Tuesday, March 7, 2017

Mashirika ya TGNP Mtandao ,Oxfam na Care International yaungana katika maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani

Mkurungezi wa TGNP  Lilian Liundi (katikati) akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kutangaza uzinduzi wa kauli mbiu ya ya mwaka huu "Kuwa Jasiri, PingaUkatili Dhidi ya Wanawake” Katika kuadhamisha siku ya wanawake duniani tarehe 8 Machi ambapo  maadhimisho hayo yatafanyika kimkoa  katika viwanja vya MwembeYanga Temeke Jijini Dar es salaam, Pembeni yake kushoto ni Mkuu wa kitengo cha ushawishi Oxfam Eluka Kibona ,na kulia ni  Mkurungezi wa  wanawake wa Basketball Dar es salaam Bainasi Wamunza na mwishoni ni Makamu mwenyekiti wa Chaneta Bi Zainab Mbiro 


Mkuu wa kitengo cha ushawishi Oxfam  Eluka Kibona akisisitiza jambo wakati wa mkutano na waandishi wa habari wakati wa kutangaza uzinduzi wa kauli mbiu ya ya mwaka huu "Kuwa Jasiri, PingaUkatili Dhidi ya Wanawake” Katika kuadhamisha siku ya wanawake duniani tarehe 8 Machi ambapo  maadhimisho hayo yatafanyika kimkoa  katika viwanja vya MwembeYanga Temeke Jijini Dar es salaam,Kulia kwake ni Mkurungezi wa TGNP  Lilian Liundi.

Wawikilishi kutoka mashirika yasiyo ya Kiserikali ya Oxfam nchini Tanzania, Care International na TGNP Mtandao wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa   ya mwaka huu "Kuwa Jasiri, PingaUkatili Dhidi ya Wanawake” Katika kuadhamisha siku ya wanawake duniani tarehe 8 Machi ambapo  maadhimisho hayo yatafanyika kimkoa  katika viwanja vya MwembeYanga Temeke
 Jijini Dar es salaam,
Waandishi wa habari wakichukua habari katika mkutano huo uliofanyika katika makao makuu ya TGNP Mtandao Mabibo Jijini Dar es salaam
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar-Es-Salaam kwa kushirikiana na mashirika yasiyo ya Kiserikali ya Oxfam nchini Tanzania, Care International na TGNP Mtandao, kwa pamoja  tunaandaa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani kwa mwaka 2017. Siku ya wanawake duniani kote huadhimishwa kila mwaka tarehe 8 ya mwezi Machi. Tunaadhimisha siku hii maalumu kila mwaka ili kusherekea, kuheshimu, kukubali na kutambua mchango na mafanikio ya wanawake duniani kote katika kuinua na kuendeleza nyanja mbalimbali za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Siku hii pia inatumika kutathmini na kutafakari changamoto anazokabiliana nazo mwanamke katika Nyanja zote muhimu za maisha yake.



Kila mwaka maadhimisho haya yanakuwa na dhima maalum ambako kidunia dhima ni “Kuwa Jasiri kuleta Mabadiliko” wakati dhima ya kitaifa ni “Tanzania ya Viwanda, Wanawake ni Msingi wa Mabadiliko  ya kiuchumi”.  Sambamba na dhima hizi sisi kama taasisi zinazohusika na masuala ya haki za wanawake na usawa wa kijinsia nchini, tunaamini kwamba ukatili wa kijinsia ni moja ya vikwazo vikubwa kwa wanawake vinavyowakwamisha kuchangia kikamilifu katika shughuli za maendeleo ikiwemo kushika nafasi za maamuzi na kumiliki rasilimali.  Ukatili wa Kijinsia hauwezi kuisha bila madadiliko makubwa katika maisha yetu ya kila siku, mila na tamaduni zetu pamoja na sera na sheria zetu. Ni kwa muktadha huo tumekuja na kauli mbiu isemayoni, “Kuwa Jasiri, Pinga Ukatili Dhidi ya Wanawake”.
Kaulimbiu hii inalenga kuhamasisha jamii, serikali na makundi mbalimbali na mtu mmoja kuchukua hatua katika kuzuia na kudhibiti ukatili dhidi ya wanawake. Ikumbukwe kuwa wanawake ambao ni zaidi ya asilimia 50 ya watanzania wote, wamekuwa wakikosa nafasi na sauti  ya kufanya maamuzi kutokana na mifumo kandamizi kwenye jamii zetu ukiwemo mfumo dume. Tunaamini na kutoa wito kwa wadau mbalimbali kusimama kwenye nafasi zao kupinga aina zote za ukatili kwa wanawake na watoto wa kike ikiwemo ndoa za utotoni ambazo bado ni changamoto na zimeongezeka kwa 4% kutoka 23% 2010 mpaka 27% 2015, huku wasichana 36 kati ya 100 wakipata mimba katika umri mdogo, rushwa ya ngono na aina nyingine za ukatili ambazo zinamzuia mwanamke na mtoto wa  kike kufikia ukombozi wa kiuchumi.
Ni dhahiri kwamba suala la kupinga ukatili wa kijinsia linahusisha rasilimali kwa kiasi kikubwa. Pamoja na juhudi za serikali kuandaa na kuzindua Mkakati wa kitaifa wa kupinga ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto mnamo mwezi Disemba mwaka 2016, tunatoa wito kwa watendaji hususan ngazi ya Halmashauri kuhakikisha fedha zinatengwa na kuelekezwa katika kutekeleza mkakati huo kama ilivyoelekezwa na Waziri wa  Fedha Mh. Philp Mpango wakati wa uzinduzi wa mpango mkakati huo.
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kimkoa kwa mwaka huu yatafanyika katika viwanja vya Mwembe Yanga vilivyopo Temeke  kwa kukusanyika katika viwanja hivyo kuanzia saa 1:30 asubuhi na kisha kufuatiwa na maandamano mafupi ya amani yatakayofanyika katika viwanja hivyo hivyo vya Mwembe Yanga. Mkusanyiko huo utahusisha wimbo mfupi na ugawaji wa vipeperushi kwa washiriki watakaohudhuria. Mgeni rasmi katika shughuli hii anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam
Tunachukua fursa hii kuwapongeza wanawake wote Tanzania na kuwatia moyo katika kupigania haki na usawa wa wanawake.

No comments: