Wednesday, June 29, 2022

Shirika la Posta Tanzania limesaini Mkataba wa kusafirisha Sampuli za Kibailojia na kampuni ya TUTUME.

Na. Vicent Macha Dsm

Shirika la posta nchini pamoja na Kampuni ya kusafirisha mizigo ya TUTUME wamepongezwa kwa ubunifu wa kushirikiana kuhakikisha watanzania hawakosi huduma muhimu za afya.

Pongezi hizo zimatolewa na Waziri wa Habari, Mawasialiano na Teknolojia ya Habari Mh. Nape Moses Nauye alipoalikwa kushuhudia utiaji saini wa mkataba wa usafirishaji wa sampuli za kibaiolojia baina ya shirika hilo pamoja na kampuni hiyo.

Aidha amesema kuwa kama lilivyo lengo la serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan la kusogeza huduma mbalimbali karibu na wananchi hivyo mikataba hiyo itasaidia sana kupanua huduma hizo hasa katika upende wa Afya.

Ameongeza kuwa licha ya kuwa mkataba huo unalenga sekta lakini angalieni pia katika maeneo mengine ambayo mnaweza kushirikiana na mkiangalia wote mnafanya kazi ya aina moja hivyo mkiongeza mashirikiano katika vitu vingi mtaweza kuwasaidia watanzania kwa sehemu kubwa sana.

Amemalizia kwa kuwataka TUTUME, Shirika la Posta pamoja na wote wanaotoa huduma za kusafirisha bidhaa kuweza kuutumia vizuri mfumo wa anuwani za makazi ili kurahisisha ufanyaji wao wa kazi, na pia amewaomba Wizara ya Afya ikiwezekana kuwafuata watu majumbani kuchukua sampuli na kutuma kwa mashirika haya na baadae kuwarudishia pia majibu kupitia wasafirishaji hao hao.

kwa upande wake Posta Masta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania (TPC) Macrice Mbodo amesema kuwa mkataba huo waliyosaini na Kampuni ya TUTUME ni wa kiuwakala wa kusambaza Sampuli mbalimbali za Mahabara

Ameongeza kuwa majukumu ya TUTUME, itakuwa ni kuchukua Sampuli kutoka katika ngazi ya kwanza ya Mahabara na kupeleka ngazi ya pili ya Mahabara na wao Shirika la Posta kazi yao itakuwa ni kutoa ngazi ya pili na kupeleka katika Mahabara za uchunguzi na baadae muhusika kupelekewa majibu yake.

Ameendelea kusisitiza kuwa Shirika la Posta limekuwa likitoa huduma za kusafirisha mizigo kwa njia mbili yaani njia ya haraka pamoja na kawaida, Na kuongeza kuwa mpaka sasa shirika hilo limetoa ajira ya uwakala kwa vijana wa boda boda zaidi ya 450.

Naye Mkurugenzi wa Kampuni ya Tutume, Misana Manyama amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi zinapohitaji kushirikiana na idara za Serikali ili kuweza kuleta maendeleo katika nchi yetu. 

Ameongeza kwa kusema kuwa waoa kama TUTUME, wataifanya kazi hiyo kwa uadilifu na weledi mkubwa sana, na kutii masharti yale yote yaliyopo kwenye mkataba huo na kwamba wao wanauzoefu wa kutosha katika kazi hiyo kwani walikwisha ifanya hapo nyuma na wanaendelea kuifanya na kuongeza kuwa mpaka sasa wanavijana wa boda boda zaidi ya 1450 nchi nzima.

HABARI PICHA.
Waziri wa Habari, Mawasialiano na Teknolojia ya Habari Mh. Nape Moses Nauye katika zoezi la kusaini mkataba kati ya shirika la Posta na Kampuni ya TUTUME.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Jim Yonaz akitoa neno katika zoezi la uwekaji saini mkataba wa kusafirisha Sampuli za kibaiolojia.
Posta Masta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania (TPC) Macrice Mbodo akiongea katika zoezi la kusaini mkataba kati ya shirika la Posta na Kampuni ya TUTUME.
Mkurugenzi wa Kampuni ya TUTUME, Misana Manyama akiongea namna watakavyoshirikiana na Shirika la Posta nchini kuweza kusafirisha sampuli za kibaiolojia.
Zoezi la utiaji wa saini likiendelea kati ya Shirika la Posta nchini na Kampuni ya TUTUME, zoezi lililofanyika mapema jana Mkoani Dar es salaam.






No comments: