kombo Haji, Abdallah Kilima pamoja na Balozi Matilda Masuka mara baada ya kuapishwa Ikulu jijini Dar es Salaam.

PICHA NA IKULU

No comments: